Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Suluhisho Ni Kuabudu Jinsi Upendavyo?

Je, Suluhisho Ni Kuabudu Jinsi Upendavyo?

Je, Suluhisho Ni Kuabudu Jinsi Upendavyo?

WATU WANAPOENDELEA KUACHA DINI, si ajabu kwamba wengi wanaweza kubuni njia yao wenyewe ya kuabudu. Hata hivyo, maswali haya yanazuka, Je, kufanya hivyo hutosheleza mahitaji ya mtu ya kiroho? Je, hilo ndilo suluhisho?6

Ili kujibu maswali hayo, hebu kwanza tutumie ‘nguvu zetu za kufikiri kuzuri’ kuchunguza iwapo inafaa kujitungia njia ya kuabudu. Nguvu hizo ni kati ya zawadi kubwa zaidi ambazo wanadamu wamepewa.—Waroma 12:1.

Mtu anayefikiri vizuri hukataa mambo yanayojipinga. Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa kuhusu watu wa Sweden ambao wameamua kuabudu kwa njia yao wenyewe, ulikata kauli kwamba mara nyingi watu “hukusanya bila kufikiri mawazo tofauti-tofauti (na labda yanayopingana) kuhusu kusudi la maisha na kubuni maoni yao wenyewe.”

Kwa mfano, asilimia 2 tu kati ya wale waliodai kuwa “Wakristo ambao wanaabudu jinsi wapendavyo” ndio waliomtaja Yesu, au hata kumtaja kuwa mtu mashuhuri. Hata hivyo, wengi wao walisema kwamba wanaamini fundisho la kuzaliwa upya katika mwili wa kiumbe mwingine. Sasa, ikiwa mtu anadai kuwa mfuasi wa Yesu Kristo huku akipuuza maisha na mafundisho yake na hata kuamini mafundisho yanayopinga kabisa yale ya Kristo, si anajipinga? *

Kwa kawaida nguvu zetu za kufikiri kuzuri hutuzuia kuamini mambo ambayo hayaeleweki waziwazi. Hata hivyo, wakati watu waliohojiwa walipoulizwa iwapo wanamwamini “Mungu au nguvu inayozidi ile ya wanadamu,” wengi walisema kwamba huenda ikawa kuna nguvu “Fulani” kama hiyo. Mmoja wao alisema hivi: “Naamini kitu kinachozidi uwezo wa wanadamu lakini si lazima iwe ni Mungu.” Wale waliosema kwamba wanamwamini Mungu walihisi kwamba “hana maana sana maishani mwao.” Hivyo, ripoti hiyo ilisema kwamba watu wanaoabudu jinsi wapendavyo wanafuata “mawazo yasiyoeleweka na yenye kuvuruga,” na ilimalizia kwa kunukuu jinsi watu wengi walivyosema: “Ninaamini kitu fulani, lakini sijui ni nini.”

Uchunguzi uliofanywa huko Kanada kuhusu watu ambao wanaabudu jinsi wapendavyo ulikuwa na matokeo kama hayo. Gazeti la Alberta Report lasema hivi: ‘Watu wengi sasa wanaamini karibu kila kitu wanachoweza kuwazia bila sababu yoyote. Na tunapojaribu kuchunguza jinsi ibada yao inavyowasaidia maishani, tunagundua kwamba haiwapi mwongozo wowote. Haina kanuni thabiti kuhusu yaliyo sawa. Kwa hiyo mambo ambayo wanaamini hayana umuhimu wowote.’ Gazeti hilo lilisema kuhusu “mungu aliyegawanywa” kwa sababu watu ambao wanaabudu jinsi wapendavyo ‘wanachagua-chagua mambo ya kuamini kutoka sehemu tofauti-tofauti za mafundisho ya dini.’ Basi, je ni jambo la akili kutegemeza imani—hata tumaini la wakati ujao—juu ya maoni hayo yasiyoeleweka, yasiyo na msingi thabiti, na yaliyogawanyika-gawanyika?

