Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mtu Huchagua Kuwa Mwalimu?

Kwa Nini Mtu Huchagua Kuwa Mwalimu?

Kwa Nini Mtu Huchagua Kuwa Mwalimu?

“Walimu wengi huchagua kazi hiyo kwa sababu wanataka kuwasaidia watu wengine. Mtu anapochagua [kazi ya ualimu] anawajibika kuwasaidia watoto wawe na maisha bora.”—Teachers, Schools, and Society.

IJAPOKUWA ualimu unaonekana kuwa kazi rahisi kwa wengine, mwalimu anaweza kukabili magumu mengi, kama vile kuwa na watoto wengi mno darasani, kushughulikia karatasi nyingi, urasimu unaolemea, wanafunzi wasiotaka kujifunza, na mshahara mdogo. Pedro, mwalimu mmoja huko Madrid, Hispania, alisema hivi: “Ualimu si kazi rahisi hata kidogo. Ni lazima mwalimu ajitolee kabisa. Hata hivyo, licha ya magumu, naona ualimu kuwa kazi yenye kuridhisha kuliko kazi yoyote ya kibiashara.”

Walimu wanaweza kulemewa na matatizo katika shule za majiji makubwa za nchi nyingi. Dawa za kulevya, uhalifu, ukosefu wa maadili, na wazazi wasiojali huathiri sana hali na nidhamu shuleni. Kutotii ni jambo la kawaida. Kwa nini, basi, watu wengi huchagua kuwa walimu?

Leemarys na Diana ni walimu huko New York City. Wao huwafundisha watoto wenye umri wa miaka 5 hadi 10. Wote wawili wanajua lugha mbili (Kiingereza na Kihispania), nao hufundisha hasa watoto Wahispania. Swali letu lilikuwa . . .

Mwalimu Husukumwa na Nini?

Leemarys alisema: ‘Ninasukumwa na upendo wangu kwa watoto. Najua kwamba wototo wengine hawana mtu mwingine wa kuwatia moyo katika jitihada zao, isipokuwa mimi.’

Diana alisema hivi: “Nilimfundisha mpwa wangu wa kiume aliyekuwa na umri wa miaka minane, ambaye alikuwa na matatizo shuleni—hasa tatizo la kusoma. Nilifurahi sana kumwona yeye na wengine wakifanya maendeleo! Kwa hiyo, niliamua kuwa mwalimu, na nikaacha kazi yangu katika benki.”

Waandishi wa Amkeni! waliwauliza walimu katika nchi kadhaa swali hilohilo, na baadhi ya majibu yanapatikana hapa chini.

Giuliano, Mwitalia mwenye umri wa miaka 40 na kitu, alieleza: “Nilichagua kazi hiyo kwa sababu nilivutiwa nayo nilipokuwa mwanafunzi (kulia). Niliona kwamba ningekuwa na nafasi nyingi za kuwachochea wengine na kutumia vipawa vyangu mbalimbali. Shauku niliyokuwa nayo hapo mwanzoni ilinisaidia kushinda magumu niliyokabili nilipoanza kufundisha.”

Nick, anayeishi New South Wales, Australia, alisema: “Mimi ni mchunguzi wa kemia lakini sikuweza kupata kazi ya aina hiyo, hata hivyo, kazi ya ualimu ilipatikana kwa urahisi. Nimefurahia kazi ya ualimu, na ninadhani kuwa wanafunzi hufurahia kufundisha kwangu.”

Mara nyingi, wale wanaochagua kazi ya ualimu huiga mfano wa wazazi wao. William, anayeishi Kenya, alijibu kwa kusema: “Nilivutiwa na kazi hiyo hasa kwa sababu baba yangu alikuwa mwalimu katika mwaka wa 1952. Ninaendelea na kazi ya ualimu hasa kwa sababu ninajua kwamba ninawasaidia watoto kuwa watu bora.”

Rosemary, anayeishi Kenya pia, alituambia: “Sikuzote nilikuwa na tamaa ya kuwasaidia watu maskini. Kwa hiyo, uchaguzi wangu ulikuwa kati ya uuguzi na ualimu. Nafasi ya kuwa mwalimu ilitokea kwanza. Naipenda kazi yangu hata zaidi kwa kuwa mimi ni mama-watoto.”

