Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipambana na Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua

Nilipambana na Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua

Nilipambana na Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua

Nilimwangalia mume wangu alipocheza kwa furaha na binti yetu aliyezaliwa karibuni nikiwaza kwamba maisha yao yangekuwa yenye furaha zaidi kama singekuwapo. Nilihisi kwamba nilikuwa mzigo kwao. Nilitaka kutoroka nisirudi kamwe. Sikujua kwamba nilikuwa na ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua.

MIAKA kumi ya kwanza ya ndoa yangu ilikuwa yenye furaha. Mimi na Jason tulifurahia kumlea binti yetu wa kwanza anayeitwa Liana. Kwa hiyo, nilipokuwa mja-mzito tena, sisi sote tulifurahi.

Lakini sikuwa na afya nzuri nilipokuwa na mimba hiyo. Hata nilikuwa karibu kufa baada ya kujifungua kwa sababu ya matatizo ya afya. Lakini hata kabla ya kujifungua, mwishoni mwa kipindi cha ujauzito, ni kana kwamba nilichanganyikiwa. Hali yangu ilizidi kuwa mbaya nilipotoka hospitalini na kurudi nyumbani pamoja na Carly, binti yetu mdogo. Nilikuwa nimechoka daima na nilihisi kwamba sikuweza kufanya hata maamuzi madogo. Nilikuwa nikimpigia Jason simu mara nyingi kila siku kumwuliza kazi za nyumbani ambazo ninapaswa kufanya, au kama nilikosea niliposema au kufanya jambo fulani.

Niliogopa kuwa pamoja na watu wengine, hata marafiki wa zamani. Mtu alipobisha mlango bila kutazamiwa nilijificha katika chumba cha kulala. Sikusafisha nyumba, na nilikengeushwa kwa urahisi na kuchanganyikiwa. Mimi hupenda sana kusoma, lakini wakati huo sikuweza kusoma hata kidogo kwa kuwa sikuweza kumakinika niliposoma. Hali yangu ya kiroho ikawa mbaya kwa sababu sikuweza kusali. Sikuweza kuhisi upendo kwa mtu yeyote, ni kana kwamba moyo wangu ulikuwa umekufa ganzi. Nilihofia kwamba watoto wangu wangeathiriwa kwa sababu nilichanganyikiwa. Sikuweza kujiheshimu. Nilifikiri ninarukwa akili.

Nilipokuwa mgonjwa, Jason alikuwa akinisaidia kusafisha nyumba au kutayarisha chakula kwa ajili ya familia baada ya kazi, nami nilimkasirikia aliponisaidia! Nilihisi kwamba kusaidia kwake kulionyesha kwamba mimi sikuwa mama mzuri. Kwa upande mwingine, alipokosa kunisaidia, nilimwambia kwamba hakunijali. Kama Jason hangalishughulikia mambo kwa hekima na kwa upendo, huenda ugonjwa wangu wa kushuka moyo baada ya kujifungua ungaliharibu ndoa yetu. Jason anaweza kueleza vizuri zaidi jinsi ugonjwa wangu ulivyomwathiri.

Mume Wangu Aeleza Jinsi Alivyoathiriwa

“Kwanza, sikuelewa kile kilichokuwa kikimpata Janelle. Alibadilika kabisa. Hakuwa tena mchangamfu na mwenye furaha. Utu wake ulibadilika kabisa. Alianza kufikiri nilimlaumu kila wakati, na hata aliudhika nilipojaribu kumsaidia kazi. Mwanzoni, nilitaka kumwambia aache tabia hiyo na kujidhibiti. Lakini nilitambua kwamba kumwambia hivyo hakungemsaidia hata kidogo.

“Uhusiano wetu ulikuwa taabani. Ni kana kwamba Janelle alifikiri watu wote walimchukia. Nilikuwa nimesikia juu ya wanawake wengine waliokuwa na dalili hizo kwa sababu ya ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua. Kwa hiyo, nilipoanza kushuku kwamba Janelle alikuwa na ugonjwa huo, nilianza kusoma vichapo vyote nilivyoweza kupata kuhusu ugonjwa huo. Kile nilichosoma kilinisadikisha kwamba Janelle alikuwa na ugonjwa huo. Nilijifunza pia kwamba Janelle hakupaswa kulaumiwa. Hakupata ugonjwa huo kwa sababu ya kutotunza afya yake.

“Ni kweli kwamba nilichoka sana kihisia na kimwili kwa sababu ya kazi ya ziada ya kumtunza Janelle na watoto. Kwa muda wa miaka miwili nilijitahidi kutimiza madaraka yote, nikiwa mzee wa kutaniko na nikiwa mume na baba, huku nikifanya kazi ya kuajiriwa. Nilipata ruhusa ya kutoka kazini mapema, hasa siku za mikutano ya Kikristo. Jambo hilo lilinisaidia sana. Janelle alihitaji kusaidiwa kutayarisha chakula cha jioni na kuvalisha watoto. Kwa hiyo, sisi sote tuliweza kuhudhuria mikutano yote.”

