Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 A2

Sehemu za Toleo Hili

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kiingereza mwaka wa 1950, na toleo zima la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya lilichapishwa mwaka wa 1961. Tangu wakati huo makumi ya mamilioni ya wasomaji katika lugha zaidi ya 120 wamefaidika na tafsiri hii sahihi na inayosomeka ya Maandiko Matakatifu iliyotafsiriwa kutoka kwa lugha za awali.

Halmashauri ya sasa ya Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatambua uhitaji wa kutumia lugha inayogusa mioyo ya wasomaji wa kisasa. Kwa sababu hiyo, kanuni kadhaa za muundo na msamiati zilifuatwa katika tafsiri hii ili kutimiza mambo yafuatayo:

  • Kutumia lugha ya kisasa na inayoeleweka. Kwa mfano, neno “ustahimilivu” linaweza kueleweka kimakosa kumaanisha “mtu anayeteseka kwa muda mrefu.” Hata hivyo, wazo linalokusudiwa ni kujizuia kwa hiari, ambalo linatokezwa vizuri zaidi kwa kutumia neno “subira.” (Wagalatia 5:22) Katika toleo hili, maneno “karamu za kupindukia” yametafsiriwa kuwa “karamu zenye vurugu.” (Wagalatia 5:19-21) Maneno “wakati usio na kipimo” yaliondolewa na badala yake maneno kama vile “milele,” “kudumu,” “zamani za kale” yakatumiwa ili kutokeza maana iliyokusudiwa katika kila muktadha.—Mwanzo 3:22; Kutoka 31:16; Zaburi 90:2; Mhubiri 1:4; Mika 5:2.

    Katika Kiebrania na Kigiriki cha kale neno “mbegu” linaweza kumaanisha mbegu ya mmea na pia uzao wa wanadamu, au wazao, au shahawa. Kwa kuwa si kawaida katika lugha ya Kiswahili kutumia neno “mbegu” kurejelea wanadamu, neno hilo liliondolewa na badala yake maneno yanayotokeza maana inayokusudiwa yakatumiwa kulingana na muktadha. (Mwanzo 1:11; 22:17; 48:4; Mathayo 22:24; Yohana 8:37) Mara nyingi, neno “uzao” sasa linatumiwa kurejelea ahadi iliyotolewa katika Edeni, kwenye Mwanzo 3:15.

  • Maneno yaliyo katika Biblia yafafanuliwa. Katika matoleo yaliyotangulia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza, neno la Kiebrania neʹphesh na neno la Kigiriki psy·kheʹ kila mara yalitafsiriwa kuwa “nafsi.” Kwa sababu ya maoni mengi yasiyo ya kweli kuhusu maana ya neno “nafsi,” mbinu hiyo ilimsaidia msomaji kuelewa jinsi waandikaji wa Biblia walioongozwa na roho ya Mungu walivyotumia maneno hayo ya lugha ya awali. Ikitegemea muktadha, maneno hayo yanaweza kumaanisha (1) mtu, (2) uhai wa mwanadamu, (3) viumbe walio hai, (4) tamaa na hamu ya mtu au, mara nyingine, (5) hata watu waliokufa. Hata hivyo, kwa kuwa matumizi kama hayo ya neno “nafsi” si ya kawaida katika Kiswahili, uamuzi ulifanywa ili kutafsiri maneno hayo ya lugha ya awali kulingana na maana iliyokusudiwa, mara nyingi yakiwa na maelezo ya chini yanayosema “Au ‘nafsi.’” (Kwa mfano, angalia, Mwanzo 1:20; 2:7; Mambo ya Walawi 19:28; Zaburi 3:2; Methali 16:26; Mathayo 6:25.) Hata hivyo, katika mashairi na mistari inayojulikana, neno “nafsi” limedumishwa, pamoja na maelezo ya chini yanayoelekeza kwenye Kamusi au yanayoonyesha maana nyingine.—Kumbukumbu la Torati 6:5; Zaburi 131:2; Methali 2:10; Mathayo 22:37.

    Vivyo hivyo, neno figo lilidumishwa linaporejelea kiungo halisi. Hata hivyo, linapotumiwa kwa njia ya mfano kama vile kwenye Zaburi 7:9 na 26:2 na Ufunuo 2:23, wazo lililokusudiwa la “hisia za ndani kabisa” au “mawazo ya ndani kabisa” limeandikwa kwenye mstari, na tafsiri ya neno kwa neno kwenye maelezo ya chini.

    Kama ilivyo katika Kiebrania na Kigiriki, neno la Kiswahili “moyo” lina maana halisi na maana ya mfano, basi mara nyingi lilidumishwa katika mistari. Hata hivyo, katika sehemu chache ambapo maana haikueleweka, ujumbe ulitafsiriwa kwa njia iliyo wazi zaidi. Kwa mfano, katika kitabu cha Methali, maneno “aliyepungukiwa moyoni” sasa yametafsiriwa kuwa “asiye na busara,” nayo tafsiri ya neno kwa neno imewekwa kwenye maelezo ya chini. Maneno mengine, kama vile, “unono,” “mwili,” na “pembe,” yalishughulikiwa kwa njia hiyo, kulingana na muktadha. (Mwanzo 45:18; Mhubiri 5:6; Ayubu 16:15) Baadhi ya maneno hayo yanafafanuliwa katika “Kamusi ya Maneno ya Biblia.”