Berthold, anayeishi Düren, Ujerumani, alisukumwa na jambo jingine: “Mke wangu alinisadikisha kwamba nina kipawa cha kufundisha.” Na hakukosea. Berthold aliongeza: “Ninaifurahia kazi yangu sana. Iwapo mwalimu hatawajali watoto na kuamini kwamba elimu ni muhimu, hatakuwa mwalimu bora na mwenye matokeo, shauku, na uradhi.”

Mwalimu Mjapani, Masahiro, anayeishi Nakatsu City, alisema hivi: ‘Nilisukumwa kuwa mwalimu kwa sababu nilikuwa na mwalimu stadi katika darasa moja. Alijitolea kabisa ili kutufundisha. Ninaendelea na kazi yangu hasa kwa sababu ninawapenda watoto.’

Yoshiya, mwenye umri wa miaka 54 sasa na anayeishi Japani pia, alikuwa na kazi yenye mshahara mnono kwenye kiwanda fulani, lakini alihisi kwamba kazi hiyo na kusafiri kazini kila siku kulimlemea. “Siku moja nilijiuliza, ‘Nitaendelea na maisha haya hadi lini?’ Niliamua kutafuta kazi inayohusisha watu wala si vitu. Ualimu ni kazi ya pekee. Ualimu huhusisha watu, kwa kuwa mwalimu hushughulikia mahitaji ya vijana.”

Valentina, anayeishi St. Petersburg, Urusi, ana maoni hayohayo pia. Alisema: “Mimi mwenyewe nilichagua kuwa mwalimu. Nimekuwa mwalimu wa shule ya msingi kwa miaka 37. Napenda kuwafundisha watoto, hasa watoto wachanga. Napenda kazi yangu, ndiyo sababu sijastaafu bado.”

William Ayers, ambaye ni mwalimu, aliandika hivi: “Watu husukumwa kuwa walimu kwa sababu wanawapenda watoto na vijana, au kwa sababu wanapenda kushirikiana nao na kuona jinsi wanavyofanya maendeleo, wanavyokua, na wanavyopata stadi, uzoefu, na uwezo maishani. . . . Walimu hufundisha . . . kwa sababu wanataka kujitolea kuwasaidia wengine. Mimi hufundisha kwa sababu ninataka kuboresha ulimwengu.”

Ndiyo, licha ya magumu na vizuizi, maelfu ya wanawake na wanaume wanaotaka kujitolea huvutiwa na kazi ya ualimu. Wanakabili magumu gani? Sehemu inayofuata itajibu swali hilo.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Jinsi Mwalimu Anavyoweza Kuwasiliana na Wazazi

✔ Fahamiana na wazazi. Kufanya hivyo si kupoteza wakati bali nyote mtanufaika. Kutakupatia nafasi ya kuwasiliana na wale wanaoweza kukusaidia sana katika kazi yako.

✔ Zungumza na mzazi kwa heshima, na usiongee naye kana kwamba hajui chochote. Epuka kutumia usemi asioweza kuelewa.

✔ Unapozungumzia watoto, kazia sifa zao nzuri. Pongezi italeta matokeo mazuri kuliko shutuma. Eleza kile ambacho wazazi wanaweza kufanya ili kumsaidia mtoto kufaulu.

✔ Acha wazazi wajieleze, kisha usikilize kwa makini.

✔ Elewa hali ya nyumbani ya mtoto. Ikiwezekana, watembelee nyumbani.

✔ Panga tarehe ya mazungumzo ya wakati ujao. Kufuatilia mazungumzo ni muhimu. Kunaonyesha kwamba unajali kwelikweli. —Habari hiyo inatoka katika kitabu Teaching in America.

[Picha katika ukurasa wa 6]

‘Baba yangu alikuwa mwalimu.’—WILLIAM, KENYA

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Ninapenda kuwafundisha watoto.”—VALENTINA, URUSI

[Picha katika ukurasa wa 7]

‘Ualimu ni kazi ya pekee. Mwalimu hushughulikia mahitaji ya vijana.’ —YOSHIYA, JAPANI