Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

A5

Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo

Wasomi wa Biblia wanakubali kwamba jina binafsi la Mungu, linalowakilishwa na Tetragramatoni (יהוה), linapatikana karibu mara 7,000 katika maandishi ya awali ya Maandiko ya Kiebrania. Hata hivyo, wengi wanahisi kwamba halikupatikana katika maandishi ya awali ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa hiyo, tafsiri nyingi za kisasa za Biblia ya Kiswahili hazitumii jina Yehova katika sehemu inayoitwa Agano Jipya. Hata wanapotafsiri sehemu zilizonukuliwa za Maandiko ya Kiebrania ambapo Tetragramatoni ilipatikana, watafsiri wengi hutumia jina “Bwana” badala ya jina binafsi la Mungu.

Biblia TakatifuTafsiri ya Ulimwengu Mpya haifuati mtindo huo wa kutafsiri. Inatumia jina Yehova mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Walipoamua kufanya hivyo, watafsiri walifikiria mambo mawili muhimu: (1) Hati za Kigiriki tulizo nazo leo si hati za awali kabisa. Kati ya maelfu ya nakala zilizopo leo, nyingi ziliandikwa miaka mia mbili hivi baada ya nakala za kwanza kuandikwa. (2) Wakati huo, wale walionakili hati za kale walibadili Tetragramatoni na kutumia Kyʹri·os, neno la Kigiriki linalomaanisha “Bwana,” au walinakili kutoka kwa hati ambazo tayari zilikuwa zimebadili jina la Mungu.

Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mpya iliamua kwamba kuna uthibitisho wa kutosha kuwa Tetragramatoni ilipatikana katika hati za awali za Kigiriki. Uamuzi huo ulitegemea uthibitisho ufuatao:

  • Nakala za Maandiko ya Kiebrania zilizotumiwa katika siku za Yesu na mitume wake zilikuwa na Tetragramatoni kotekote katika Maandiko. Zamani watu fulani walipinga hoja hiyo. Kwa kuwa sasa nakala za Maandiko ya Kiebrania zilizoandikwa katika karne ya kwanza zimepatikana karibu na Qumran, jambo hilo limethibitishwa kikamili.

  • Katika siku za Yesu na mitume wake, Tetragramatoni ilipatikana pia katika tafsiri za Kigiriki za Maandiko ya Kiebrania. Kwa karne nyingi, wasomi walifikiri kwamba Tetragramatoni haikupatikana katika hati za Septuajinti, yaani, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania. Kisha, katikati ya karne ya 20, wasomi walipata vipande fulani vya kale sana vya Septuajinti ya Kigiriki ambavyo vilitumiwa katika siku za Yesu. Vipande hivyo vina jina binafsi la Mungu, likiwa limeandikwa kwa herufi za Kiebrania. Basi katika siku za Yesu, nakala za Maandiko ya Kigiriki zilikuwa na jina la Mungu. Hata hivyo, kufikia karne ya nne W.K., hati kuu za Septuajinti ya Kigiriki, kama vile Kodeksi ya Vatikani na Kodeksi ya Sinai, hazikuwa na jina la Mungu kuanzia kitabu cha Mwanzo hadi Malaki (ingawa hati za awali zilikuwa na jina hilo). Hivyo, haishangazi kuona kwamba nakala zilizohifadhiwa za wakati huo, hazina jina la Mungu katika sehemu inayoitwa Agano Jipya, au Maandiko ya Kigiriki katika Biblia.

    Yesu alisema hivi waziwazi: “Nimekuja katika jina la Baba yangu.” Pia, alikazia kwamba alifanya kazi katika “jina la Baba” yake

  • Maandiko ya Kigiriki yanaripoti kwamba Yesu alitumia jina la Mungu mara nyingi na kuwajulisha wengine kulihusu. (Yohana 17:6, 11, 12, 26) Yesu alisema hivi waziwazi: “Nimekuja katika jina la Baba yangu.” Pia, alikazia kwamba alifanya kazi katika “jina la Baba” yake.—Yohana 5:43; 10:25.

  • Kwa kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yaliongezwa kwenye Maandiko matakatifu ya Kiebrania, haingewezekana jina la Mungu liondolewe ghafula. Katika karne ya kwanza W.K., mwanafunzi Yakobo aliwaambia hivi wazee huko Yerusalemu: “Simioni amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Yakobo hangesema maneno hayo ikiwa hakuna mtu yeyote katika karne ya kwanza ambaye alijua au kutumia jina la Mungu.

  • Jina la Mungu limeandikwa kwa ufupisho katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwenye andiko la Ufunuo 19:1, 3, 4, 6, jina la Mungu linapatikana katika neno “Haleluya.” Neno hilo linatokana na maneno ya Kiebrania yanayomaanisha “Msifuni Yah.” “Yah” ni ufupisho wa jina Yehova. Majina mengi yaliyotumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalitokana na jina la Mungu. Kwa kweli, utafiti unaonyesha kwamba jina Yesu linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.”

