Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanya Nini ili Niwe Mwenye Kuvutia Zaidi?

Ninaweza Kufanya Nini ili Niwe Mwenye Kuvutia Zaidi?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza Kufanya Nini ili Niwe Mwenye Kuvutia Zaidi?

“Haikuwa rahisi kuzungumza na wasichana. Sikujua mambo waliyofikiria, jinsi walivyohisi, au namna walivyoona mambo.”—Tyler.

WASICHANA hupenda wavulana wenye sifa gani? “Wenye uhakika” asema msichana aitwaye Emily. Robyn, msichana mwingine, asema kwamba yeye hupenda wavulana wacheshi. Vipi wavulana, wao hupenda wasichana wenye sifa gani? Haishangazi kwamba uchunguzi mmoja ulionyesha kuwa wanapendezwa hasa na wasichana wenye sura ya kuvutia. Wavulana hao walisema kwamba jambo kuu la sita wanalopenda ni wasichana wenye mapendezi na maadili kama yao.

Makala na uchunguzi kuhusu mahusiano kati ya wavulana na wasichana hupatikana katika magazeti ya vijana. Ni wazi kwamba vijana wengi hufikiria sana au hata huhangaishwa na namna watu wa jinsia tofauti wanavyowaona. Huenda ikawa hata wewe huhangaishwa na jambo hilo wakati mwingine. Hilo halimaanishi kwamba uko tayari kuoa au kuolewa karibuni. Ni kwamba tu hakuna asiyetaka kuvutia au kupendeza! Tyler anasema: “Ukiwa kijana, unataka kumvutia kila mtu. Unataka kukubaliwa na marika wako, wavulana kwa wasichana.” Huenda ukahisi pia kwamba siku moja utahitaji kutafuta mwenzi wa ndoa anayefaa. Wakati huo ufikapo, bila shaka utataka kumvutia mtu huyo.

Hata hivyo, ukiwa kijana Mkristo, huenda huna ujuzi mwingi kuhusu jinsi ya kushughulika na watu wa jinsia tofauti. Huenda pia ukataka maumbile yenye kuvutia kwa sababu ya kushawishiwa na marika wako. Unapoona wanamitindo wenye kuvutia na waigizaji wenye misuli mingi katika televisheni na magazetini, huenda ukahisi kuwa hufai na kwamba hufikii viwango vinavyohitajiwa! Basi ni nini kinachohitajiwa ili kuwavutia wengine kutia ndani watu wa jinsia tofauti kwa njia inayofaa?

Upumbavu wa Kutaka Kuwa na Umbo “Kamilifu”

Mwanasaikolojia William S. Pollack anasema kwamba kwa sababu ya kushawishiwa na ulimwengu wa burudani, vijana wengi “hujitahidi sana kupunguza uzito na kubadili umbo lao la mwili kwa kujinyima chakula, kujenga misuli na kufanya mazoezi kwa muda mrefu.” Ili kupata huo mwili “mkamilifu,” wengine hata wamejihatarisha zaidi kwa kujinyima chakula kabisa. Hata hivyo, Kituo cha Utafiti wa Masuala ya Jamii kinasema hivi: “Kwa habari ya umbo na uzito, ni asilimia isiyozidi 5 tu ya idadi ya wanawake wanaofikia kiwango cha sasa cha urembo. Na asilimia 1 hivi ya idadi ya wanawake ndio tu wanaoweza kufikia kiwango cha umbo na sura nzuri.”

Shauri la Biblia katika Waroma 12:2 linafaa: “Msiruhusu ulimwengu unaowazunguka uwasonge katika muundo wake.” (Phillips) Hilo halimaanishi kwamba hupaswi kujali unavyoonekana. Ni jambo la busara kutunza mwili wako kwa kufanya mazoezi ya kiasi na kula chakula chenye lishe bora. (Waroma 12:1; 1 Timotheo 4:8) Kupumzika na kulala vya kutosha kunaweza pia kukufanya ujihisi vizuri na uonekane maridadi. Wakati huohuo, zingatia usafi na jinsi unavyojipamba. Kijana mmoja Mwingereza aitwaye David anasema hivi: “Kuna msichana ambaye ni mwenye kuvutia sana, lakini yeye hunuka. Na kwa sababu hiyo watu humhepa.” Basi oga kwa ukawaida, nawa mikono, osha nywele, na kata kucha zako na kwa kufanya hivyo utaboresha sura yako.

