Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kukabilianaje na Hali Baada ya Baba Kutuacha?

Naweza Kukabilianaje na Hali Baada ya Baba Kutuacha?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kukabilianaje na Hali Baada ya Baba Kutuacha?

“Ilikuwa vigumu sana kukua bila baba. Nilitamani tu kupendwa kidogo.”—Henry. *

JOAN alikuwa na umri wa miaka 13 baba yake alipoondoka nyumbani. Akiwa mraibu sugu wa pombe, hakuwasiliana sana na watoto wake baada ya kuwaacha. Kwa kusikitisha, Joan hayuko peke yake katika hali hii; vijana wengi wameachwa na baba zao.

Ikiwa umepatwa na hali hii, basi huenda ikawa vigumu kwako kukabiliana na hali hiyo. Huenda ukalemewa na hisia za uchungu na hasira mara kwa mara. Nyakati nyingine huenda ukahuzunika na kushuka moyo. Huenda hata ukawa na tamaa ya kuasi. Kama vile Solomoni, mwandikaji wa Biblia alivyosema pindi moja, “jeuri humpumbaza mwenye hekima.”—Mhubiri 7:7.

‘Kutenda Kipumbavu’

James ‘alitenda kipumbavu’ baba yake alipoondoka nyumbani. James alisema hivi: “Sikutii mamlaka yoyote, hata sikumtii mama yangu. Nilihusika kwenye mapigano mengi. Nilikuwa nikidanganya na kutoroka nyumbani usiku kisiri mara nyingi, kwa kuwa hakukuwa na mtu wa kunitia nidhamu. Mama alijaribu kunizuia lakini alishindwa kabisa.” Je, kuasi huko kuliboresha maisha ya James? Hata kidogo. James asema kwamba punde si punde alikuwa “akitumia dawa za kulevya, akikosa shule, na kuanguka mitihani.” Tabia hiyo ilizidi kuwa mbaya. “Niliiba madukani,” yeye akiri, “na kuwanyang’anya watu mali yao. Nilikamatwa mara mbili na kufungwa gerezani kwa muda mfupi, lakini sikukoma.”

Alipoulizwa ni nini kilichomfanya aasi hivyo, James alisema hivi: “Kwa sababu baba yangu aliondoka nyumbani, sikuwa mwenye nidhamu. Sikufikiria jinsi nilivyokuwa nikimwumiza mama yangu, ndugu yangu mdogo, dada yangu, na hata mimi mwenyewe. Nilihitaji utunzaji na nidhamu kutoka kwa baba yangu.”

Lakini kuasi hufanya hali kuwa mbaya zaidi. (Ayubu 36:18, 21) Kwa mfano, James hakujiletea mwenyewe tu matatizo bali pia mama na ndugu na dada yake walipatwa na mkazo na mfadhaiko usio wa lazima. Jambo baya hata zaidi ni kwamba matendo ya uasi yaweza kuharibu uhusiano wa mtu na Mungu. Kwa vyovyote, Yehova huamuru vijana wawatii mama zao.—Mithali 1:8; 30:17.

Kudhibiti Hasira

Basi, unaweza kukabilianaje na hasira na chuki ambayo huenda ukahisi kuelekea baba yako? Kwanza, labda unahitaji kukumbuka kwamba hulaumiki kwa sababu ya baba yako kuondoka. Wala haimaanishi kwamba sasa yeye hakupendi au hakujali tena. Bila shaka, ni jambo linaloumiza ikiwa baba hafanyi jitihada yoyote ya kuwasiliana au kutembelea. Lakini kama makala inayotangulia katika mfululizo huu ilivyoonyesha, * baba wengi ambao wameondoka nyumbani hukosa kuwasiliana na watoto, si kwa sababu hawawapendi, bali kwa sababu wamelemewa na hatia na aibu. Wengine, kama vile baba ya Joan, ni waraibu wa dawa za kulevya au pombe, na hilo hudhoofisha uwezo wao wa kutenda.

Hata hali iweje, kumbuka kwamba wazazi wako si wakamilifu. Biblia husema hivi: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23; 5:12) Bila shaka, hilo halitolei udhuru matendo yenye kuumiza au kutojali. Lakini kutambua kwamba sote tumerithi kutokamilika huenda kukasaidia kutupilia mbali hasira yenye kudhuru na chuki.

Yanayosemwa na Mhubiri 7:10, Biblia Habari Njema, yaweza kukusaidia kukabiliana na hasira na chuki ambayo huenda ukawa nayo kuelekea wazazi wako. Tazama inavyoonya dhidi ya kukazia fikira wakati uliopita: “Usiulize, ‘Kwa nini nyakati za kale zilikuwa bora kuliko za sasa?’ Huulizi hivyo kwa kutumia hekima.” Hivyo, badala ya kufikiria sana yaliyopita, ni vyema kufikiria jinsi uwezavyo kutumia kwa njia bora zaidi hali yako ya sasa.

Kuchukua Hatua ya Kwanza

Kwa mfano, huenda ukaamua kuchukua hatua ya kuwasiliana na baba yako. Ni kweli kwamba yeye ndiye aliyekuacha na huenda kwa haki ukahisi kwamba ni daraka lake kuchukua hatua ya kwanza. Lakini ikiwa ameshindwa kufanya hivyo na ukosefu wa mawasiliano unakufanya uhuzunike na kukosa furaha, Je, haingefaa wewe kujaribu kurekebisha hali hiyo? Fikiria jinsi Yesu Kristo alivyoshughulikia hali marafiki wake walipomwumiza. Katika usiku wake wa mwisho akiwa binadamu, mitume walikimbia na kumwacha. Petro alikuwa amejigamba kwamba angeshikamana na Yesu hata hali iweje. Na bado, Petro alimkana Yesu—si mara moja bali mara tatu!—Mathayo 26:31-35; Luka 22:54-62.

