Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Licha ya Majaribu, Tumaini Langu Halijafifia

Licha ya Majaribu, Tumaini Langu Halijafifia

Licha ya Majaribu, Tumaini Langu Halijafifia

IMESIMULIWA NA ANDREJ HANÁK

Ilikuwa mwaka wa 1943, na Vita ya Pili ya Ulimwengu ilikuwa ikiendelea. Kwa sababu sikuunga mkono upande wowote vitani nilikuwa gerezani huko Budapest, Hungaria. Nilipokuwa gerezani kasisi mwenye ndevu nyingi wa Kanisa Othodoksi alitaka kubadilisha Biblia yake kwa posho langu la mkate wa siku tatu. Ijapokuwa nilikuwa na njaa, nina hakika kwamba badilishano hilo lilinifaidi.

HAIKUWA rahisi kudumisha dhamiri safi ya Kikristo wakati Wanazi walipovamia nchi yetu wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Baadaye, Wakomunisti walipotawala nchi yetu kwa zaidi ya miaka 40, tulihitaji pia kujikakamua kumtumikia Muumba wetu, Yehova Mungu, na kudumisha uaminifu wetu.

Kabla ya kusimulia jinsi tulivyodumisha uaminifu kwa Mungu wakati huo, acha nieleze kidogo juu yangu mwenyewe. Bila shaka utapendezwa kujifunza kuhusu magumu ambayo Mashahidi wa Yehova walivumilia wakati huo. Kwanza, acha nieleze kuhusu hali ya kidini iliyonifanya nitilie shaka dini maarufu za eneo letu.

Swali la Kidini Lililonitatiza

Nilizaliwa mnamo Desemba 3, 1922, katika kijiji cha Hungaria cha Pácin, karibu na mpaka wa Slovakia. Wakati huo, Slovakia ilikuwa sehemu ya mashariki ya Chekoslovakia. Baada ya Vita ya Pili ya Ulimwengu, wakati ambapo Muungano wa Sovieti ulidhibiti sehemu kubwa ya Chekoslovakia, mpaka wa Ukrainia ulihamishwa hadi umbali wa kilometa 30 kutoka Pácin.

Mimi nilikuwa mtoto wa pili kati ya watoto watano, na wazazi wetu walikuwa Wakatoliki wenye bidii. Nilipokuwa na umri wa miaka 13, jambo fulani lilinifanya nifikirie dini kwa uzito. Niliandamana na Mama katika safari ya kilometa 80 ili kwenda kuabudu katika kijiji cha Máriapócs huko Hungaria. Tulitembea kwa miguu hadi kijiji hicho kwa sababu tuliamini kwamba tungepata baraka nyingi zaidi kwa kufanya hivyo. Wakatoliki wa Kanisa Katoliki la Roma na la Ugiriki vilevile walikwenda kuabudu katika kijiji hicho. Hapo awali niliamini kwamba makanisa hayo mawili yalikuwa sehemu ya dini ya Katoliki iliyokuwa na umoja wa kadiri fulani. Lakini punde nilitambua kwamba haikuwa hivyo.

Nilipata kwamba Misa ya Kanisa Katoliki la Ugiriki ilikuwa ya kwanza. Nikaamua kuhudhuria hiyo. Baadaye, Mama alipojua kwamba nilikuwa nimehudhuria Misa hiyo alikasirika sana. Nilimwuliza hivi nikiwa nimevurugika kidogo: ‘Kuna ubaya gani kuhudhuria Misa mbalimbali? Sote tunashiriki ule mwili mmoja wa Kristo.’

Kwa kuwa Mama hakuweza kunijibu alisema tu: “Mwanangu, ni dhambi kuuliza maswali kama hayo.” Hata hivyo, maswali hayo yalibaki akilini mwangu.

Maswali Yangu Yanajibiwa

Muda mfupi baada ya Vita ya Pili ya Ulimwengu kuanza mwaka wa 1939, nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilihamia Streda nad Bodrogom. Mji huo mdogo uko umbali wa kilometa chache kutoka nyumbani, na sasa uko katika eneo la mashariki la Slovakia. Nilikwenda huko kufundishwa kazi na mhunzi mmoja. Hata hivyo, nilijifunza jambo jingine nyumbani kwake ambalo lilikuwa muhimu kuliko kutengeneza viatu vya farasi na vitu vingine vya chuma.