Ijapokuwa Biblia inakataza kutilia mkazo sana unachovalia, inawashauri Wakristo “wajirembe wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.” (1 Timotheo 2:9) Valia mavazi yenye kupendeza na ya kiasi. * Kuzingatia sura yako kwa njia inayofaa kutaboresha hali yako ya kujistahi. Kijana aitwaye Paul aeleza hivi: “Huenda usiwe mwenye kuvutia sana, lakini unaweza kuboresha sura yako.”

Sifa za Moyoni

Ijapokuwa sura na umbo zuri huvutia, hatimaye “urembo ni povu tu.” (Mithali 31:30, Byington) Sura nzuri ni ya muda tu, na haiwezi kamwe kuchukua mahali pa sifa nzuri zenye kuvutia za mtu. (Mithali 11:22) Kumbuka pia kwamba, “wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Kwa hiyo, badala ya kuzingatia wembamba wa kiuno chako, au ukubwa wa misuli yako, remba “yule mtu wa siri wa moyoni katika vao lisilofisidika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” (1 Petro 3:3, 4; Waefeso 4:24) Ni kweli kwamba vijana wengi leo hawaoni umuhimu wa kuwa na sifa zenye kuvutia wala hawajali sifa za kiroho. * Lakini wale wanaofuata kanuni za Mungu huthamini sifa hizo na kuziona kuwa zenye kuvutia!

Basi, njia bora zaidi ya kuwavutia wanaume na wanawake Wakristo wa kiroho ni wewe mwenyewe kuwa mtu wa kiroho. Kuza hali yako ya kiroho kupitia sala, funzo la kibinafsi la Biblia, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. (Zaburi 1:1-3) Hata hivyo, unaweza kukuza sifa na stadi nyingine nzuri. Huhitaji kufanya urafiki na mtu wa jinsia tofauti au kuwa na uhusiano wa kimapenzi ili kukuza sifa hizo. Unaweza kujizoeza sifa hizo kila siku unaposhughulika na wengine.

Kwa mfano, je, wewe hubabaika au kuona haya unapokuwa na mtu wa jinsia tofauti? Kijana aitwaye Paul asema hivi: “Wakati mwingine mimi hubabaika ninapokuwa miongoni mwa wasichana kwa sababu siwaelewi kama vile ninavyowaelewa wavulana. Na sitaki kujiaibisha mbele yao.” Unawezaje kukuza utulivu ambao utawastarehesha wengine? Njia moja ni kwa kushirikiana na washiriki mbalimbali katika kutaniko la Kikristo. Unapokuwa mikutanoni, onyesha kwamba hupendezwi tu na watu wa jinsia tofauti wa rika lako, bali pia watoto, watu wazima, na wazee-wazee. (Wafilipi 2:4) Kujua jinsi ya kushughulika vizuri na watu wa aina mbalimbali kutakusaidia kukuza hali yako ya kuwa na uhakika.

Hata hivyo, uwe mwangalifu. Yesu alisema: “Lazima upende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 19:19) Ikiwa una uhakika, hutababaika unapokuwa na wengine. * Hata hivyo, ijapokuwa ni vizuri “kujistahi kwa kiasi fulani,” angalia usipite kiasi. Mtume Paulo alisema: “Naambia kila mtu huko miongoni mwenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.”—Waroma 12:3.