  • Kusomeka kwa urahisi. Katika matoleo yaliyotangulia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, vitenzi visaidizi vilitumiwa kuonyesha ikiwa kitenzi cha Kiebrania kilikuwa kimekamilika au la. Kwa mfano, kitendo kinachoendelea ambacho mara nyingi huelezwa kwa kutumia kitenzi ambacho hakijakamilika, kilionyeshwa kwa kutumia maneno kama “akaendelea,” “ikawa,” na kadhalika. Mkazo ambao mara nyingi huwasilishwa na kitenzi cha Kiebrania kilichokamilika ulionyeshwa kwa kuongezea maneno “kwa hakika,” “lazima,” na maneno kama hayo. Kwa hiyo, maneno hayo yalitumiwa mara nyingi sana katika maandishi. Katika toleo hili, vitenzi visaidizi vilidumishwa katika sehemu fulani kwa kutumia maneno kama vile “kuendelea,” na “alizoea” kulipokuwa na sababu za msingi za kuonyesha kitendo kinachoendelea. (Mwanzo 3:9; 34:1; Methali 2:4) Hata hivyo, yaliondolewa ili kurahisisha usomaji wakati vitenzi visaidizi havikuhitajiwa katika kuwasilisha maana iliyokusudiwa mwanzoni.

  • Kuwasilisha mawazo sahihi ya maneno yanayohusu jinsia. Maneno ya Kiebrania na Kigiriki huonyesha jinsia ya kiume au ya kike, na katika Kigiriki, pia kuna maneno yasiyo na jinsia. Hata hivyo, nyakati nyingine, kuonyesha jinsia ya maneno ya lugha ya awali kunaweza kuficha maana iliyokusudiwa. Katika Kiebrania na Kigiriki, maneno yaliyo katika wingi kwa kawaida huwa na jinsia ya kiume, si yanaporejelea wanaume tu bali pia yanaporejelea wanaume na wanawake. Kwa mfano, ingawa maneno “wana wa Israeli” yanaweza kurejelea wana 12 wa Yakobo, mara nyingi hurejelea taifa zima la Israeli, wanaume na wanawake. (Mwanzo 46:5; Kutoka 35:29) Kwa hiyo, katika toleo hili, mara nyingi maneno hayo yanatafsiriwa kuwa “Waisraeli” ili kuonyesha kwamba inarejelea taifa zima. Vivyo hivyo, maneno “mvulana asiye na baba” yametafsiriwa kuwa “mtoto asiye na baba” au “yatima” ili kuonyesha kwamba yanaweza kurejelea mvulana au msichana. Kwa upande mwingine, kwa kuwa Biblia inatumia jinsia ya kiume inaporemjelea Mungu na Mwana wake, na pia malaika mbalimbali na roho waovu, hakuna msingi wa kutumia maneno yasiyo na jinsia kama inavyofanywa katika baadhi ya tafsiri za kisasa.

  • Marekebisho yote katika maandishi ya Biblia yalifanywa kwa sala, kwa makini, na kwa heshima kubwa kuelekea kazi nzuri iliyofanywa mwanzoni na Halmashauri ya Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

Sehemu nyingine za toleo hili:

Toleo hili la Biblia lina maelezo ya chini. Kwa ujumla kuna aina zifuatazo za maelezo ya chini:

  • “Au” Njia mbalimbali ambazo maandishi ya Kiebrania, Kiaramu, au Kigiriki yanaweza kutafsiriwa ili kutokeza wazo lilelile.—Mwanzo 1:2, maelezo ya chini kwenye neno “nguvu ya utendaji ya Mungu”; Yoshua 1:8, “sauti ya chini.”

  • “Au labda” Njia nyingine ambazo maandishi yanaweza kutafsiriwa na kuwasilisha wazo linalokubalika lakini lililo tofauti.—Mwanzo 21:6, “atacheka pamoja nami”; Zekaria 14:21, “Mkanaani.”

  • “Tnn.” Tafsiri ya neno kwa neno ya Kiebrania, Kiaramu, au Kigiriki au maana ya msingi ya maneno ya lugha ya awali.—Mwanzo 30:22, “mimba”; Kutoka 32:9, “wakaidi.”

  • Maana na maelezo ya ziada Maana ya majina (Mwanzo 3:17, “Adamu”; Kutoka 15:23, “Mara”); habari kuhusu uzito na vipimo (Mwanzo 6:15, “mikono”); habari muhimu kwenye Nyongeza na Kamusi.—Mwanzo 37:35, “Kaburini”; Mathayo 5:22, “Gehena.”

Sehemu iliyo upande wa mbele, yenye kichwa “Utangulizi wa Neno la Mungu,” ina muhtasari wa mafundisho ya msingi yanayopatikana kwenye Biblia. Baada ya kitabu cha Ufunuo kuna “Orodha ya Vitabu vya Biblia,” “Fahirisi,” na “Kamusi ya Maneno ya Biblia.” Kamusi hiyo humsaidia msomaji aelewe maneno yaliyoorodheshwa humo kulingana na matumizi yake hususa katika Biblia. Nyongeza A ina sehemu zifuatazo “Kanuni za Kutafsiri Biblia,” “ Sehemu za Toleo Hili,” “Jinsi Biblia Ilivyotufikia,” “Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania,” “Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo,” “Chati: Manabii na Wafalme wa Yuda na Israeli,” na “Matukio Muhimu Katika Maisha ya Yesu Duniani.” Nyongeza B ina ramani, chati, na habari nyingine muhimu kwa wanafunzi wenye bidii wa Biblia.

Kila kitabu cha Biblia kina sehemu ya yaliyomo, ambayo ina habari zilizo katika sura za kitabu hicho, pamoja na mistari hususa, na hivyo kumpa msomaji muhtasari wa kitabu chote. Sehemu ya katikati kwenye kila ukurasa ina marejeo muhimu zaidi kutoka katika matoleo yaliyotangulia, yanayoonyesha mistari ya Biblia inayohusiana.