Mke wa mhunzi huyo, Mária Pankovics, alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, wakati wa mchana nilijifunza kazi ya uhunzi kutoka kwa mume wake, lakini usiku nilijifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu nilijifunza kazi ya uhunzi, nilielewa vizuri sana maneno haya ya Zaburi 12:6: “Maneno ya BWANA ni maneno safi, ni fedha iliyojaribiwa kalibuni juu ya nchi; iliyosafishwa mara saba.” Nilifurahia sana kuchunguza maneno ya Yehova na kupata majibu kwa maswali yangu ya Biblia!

Sikujua kwamba baada ya muda mfupi, imani yangu mpya ingejaribiwa wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilipopamba moto.

Nilifungwa kwa Sababu ya Imani Yangu

Muda mfupi baada ya kuanza kujifunza kazi ya uhunzi, vijana wote wa kiume huko Hungaria walitakiwa kuzoezwa kuwa wanajeshi. Lakini niliamua kufuata kanuni ya Biblia inayopatikana kwenye Isaya 2:4 ya ‘kutojifunza vita tena kamwe.’ Kwa sababu hiyo, nilihukumiwa kifungo cha siku kumi. Baada ya kuachiliwa, niliendelea kujifunza Biblia. Kisha, ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova nilibatizwa Julai 15, 1941.

Wakati huo, Ujerumani ya Nazi ilikuwa imevamia Muungano wa Sovieti, na nchi za mashariki mwa Ulaya zilikuwa vitani. Uchochezi wa vita na uzalendo ulienea kotekote. Lakini kwa sababu ya imani yao inayotegemea Biblia, Mashahidi wa Yehova hawakuunga mkono upande wowote.

Mnamo Agosti 1942, tulishambuliwa vikali. Wenye mamlaka walitayarisha vituo kumi na kuwapeleka Mashahidi, vijana kwa wazee, huko. Hata wale ambao walishirikiana nasi ijapokuwa hawakuwa wamebatizwa walipelekwa kwenye vituo hivyo. Nilikuwa miongoni mwa wale waliopelekwa kwenye gereza fulani huko Sárospatak, jiji lililokuwapo umbali wa kilometa 20 hivi kutoka kijiji chetu cha Pácin.

Mfungwa mchanga zaidi alikuwa na umri wa miezi mitatu tu. Alikuwa amefungwa pamoja na mama yake aliyekuwa Shahidi. Tulipoomba chakula kidogo angalau kwa ajili ya mtoto huyo, mlinzi alijibu hivi: “Acha alie. Kulia kutamfanya awe Shahidi mshupavu.” Tulimhurumia mtoto huyo, lakini tulihuzunika hasa kuona jinsi uchochezi wa kizalendo ulivyomfanya mlinzi huyo kijana kuwa na moyo mgumu.

Nilihukumiwa kifungo cha miaka miwili. Kisha nikahamishwa hadi gereza lililokuwa kwenye 85 Margit Körút huko Budapest. Vyumba vya gereza vilikuwa vyenye ukubwa wa meta 4 kwa meta 6, na watu 50 hadi 60 hivi waliingizwa humo. Tuliishi katika vyumba hivyo visivyokuwa na bafu wala vyoo kwa muda wa miezi minane. Kwa hiyo, hatukuweza kuoga wala kufua nguo zetu. Sote tulikuwa na chawa, na wakati wa usiku wadudu walitambaa juu ya miili yetu michafu.

Tuliamka saa kumi alfajiri. Tulikunywa tu kikombe kidogo cha kahawa asubuhi. Wakati wa adhuhuri tulikunywa kikombe kidogo cha supu na kula gramu 150 za mkate pamoja na uji kidogo. Hatukupewa chakula chochote jioni. Ijapokuwa nilikuwa na umri wa miaka 20 na hapo awali nilikuwa na afya nzuri, hatimaye nikawa mnyonge sana hivi kwamba sikuweza kutembea. Wafungwa wakaanza kufa kwa sababu ya njaa na magonjwa ya kuambukizwa.

Wakati huo, mfungwa mpya aliletwa kwenye chumba chetu cha gereza. Alikuwa yule kasisi mwenye ndevu nyingi wa Kanisa Othodoksi niliyemtaja mwanzoni. Alikuwa ameruhusiwa kubaki na Biblia yake. Lo! jinsi nilivyotamani kuisoma! Lakini nilipomwomba aniruhusu kuisoma alikataa. Hata hivyo, baadaye alinijia na kusema hivi: ‘Kijana, nitakuuzia Biblia yangu.’

“Kuniuzia? Nitakulipa nini?” nikamwuliza. “Mimi sina pesa.”