  • Maandishi ya kale ya Wayahudi yanaonyesha kwamba Wakristo Wayahudi walitumia jina la Mungu katika maandishi yao. Mkusanyo wa sheria unaoitwa Tosefta, ambao ulikamilishwa karibu mwaka wa 300 W.K., unasema hivi kuhusu maandishi ya Wakristo yaliyoteketezwa siku ya Sabato: “Wanaviteketeza vitabu vya Waeneza Injili na vitabu vya minim [watu wanaodhaniwa kuwa Wakristo Wayahudi]. Vinateketezwa popote vinapopatikana, pamoja na marejeo ya Jina la Mungu lililo katika vitabu hivyo.” Maandishi hayo pia yanamnukuu Mgalilaya anayeitwa Rabi Yosé aliyeishi mwanzoni mwa karne ya pili W.K., akisema kwamba katika siku nyingine za juma “mtu hukata marejeo ya Jina la Mungu [katika maandishi ya Kikristo] na kuyahifadhi, kisha anateketeza maandishi yanayobaki.”

  • Baadhi ya wasomi wa Biblia wanasema inawezekana kwamba jina la Mungu lilipatikana katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwenye sehemu zilizonukuu Maandiko ya Kiebrania. Kamusi ya The Anchor Bible Dictionary chini ya kichwa “Tetragramatoni Katika Agano Jipya,” inasema: “Kuna uthibitisho kwamba, maandishi ya Agano Jipya yalipoandikwa kwa mara ya kwanza, Tetragramatoni, Jina la Mungu, Yahweh, ilipatikana katika baadhi au sehemu zote za Agano la Kale zilizonukuliwa katika Agano Jipya.” Msomi George Howard anasema hivi: “Kwa kuwa bado Tetragramu iliandikwa katika nakala za Biblia ya Kigiriki [Septuajinti] iliyofanyiza Maandiko ya kanisa la awali, ni jambo la busara kuamini kwamba waandishi wa Agano Jipya walitumia Tetragramu katika Biblia waliponukuu Maandiko.”

  • Watafsiri maarufu wa Biblia wametumia jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Baadhi ya watafsiri hao walifanya hivyo muda mrefu kabla ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kuchapishwa. Tafsiri hizo zinatia ndani A Literal Translation of the New Testament . . . From the Text of the Vatican Manuscript, ya Herman Heinfetter (1863); The Emphatic Diaglott, ya Benjamin Wilson (1864); The Epistles of Paul in Modern English, ya George Barker Stevens (1898); St. Paul’s Epistle to the Romans, ya W. G. Rutherford (1900); The New Testament Letters, ya J.W.C. Wand, Askofu wa London (1946). Isitoshe, katika tafsiri ya Kihispania mwanzoni mwa karne ya 20, mtafsiri Pablo Besson alitumia jina “Jehová” kwenye Luka 2:15 na Yuda 14, na katika tafsiri yake, maelezo 100 hivi ya chini yanarejelea jina la Mungu. Muda mrefu kabla ya tafsiri hizo, tafsiri za Kiebrania za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuanzia karne ya 16 na kuendelea zilitumia Tetragramatoni katika sehemu nyingi. Katika Kijerumani peke yake, karibu tafsiri 11 zinatumia jina “Yehova” (au “Yahweh” kama linavyotoholewa kutoka katika Kiebrania) katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na watafsiri wanne waliongeza jina hilo katika mabano baada ya jina “Bwana.” Zaidi ya tafsiri 70 za Kijerumani zinatumia jina la Mungu katika maelezo ya chini au katika marejeo.

    Jina la Mungu kwenye Matendo 2:34 katika tafsiri ya The Emphatic Diaglott, ya Benjamin Wilson (1864)

  • Tafsiri za Biblia katika lugha zaidi ya 100 zina jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Lugha nyingi za Afrika, za wenyeji wa asili wa Amerika, Asia, Ulaya, na visiwa vya Pasifiki zinatumia jina la Mungu mara nyingi. (Ona orodha iliyo kwenye ukurasa wa 2062 na 2063.) Watafsiri wa matoleo hayo waliamua kutumia jina la Mungu kwa sababu zinazofanana na zile zilizotajwa hapo juu. Baadhi ya tafsiri hizo za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zimechapishwa hivi karibuni, kama vile Biblia ya Kirotuma (1999), inayotumia jina “Jihova” mara 51 katika mistari 48, na tafsiri ya Batak (Toba) ya Indonesia (1989), inayotumia jina “Jahowa” mara 110.

    Jina la Mungu kwenye Marko 12:29, 30 katika tafsiri ya Kihawaii

Bila shaka, kuna msingi thabiti wa kurudisha jina la Mungu, Yehova, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hivyo ndivyo walivyofanya watafsiri wa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Wanaliheshimu sana jina la Mungu na kwa kufaa wanaogopa kuondoa chochote kilichokuwa kimeandikwa katika maandishi ya awali.—Ufunuo 22:18, 19.