Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Utekaji-Nyara Nawaandikia kuwashukuru sana kwa ajili ya mfululizo “Utekaji-Nyara—Sababu Ni Tisho la Tufeni Pote.” (Desemba 22, 1999) Mwezi uliopita kulitokea wizi katika duka kuu ninapofanya kazi. Wanaume wawili wenye kujifunika uso waliingia ndani, mmoja ameshika bunduki tayari kuifyatua. Kwa sababu makala hizo zilipendekeza kufanya vile watekaji-nyara wanavyosema, sikushindana nao waliponifunga mikono, miguu na macho na kunilazimisha kuketi sakafuni. Waliiba yen 9,500,000 (karibu dola za Marekani 90,000). Lakini nilikuwa mtulivu na sikujeruhiwa. Makala hizo zilikuja kwa wakati unaofaa!

S. H., Japani

Anafurahia Amkeni! Ingawa mimi ni mshiriki wa kanisa la Assembly of God hilo halinizuii kusoma Amkeni! Bado sijapata kusoma gazeti jingine la hali ya juu na lenye kuzungumzia mambo mbalimbali kama hili. Mimi sina televisheni nyumbani mwangu, lakini naweza kushiriki habari za karibuni pamoja na marafiki zangu kwa sababu huwa nimezipata kwenye gazeti lenu.

A.B.A., Brazili

Unyoaji Laini Kabisa Makala “Unyoaji Laini Kabisa” (Januari 22, 2000) ilikuja kwa wakati ufaao kwangu. Mume wangu anahitaji kutunzwa siku zote na hawezi kujinyoa. Yale madokezo manne ya kunyoa yalinisaidia sana. Sasa anataka nimnyoe kila siku!

L. D., Ujerumani

Kusema Uwongo Ile makala “Maoni ya Biblia: Kusema Uwongo—Je, Kwaweza Kutetewa Wakati Wowote?” (Februari 8, 2000) ilinichochea fikira sana. Hata hivyo, si Biblia inakataza aina yote ya udanganyifu?

D. S., Marekani

Katika Biblia, kwa kawaida kusema uwongo humaanisha kumpa habari isiyo ya kweli mtu ambaye anastahili kujua ukweli wa jambo na kufanya hivyo kwa nia ya kumdanganya au kumuumiza yeye au mtu mwingine. Hivyo watu wenye kumhofu Mungu kama vile Abrahamu, Isaka, Rahabu, na Daudi walitoa habari isiyo ya kweli lakini hawakuhukumiwa kuwa waongo. Bila shaka, walitenda hayo wakiwa katika hali isiyo ya kawaida. Walivyotenda hakumpi yeyote udhuru wa kudanganya. Kwa mfano, iwapo Mkristo ameapa mbele ya mahakama kwamba atasema ukweli, basi itambidi afanye hivyo au anyamaze.—Mhariri.

Familia Zisizo na Baba Toleo la Februari 8, 2000, lilizungumzia zoea la watoto wasio na baba. (“Familia Zisizo na Baba—Kukomesha Zoea Hilo”) Siwezi kueleza jinsi nilivyoudhika na kukasirika baada ya kusoma makala hiyo. Mnatetea mwenendo wa baba wanaotoweka nyumbani kwa kuzungumzia habari inayowahusu kama vile haki zao za kuwatembelea watoto na kuathiriwa kwao na kuzorota kwa uchumi. Mbona hamkuwakemea? Mnawachocheaje wanaume kurekebisha makosa yao?

S. L., Marekani

Tunaelewa jinsi wengine wanavyoweza kuhisi uchungu wasomapo habari hiyo, hasa wale ambao wameachwa na baba zao. Hata hivyo, makala hiyo haikukusudiwa kuwakemea wanaume. Badala yake, tulijitahidi kufahamisha watu pande zote za maswala tata yanayohusika. Pia tuliwatolea watu walioachwa madokezo yenye kutumika. Jambo la kupendeza ni kwamba makala ya kumalizia, “Familia Zisizo na Baba—Kukomesha Zoea Hilo,” ilisema hivi: “Mielekeo ya sasa ya familia itakomeshwa tu ikiwa watu wako tayari kufanya mabadiliko makubwa katika kufikiri kwao, mtazamo wao, tabia yao, maadili yao.”—Mhariri.

Nilipoiona picha ya baba na binti yake kwenye jalada, nilitokwa na machozi. Nimetamani siku zote kuwa na uhusiano kama huo pamoja na baba yangu. Makala hiyo ilinisaidia nifahamu kilichosababisha hali tuliyo nayo katika familia yetu. Ilikuwa kama mwale wa jua ukimulika mahali penye giza na kujibu maswali ambayo yamekuwa yakinisumbua kwa muda mrefu.

M. M., Marekani