Chunguza kwa makini tabia zako na jinsi unavyoshughulika na wengine. Msichana mmoja Mwingereza, anayeitwa Lydia, asema hivi: “Kuna mvulana shuleni kwetu anayependwa sana na wasichana. Lakini wasichana hao wanapopata kumjua vizuri, wao humchukia sana kwa sababu hana adabu wala busara.” Watu huvutiwa na mtu anayesema kwa fadhili na busara na anayewajali wengine. (Waefeso 4:29, 32; 5:3, 4) “Tabia zinazovutia ni kama cheti cha kusafiria, zinawapa watu uhuru wa kuwafikia wengine,” asema Dakt. T. Berry Brazelton. Tabia nzuri “ni muhimu ili kukubaliwa na wengine.”

Ulimwenguni pote desturi na sheria zinazohusu tabia nzuri zinatofautiana. Kwa hiyo huenda ukataka kuchunguza namna wanaume na wanawake Wakristo walio wakomavu wanavyotendeana. Kwa mfano, ni vizuri kujua kama ni desturi ya nchi yenu mwanamume kumfungulia mwanamke mlango. Ukijizoeza kufanya hivyo utaboresha sifa zako za kuwa mtu mwenye tabia nzuri.

Hatimaye, itakuwa vyema pia ukisitawisha usawaziko kwa habari ya ucheshi. Biblia husema kwamba kuna “wakati wa kucheka,” na mtu mwenye sifa za ucheshi huwa na rafiki wengi.—Mhubiri 3:1, 4.

Kuwa Mwenye Urafiki au Kuchezea-chezea Watu?

Kitabu kinachodai kufanikisha urafiki kati ya watu wa jinsia tofauti kilishauri kwamba siri ya kuvutia watu wa jinsia tofauti ni kuwachezea-chezea kimapenzi. Wasomaji waliambiwa wajizoeze kutabasamu, kumtazama mtu ana kwa ana na kuwa na ‘utangulizi’ bora. Shauri hilo linapingana na shauri la Paulo kwa Timotheo la kuwatendea washiriki wa jinsia tofauti “kwa usafi wote wa kiadili.”—1 Timotheo 5:2.

Kuchezea-chezea wengine kimapenzi ni kutenda kwa unafiki na udanganyifu ijapokuwa anayefanya hivyo huenda akataka sifa. Hupaswi kuchezea-chezea wengine kimapenzi au kuwatania-tania ili kuendeleza mazungumzo yenye kupendeza. Wala huhitaji kuuliza maswali yenye kuaibisha au yasiyofaa ili kujua jinsi mtu wa jinsia tofauti anavyohisi na kufikiri. Endelea kuzungumza mambo yaliyo ya ‘kweli, yaliyo safi kiadili, na ya kupendeka,’ na hivyo utaonyesha kwamba unaendelea kukomaa na kuwa mwanamume au mwanamke wa kiroho. (Wafilipi 4:8) Utii wako kwa viwango vya Mungu utakufanya uvutie si kwa watu wa jinsia tofauti tu bali kwa Mungu mwenyewe. *Mithali 1:7-9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona makala ya “Vijana Huuliza . . . Ni Nini Siri ya Kuchagua Nguo Zifaazo?” katika toleo letu la Mei 8, 1990.

^ fu. 12 Mtafiti mmoja alisema kwamba uchunguzi unaonyesha kuwa vijana werevu hudhihakiwa mara nyingi. Baadhi yao hujifanya kuwa wajinga ili kuepuka dhihaka hizo.

^ fu. 15 Katika sura ya 12 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kuna madokezo mengi kuhusu namna ya kukuza sifa ya kujistahi.

^ fu. 21 Iwapo hujafikia umri wa kuoa au kuolewa, ni jambo la busara kuwa na watu wa jinsia tofauti katika kikundi kilicho na mchanganyiko wa watu mbalimbali. Ona makala ya “Vijana Huuliza . . . Vipi Ikiwa Wazazi Wangu Wanafikiri Mimi Ni Mchanga Mno Kuweka Miadi ya Kijinsia?” katika toleo la Amkeni! la Januari 22, 2001.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Badala ya kufikiria sana juu ya sura yako, kuza sifa za kiroho

[Picha katika ukurasa wa 15]

Jifunze kuwa huru na watu wa aina zote