Ndipo aliposema kwamba angebadilisha Biblia yake kwa posho langu la mkate wa siku tatu. Badilishano hilo lilikuwa lenye manufaa sana. Ijapokuwa nilihisi njaa, nilipata chakula cha kiroho ambacho kiliniimarisha na hata kuwaimarisha wengine katika majaribu ya wakati huo wa taabu. Nimehifadhi Biblia hiyo hadi leo hii.—Mathayo 4:4.

Msimamo Wetu Unajaribiwa

Mnamo Juni 1943, vijana wa kiume Mashahidi wapatao 160, kutoka sehemu zote za Hungaria, walipelekwa Jászberény, mji uliokuwa karibu na Budapest. Mimi nilikuwa mmoja wao. Tulipokataa kuvaa kofia za wanajeshi na kubandikwa ukanda wenye rangi tatu kwenye mikono yetu, tuliingizwa katika mabehewa ya kubeba mizigo na kupelekwa kwenye kituo cha gari-moshi cha Budapest-Kőbánya. Huko, maofisa wa jeshi walisoma majina yetu, moja baada ya jingine, na kutuamuru tujiandikishe jeshini.

Tuliamriwa kusema: “Heil Hitler” yaani, “Hitler Atukuzwe.” Kila Shahidi alipokataa kufanya hivyo, alipigwa vibaya sana. Hatimaye, wanyanyasaji hao walichoka na mmoja wao akasema hivi: “Tutampiga mtu wa mwisho, naye hatanusurika.”

Tibor Haffner, mzee ambaye alikuwa Shahidi kwa muda mrefu, alikuwa na orodha ya Mashahidi waliokuwemo katika mabehewa hayo. Aliniambia hivi kwa sauti ya chini: “Ndugu, ni wewe. Uwe na moyo mkuu! Mtumaini Yehova.” Kisha nikaitwa. Niliposimama kwenye mlango wa behewa niliambiwa nishuke. Askari mmoja alisema: “Amekonda sana hivi kwamba hakuna mnofu wa kupiga.” Kisha akaniambia: “Ukijiandikisha kama ambavyo umeambiwa, tutahakikisha umepewa kazi ya kutayarisha chakula jikoni. La sivyo, utauawa.”

“Mimi sitajiandikisha jeshini, ninataka kurudi kwa ndugu zangu ndani ya mabehewa,” nikajibu.

Askari mmoja alinihurumia na kunitupa ndani ya behewa. Kwa kuwa nilikuwa na uzito wa chini ya kilogramu 40, ilikuwa rahisi kwake kufanya hivyo. Ndugu Haffner aliweka mkono wake kwenye mabega yangu, akanipapasa usoni, na kunukuu maneno ya Zaburi 20:1: “Mwenyezi-Mungu akujibu uwapo taabuni; jina la Mungu wa Yakobo likulinde.” (Biblia Habari Njema)

Katika Kambi ya Kazi Ngumu

Baada ya hapo tulipelekwa kwenye meli na kusafirishwa hadi Yugoslavia kupitia Mto Danube. Mnamo Julai 1943 tuliwasili kwenye kambi ya kazi ngumu karibu na jiji la Bor. Huko kulikuwepo mojawapo ya migodi mikubwa ya shaba huko Uingereza. Muda si muda, kulikuwa na watu 60,000 hivi katika kambi hiyo. Walitoka nchi nyingi, kutia ndani Wayahudi 6,000 hivi, na Mashahidi wa Yehova 160 hivi.

Mashahidi waliwekwa katika banda moja kubwa. Katikati kulikuwa na meza na mabenchi, na mara mbili kwa juma tulifanya mikutano yetu humo. Tulijifunza magazeti ya Mnara wa Mlinzi yaliyoingizwa kisiri kambini, na tukasoma ile Biblia ambayo nilinunua kwa kubadilishana na posho langu la mkate. Pia tuliimba na kusali pamoja.

Tulijaribu kudumisha uhusiano mzuri pamoja na wafungwa wengine na jambo hilo lilitufaidi. Ndugu mmoja alikuwa na maumivu makali ya matumbo, lakini maaskari walikataa kumpeleka kutibiwa. Hali yake ilipozidi kuwa mbaya, mfungwa mmoja Myahudi, aliyekuwa daktari, alikubali kumfanyia upasuaji. Alimpa ndugu huyo unusukaputi wa kizamani, na akafanya upasuaji kwa kutumia mkono ulionolewa wa kijiko. Ndugu huyo alipona na akarudi nyumbani baada ya vita.