Uhitaji Wetu wa Ushirika

Kwa muda mrefu wafuasi wa dini wamethamini sana ushirika, udugu, na umoja. (Matendo 2:42, 46) Basi ikiwa mtu amechagua kuabudu kivyake, je, kweli anaweza kutosheleza mahitaji hayo?

Je, si kweli kwamba watu wanapochagua kuamini mambo yao wenyewe hiyo hutokeza na kuongeza migawanyiko ya kidini miongoni mwao? Gazeti la Alberta Report lilisema hivi: ‘Sasa mtu anaweza kufuata maoni yake mwenyewe kuhusu dini, na ndiyo sababu kuna mamilioni ya mafundisho ya kidini katika nchi yetu.’ Basi, haishangazi kwamba wazo la kuabudu jinsi mtu apendavyo limefafanuliwa kuwa kukosa utaratibu wa kiroho.

Vipi Kuhusu Maadili?

Askofu wa Sweden Martin Lönnebo alipohojiwa na gazeti la Svenska Dagbladet, alisema kwamba ‘kuabudu jinsi mtu apendavyo hakuwezi kuleta maendeleo katika siku zetu, na mtu anayefanya hivyo hawezi kupitishia kizazi kingine maadili yake.’ Maoni hayo yanaungwa mkono kwa kiasi fulani na mtazamo wa wazazi wengi huko Sweden kuhusu kulea watoto. Gazeti la Svenska Dagbladet lasema kwamba wazazi hao huwa na maoni haya: “Amini unachopenda! Na usiwalazimishe watoto wako waamue. Lakini waache wachague wanapokuwa wakubwa.”

Gazeti hilo lilisema kwamba kuwafundisha watoto maadili ya kidini ni kama kuwaamulia wanachotaka kufanya. Hata hivyo, gazeti hilo lilimalizia hivi: “Kuwapitishia watoto maadili ya kidini kwaweza kuwa jambo lenye manufaa na labda ndiyo njia pekee ya kuwawezesha . . . kujiamulia mambo.” Kwa kweli, hali mbaya ya vijana leo inaonyesha kwamba wazo la kuabudu jinsi mtu apendavyo halijasaidia kuunganisha familia kupitia maadili thabiti ambayo yanaweza kupitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Basi, yaonekana kwamba wazo la kuabudu jinsi mtu apendavyo haliwezi kutoa majibu thabiti na yenye kutegemeka kwa maswali ya maisha, wala haliwezi kuunganisha watu wala kutosheleza uhitaji wao wa mwongozo wa maadili. Makala ya gazeti la Svenska Dagbladet, iliyonukuliwa hapo awali, ilisema hivi kuhusu kuabudu jinsi mtu apendavyo: ‘Ikiwa dini ina kila kitu ambacho mtu anataka, basi “dini” hiyo ni bure. Na ikiwa uhuru hauna mipaka, basi uhuru huo ni bure.’

Kwa wazi, mambo mengi yanaonyesha kwamba kuabudu jinsi mtu apendavyo hakuwezi kutosheleza mahitaji ya kiroho ya watu. Mtu anawezaje kutazamia kutosheleza mahitaji hayo kwa kuchagua mambo anayotaka kuamini kutoka kwenye dini mbalimbali, kana kwamba anachagua chakula kwenye meza yenye vyakula mbalimbali? Pia, ni wazi kwamba dini hazijatosheleza mahitaji hayo. Basi, tutapata suluhisho wapi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Yesu hakufundisha kwamba wafu huzaliwa upya katika mwili wa kiumbe mwingine. Badala yake, alifundisha kuwa wafu hawako, ni kana kwamba wamelala usingizi, huku wakisubiri kufufuliwa wakati ujao.—Yohana 5:28, 29; 11:11-14.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Je, tuione dini kama kuchagua chakula kwenye meza yenye vyakula mbalimbali, huku tukichagua mafundisho yale tu yanayotupendeza?