Hata hivyo, Yesu aliendelea kumpenda Petro ijapokuwa mapungukio ya Petro. Baada ya ufufuo wake, Yesu alichukua hatua ya kwanza kurudisha uhusiano wao kwa kumtokea Petro kwa njia ya pekee. (1 Wakorintho 15:5) Kwa kupendeza, Yesu alipomwuliza Petro swali, “Je, wanipenda?” Jibu la Petro lilikuwa “Ndiyo, Bwana, wajua nina shauku na wewe.” Ijapokuwa matendo yake ya aibu, Petro bado alimpenda Yesu.—Yohana 21:15.

Kama ilivyokuwa katika kisa cha Petro na Yesu, hali baina yako na baba yako huenda isiwe bila tumaini kama inavyoonekana. Huenda akaitikia ikiwa ungechukua hatua fulani kama vile kupiga simu, kuandika barua, au kumtembelea. Henry, anayetajwa mwanzoni, akumbuka hivi: “Pindi moja nilimwandikia baba yangu barua na yeye akaandika majibu akisema kwamba ananionea fahari. Niliweka barua hiyo kwenye fremu na kuiangika ukutani kwa miaka mingi. Ningali nayo hadi leo.”

Joan na ndugu na dada zake vivyo hivyo walichukua hatua na kwenda kumwona baba yao aliye mraibu wa pombe. “Hali yake haikuwa nzuri,” Joan akiri, “lakini bado tulifurahi kumwona.” Labda huenda ukapata matokeo mazuri ukichukua hatua ya kwanza. Ikiwa hupati itikio mwanzoni, afadhali uache wakati fulani upite halafu ujaribu tena.

Kukabiliana na Uchungu wa Kukataliwa

Solomoni atukumbusha kwamba “kuna wakati wa kutafuta na wakati wa kupoteza.” (Mhubiri 3:6) Nyakati nyingine huenda kijana akakabili ukweli wenye kuumiza wa kwamba baba yake hataki tena kuwa na uhusiano pamoja na watoto wake. Ikiwa ndivyo baba yako alivyo, huenda siku moja atang’amua hasara anayopata kwa kushindwa kudumisha uhusiano pamoja nawe.

Hata hivyo, kwa sasa uwe na uhakika kwamba kukataliwa na baba yako hakumaanishi kwamba hufai kitu. Mtunga-zaburi wa Biblia Daudi, alisema hivi: ‘Baba yangu na mama yangu wakiniacha, BWANA atanikaribisha kwake.’ (Zaburi 27:10) Naam, wewe ungali mwenye thamani kubwa machoni pa Mungu.—Luka 12:6, 7.

Hivyo ukihisi umevunjika moyo au kushuka moyo, mkaribie Mungu katika sala. (Zaburi 62:8) Mwambie hisia zako zote. Uwe na hakika kwamba atakusikiliza na kukufariji. Mtunga-zaburi mwingine wa Biblia aliandika hivi: “Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.”—Zaburi 94:19.

Ushirika mchangamfu pamoja na Wakristo wenzako waweza pia kukusaidia kukabiliana na kukataliwa huko. Mithali 17:17 husema hivi: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Waweza kupata rafiki wa kweli kama hao ndani ya kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova. Itafaa sana kujuana na baadhi ya waangalizi wa kutaniko. Peter, ndugu ya Joan anatoa ushauri huu: “Sema na wazee kutanikoni, nao watakusaidia sana. Ikiwa umeachwa na baba yako, waeleze hisia zako.” Waangalizi wa kutaniko hata waweza kukupa madokezo yenye kutumika ya kushughulikia baadhi ya kazi alizokuwa akifanya baba yako hapo awali, kama vile kurekebisha vitu nyumbani.

Mama yako aweza pia kukutegemeza. Kwa kweli, huenda yeye mwenyewe akawa analemewa na maumivu ya kihisia-moyo. Lakini ukieleza hisia zako kwa staha, bila shaka atafanya awezavyo ili kukusaidia ifaavyo.

Unga Mkono Familia Yenu!

Kuondoka kwa baba yako huenda kukaathiri familia yenu katika njia kadhaa. Huenda mama akalazimika kuajiriwa—labda hata kuchukua kazi mbili—ili kukidhi mahitaji. Wewe, ndugu na dada zako huenda ikawabidi kufanya kazi nyingi zaidi za nyumbani kuliko awali. Lakini unaweza kukabiliana na mabadiliko hayo ukikuza upendo wa Kikristo usio na ubinafsi. (Wakolosai 3:14) Hilo laweza kukusaidia kudumisha mwelekeo chanya na kupunguza kabisa chuki. (1 Wakorintho 13:4-7) Peter asema hivi: “Kuisaidia familia yetu ni jambo muhimu, nami hupata uradhi kwa kujua kwamba nawasaidia mama yangu na dada zangu.”

Bila shaka, baba kuondoka nyumbani ni tukio lenye kuhuzunisha na lenye kuumiza sana. Lakini waweza kuwa na hakika kwamba kupitia msaada wa Mungu na msaada wa rafiki Wakristo na washiriki wa familia wenye upendo, wewe na familia yenu mwaweza kukabiliana na hali hiyo. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Baba Alituacha?” katika toleo letu la Novemba 22, 2000.

^ fu. 27 Ili kupata habari zaidi juu ya kuishi katika familia yenye mzazi mmoja, ona makala “Vijana Huuliza . . . ” katika toleo la Mei 8, 1992, Kiswahili au Desemba 22, 1990, Kiingereza na toleo la Agosti 8, 1992, Kiswahili au Machi 22, 1991, Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Vijana fulani wamechukua hatua ya kuwasiliana na baba yao