Kazi katika migodi ilikuwa ngumu sana, na chakula kilikuwa haba. Ndugu wawili walifia kazini, na mmoja alikufa kwa ugonjwa. Mnamo Septemba 1944, jeshi la Urusi lilipokaribia, iliamuliwa kwamba kambi hiyo ifungwe. Singeamini yale yaliyotukia baadaye kama singeyaona kwa macho yangu.

Safari ya Kutisha

Baada ya kutembea kwa juma moja, sisi na wafungwa wengi Wayahudi tulifika Belgrade tukiwa tumechoka. Kisha tukaendelea kutembea tena kwa siku kadhaa na kuwasili katika kijiji cha Cservenka.

Tulipofika Cservenka, Mashahidi wa Yehova waliambiwa wajipange katika mistari, kila mstari ukiwa na watu watano. Kisha Shahidi mmoja akachukuliwa kwenye kila mstari wa pili. Tuliwatazama wale waliochukuliwa tukitokwa na machozi, kwa sababu tulifikiri walichukuliwa kuuawa. Lakini baada ya muda wakarudi. Ni nini kilitokea? Maaskari Wajerumani walitaka wachimbe makaburi, lakini kamanda mmoja wa jeshi la Hungaria alisema kwamba hawakuwa wamekula kwa juma moja na hawakuwa na nguvu za kufanya kazi.

Jioni hiyo, Mashahidi wote walipelekwa kwenye dari la jengo lililotumiwa kukausha matofali. Afisa mmoja Mjerumani alituambia: “Kaeni hapa na mnyamaze. Usiku huu utakuwa usiku mbaya sana.” Kisha akafunga mlango. Baada ya dakika chache tulisikia maaskari wakipiga kelele hivi: “Harakisheni! Harakisheni!” Kisha tukasikia milio ya bunduki, na baadaye kukawa kimya cha kuogopesha. Tena tukasikia, “Harakisheni! Harakisheni!” kisha risasi zikafyatuliwa tena.

Tuliweza kuona kile kilichokuwa kikiendelea kupitia kwenye paa. Maaskari walileta vikundi vya wafungwa Wayahudi na kuwaweka kwenye ukingo wa shimo, kisha wakawapiga risasi. Baadaye maaskari wakatupa mabomu ya mkono kwenye marundo ya maiti. Kulipopambazuka wanane tu kati ya wale wafungwa Wayahudi ndio waliokuwa hai na maaskari Wajerumani walikuwa wametoroka. Tulikuwa tumechoka na kufadhaika kabisa. János Török na Ján Bali, ambao bado wako hai, walikuwa miongoni mwa Mashahidi waliokuwepo wakati wa mauaji hayo.

Kuponea Chupuchupu

Tuliendelea na safari yetu kuelekea magharibi na kaskazini huku maaskari Wahungaria wakitulinda. Tena na tena tulishawishiwa tujiandikishe jeshini, lakini tulidumisha msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote na bado tukanusurika.

Mnamo Aprili 1945, tulifika katikati ya jeshi la Ujerumani na la Urusi katika jiji la Szombathely, lililoko karibu na mpaka wa Hungaria na Austria. Wakati shambulizi la ndege lilipotangazwa, kapteni mmoja Mhungaria, ambaye alikuwa mlinzi wetu, alituomba hivi: “Je, ninaweza kuambatana nanyi kutafuta kimbilio? Ninaona kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” Baada ya shambulizi hilo tuliondoka katika jiji hilo, huku tukipita mizoga ya wanadamu na wanyama.

Alipoona ya kwamba vita ilikuwa karibu kwisha, kapteni huyo alituita na kutuambia: “Asanteni kwa kuniheshimu. Hapa nina majani ya chai na sukari kwa kila mmoja wenu. Ni kitu kidogo tu.” Tulimshukuru kwa kututendea kwa huruma.

Warusi walifika baada ya siku chache, nasi tukaanza safari ya kurudi nyumbani tukiwa vikundi vidogo-vidogo. Lakini magumu yetu hayakuwa yamekwisha. Baada ya kufika Budapest, Warusi walitutia gerezani na kutuamuru tujiandikishe katika jeshi la Sovieti.

Mwanamume aliyesimamia shughuli hiyo alikuwa daktari, afisa Mrusi mwenye cheo cha juu. Tulipoingia chumbani mwake hatukumtambua, lakini yeye alitutambua. Tulikuwa pamoja naye kwenye kambi ya kazi ngumu huko Bor, naye alikuwa mmojawapo wa wale Wayahudi wachache walionusurika yale mauaji yaliyofanywa na Wanazi. Alipotuona, aliwaambia maaskari hivi: “Acha wanaume hawa wanane warudi nyumbani kwao.” Tulimshukuru, lakini zaidi ya yote tulimshukuru Yehova kwa ulinzi wake.

