Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utangulizi

Biblia Takatifu ni ujumbe wa Mungu ulioandikwa kwa ajili yetu sote. Ni lazima tujifunze Biblia ili tumjue Mtungaji wake. (Yohana 17:3; 2 Timotheo 3:​16) Katika Biblia, Yehova Mungu hufunua kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na kwa ajili ya dunia, makao ya wanadamu.​—⁠Mwanzo 3:​15; Ufunuo 21:​3, 4.

Hakuna kitabu kingine chochote kilicho na nguvu za kubadili maisha ya watu kama Biblia. Biblia hutuchochea kutafakari kuhusu sifa za Yehova kama vile upendo, rehema, na huruma. Huwapa watu tumaini na kuwasaidia kuvumilia hata mateso makali sana. Nayo inaendelea kufunua mambo ya ulimwengu huu yasiyopatana na mapenzi makamilifu ya Mungu.​—⁠Zaburi 119:105; Waebrania 4:​12; 1 Yohana 2:​15-​17.

Mwanzoni Biblia iliandikwa katika lugha ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki, lakini sasa imetafsiriwa, ikiwa nzima au kwa sehemu, katika lugha 2,600 hivi. Ndicho kitabu kilichotafsiriwa katika lugha nyingi zaidi na kusambazwa kwa wingi sana katika historia. Na jambo hilo halitushangazi. Unabii wa Biblia unasema hivi: “Hii habari njema ya Ufalme [ambao ndio ujumbe wa msingi wa Biblia] itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”​​—⁠Mathayo 24:14.

Kwa kuwa tunatambua umuhimu wa ujumbe wa Biblia, tumeboresha tafsiri hii tukiwa na heshima kubwa sana kuelekea ujumbe wa Biblia. Tunatambua kwamba tuna wajibu mzito sana wa kuwasilisha ujumbe wake kwa usahihi. Toleo hili lililorekebishwa linategemea msingi mzuri uliowekwa na matoleo ya awali ya New World Translation of the Holy Scriptures, Biblia iliyotolewa kwa mara ya kwanza zaidi ya miaka 60 iliyopita. Hata hivyo, lugha ya Kiingereza imebadilika katika muda wa miaka 50 iliyopita. Mabadiliko hayo ndiyo yaliyofanya washiriki wa sasa wa Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mpya waanze kazi kubwa ya kuiboresha. Lengo letu lilikuwa kutayarisha tafsiri inayowasilisha kwa uaminifu mawazo ya maandishi ya awali na ambayo inaeleweka na kusomeka kwa urahisi. Makala za Nyongeza zenye kichwa “Kanuni za Kutafsiri Biblia,” “Sehemu za Toleo Hili,” na “Jinsi Biblia Ilivyotufikia” zinazungumzia baadhi ya mambo yaliyoboreshwa katika toleo hili kuhusiana na lugha.

Wale wanaompenda Yehova Mungu na kumwabudu wanatamani kuwa na tafsiri sahihi na inayoeleweka ya Neno la Mungu. (1 Timotheo 2:4) Kwa hiyo, tumetoa toleo hili lililorekebishwa katika Kiingereza tukikusudia litafsiriwe katika lugha nyingi iwezekanavyo. Tunatumaini na kusali kwamba, wewe msomaji mpendwa, utanufaika na toleo hili la Maandiko Matakatifu unapojitahidi ‘kumtafuta Mungu na kwa kweli umpate.’​​—⁠Matendo 17:27.

Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mpya

Agosti 2013

Biblia Takatifu​—⁠Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kiswahili ilitolewa mwaka wa 2003. Toleo hili la Kiswahili la mwaka wa 2017 ambalo ndilo la karibuni zaidi limerekebishwa kwa kutegemea Biblia ya Kiingereza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa mwaka wa 2013, na lina sehemu zote zilizo katika tafsiri ya Kiingereza.