Tumaini Langu Halijafifia

Hatimaye, nilifika nyumbani huko Pácin mnamo Aprili 30, 1945. Muda mfupi baadaye nilirudi huko Streda nad Bodrogom kwa yule mtu aliyekuwa akinifundisha uhunzi ili nimalize mazoezi yangu. Akina Pankovic walikuwa wamenifundisha ufundi ulioniwezesha kujiruzuku maishani, na jambo la maana zaidi ni kwamba walikuwa wamenifundisha kweli za Biblia zilizobadili maisha yangu. Sasa walinipa kitu kingine tena. Mnamo Septemba 23, 1946, nilimwoa Jolana, binti yao mrembo.

Mimi na Jolana tuliendelea kufanya shughuli zetu za kawaida za kujifunza Biblia na kuhubiri. Kisha, mwaka wa 1948, tukabarikiwa kupata mwana wetu, Andrej. Hata hivyo, shangwe yetu ya kuwa na uhuru wa kidini haikudumu. Punde, Wakomunisti wakaanza kumiliki nchi yetu, na mnyanyaso ulianza upya. Mwaka wa 1951, wenye mamlaka Wakomunisti huko Chekoslovakia waliniagiza nijiandikishe jeshini. Nilipatwa na mambo yaleyale niliyokuwa nimepitia hapo awali: kushtakiwa mahakamani, kuhukumiwa kifungo gerezani, kufungwa, kufanya kazi ngumu, na njaa. Lakini kwa msaada wa Mungu nilinusurika tena. Nilisamehewa na kuachiliwa mwaka wa 1952 na nikajiunga na familia yangu huko Ladmovce, Slovakia.

Ijapokuwa huduma yetu ya Kikristo ilipigwa marufuku kwa miaka 40 hivi, tuliendelea na utumishi wetu mtakatifu. Kuanzia 1954 hadi 1988 nilikuwa na pendeleo la kutumikia kama mwangalizi asafiriye. Wakati wa miisho-juma nilitembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova na kuwatia ndugu na dada moyo waendelee kudumisha uaminifu wao. Kisha, katikati ya juma nilikaa pamoja na familia yangu nikifanya kazi ili kupata riziki. Wakati huo wote tulihisi kwamba Yehova alituongoza kwa upendo. Niliona ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi: “Kama si BWANA aliyekuwa pamoja nasi, wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, hasira yao ilipowaka juu yetu.”—Zaburi 124:2, 3.

Mimi na Jolana tulifurahi wakati mwana wetu Andrej alipooa na hatimaye akawa mwangalizi Mkristo mkomavu. Mke wake, Eliška, na wana wao wawili Radim na Daniel, pia wakawa wahudumu Wakristo wenye bidii. Kisha, mwaka wa 1998 nilihuzunika sana mpenzi wangu Jolana alipokufa. Jaribu hilo ni gumu kuliko mengine yote ambayo nimewahi kuvumilia. Ninamkosa kila siku, lakini tumaini la ufufuo hunifariji.—Yohana 5:28, 29.

Sasa nina umri wa miaka 79, nami ninatumikia nikiwa mzee katika kutaniko moja kwenye kijiji cha Slovenské Nové Mesto, Slovakia. Ninafurahi sana kuwaeleza majirani wangu kuhusu tumaini langu zuri la Biblia. Ninapotafakari mambo yaliyopita, na utumishi wangu kwa Yehova kwa zaidi ya miaka 60, nina hakika kwamba kwa msaada wa Yehova tunaweza kushinda vikwazo na majaribu yote. Matazamio yangu na matumaini yangu yanapatana na maneno ya Zaburi 86:12: “Nitakusifu Wewe, Bwana, Mungu wangu, kwa moyo wangu wote, nitalitukuza jina lako milele.”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Hii ndiyo Biblia niliyopata kwa kupeana posho langu la mkate

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tibor Haffner alinitia moyo katika majaribu yangu

[Picha katika ukurasa wa 22]

Mashahidi katika kambi ya kazi ngumu ya Bor

[Picha katika ukurasa wa 22]

Mazishi ya Shahidi kwenye kambi ya kazi ngumu ya Bor yaliyohudhuriwa pia na maaskari Wajerumani

[Picha katika ukurasa wa 23]

János Török na Ján Bali (picha ndogo), ambao walikuwapo wakati wa yale mauaji ya Wayahudi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nilimwoa Jolana mnamo Septemba 1946

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa pamoja na mwanangu, mke wake, na wajukuu wangu