Jinsi Nilivyopata Nafuu

Bila shaka nilipona haraka kwa sababu ya msaada na upendo wa mume wangu. Jason alinisikiliza kwa subira nilipomwambia juu ya mambo niliyohofia. Niliona kwamba ni muhimu sana kwangu kumwelezea mtu mwingine jinsi nilivyohisi. Hata nyakati nyingine niliongea kana kwamba nilikuwa nimekasirika. Lakini Jason aliniambia kila wakati kwamba alinipenda na angenisaidia kupambana na ugonjwa huo. Sikuzote alijitahidi kunisaidia kuwa na maoni yanayofaa. Baadaye nilimwomba msamaha kwa sababu ya yale niliyokuwa nimesema kwa hasira. Alinitia moyo kwa kusema kwamba niliongea hivyo kwa sababu ya ugonjwa wangu. Sasa ninatambua kwamba maneno yake yenye upendo yalinisaidia sana.

Hatimaye, tulipata daktari mzuri aliyesikiliza kwa subira nilipomweleza jinsi nilivyohisi. Alitambua kwamba nilikuwa na ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua na kupendekeza nitumie dawa kutuliza wasiwasi uliozuka kwa ghafula mara nyingi. Pia, alipendekeza nimwone daktari wa akili. Zaidi ya hayo, alipendekeza nifanye mazoezi kwa ukawaida, jambo ambalo limewasaidia wengi kupambana na kushuka moyo.

Jambo moja lililonizuia nisipone haraka ni kuona aibu. Watu wengi huona ugumu kumhurumia mtu aliye na ugonjwa ambao hawaelewi. Ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua si kama kuvunjika mguu. Watu wanaweza kuuona mguu uliovunjika, kwa hiyo, wao humwonea huruma mtu aliyevunjika mguu. Hata hivyo, familia yangu na marafiki wa karibu walinisaidia sana na walielewa hali yangu.

Msaada Kutoka kwa Familia na Marafiki Wenye Upendo

Mimi na Jason tulithamini sana msaada wa mama yangu nilipokuwa mgonjwa. Nyakati nyingine Jason alihitaji kupumzika. Mama alinitia moyo kila wakati na hakuingilia kazi yangu. Badala yake, alinisaidia na kunitia moyo kufanya kile nilichoweza.

Marafiki katika kutaniko pia walinisaidia sana. Wengi walinitumia barua fupi kuniambia kwamba walinifikiria. Nilithamini sana maneno hayo yenye upendo! Barua hizo zilikuwa zenye kutia moyo hasa kwa sababu sikuweza kuongea na watu uso kwa uso, wala kwa simu. Hata niliona vigumu kuongea na Wakristo wenzangu kabla na baada ya mikutano. Kwa hiyo, kwa kutuandikia barua, marafiki wetu walionyesha kwamba walielewa hali yangu na vilevile kuonyesha kwamba walinipenda na kunijali mimi na familia yangu.

Unaweza Kupona!

Sasa nimepata nafuu, kwa sababu ya ushauri mzuri wa daktari wangu, na msaada wa familia yangu na marafiki wanaojali. Bado ninafanya mazoezi kwa ukawaida, hata nikiwa nimechoka, kwa kuwa mazoezi yamenisaidia kupata nafuu. Pia, ninajaribu kuitikia ifaavyo wengine wanaponitia moyo. Ninaposhuka moyo mimi huzisikiliza kaseti za Biblia na muziki wa Kingdom Melodies, ambao ni wenye kuchangamsha na kujenga kiroho. Muziki huo ulitungwa na Mashahidi wa Yehova. Vifaa hivyo vizuri huniimarisha kiroho na kunisaidia kufikiri vizuri. Hivi majuzi, nilianza tena kutoa hotuba za wanafunzi za Biblia kwenye mikutano ya kutaniko.

Sasa, baada ya zaidi ya miaka miwili na nusu ninaweza kuhisi na kuonyesha upendo kikamili zaidi kwa mume wangu, watoto wangu, na wengine. Ijapokuwa hiyo ilikuwa pindi ngumu kwa familia yangu, hatujawahi kuwa na uhusiano wa karibu kama wakati huu. Hasa ninamshukuru Jason ambaye alionyesha kwa kila njia kwamba ananipenda. Alivumilia nilipokuwa nimeshuka moyo sana na sikuzote alikuwa tayari kunisaidia nilipohitaji msaada. Zaidi ya yote, sasa mimi na mume wangu tuna uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, ambaye alitupatia nguvu ya kuvumilia majaribu yetu.

Bado ninashuka moyo mara kwa mara, lakini kwa msaada wa familia yangu, daktari wangu, kutaniko, na roho takatifu ya Yehova, ninaendelea kupata nafuu. Naam, mtu aliye na ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua anaweza kupona. Ugonjwa huo ni adui anayeweza kushindwa.—Imesimuliwa na Janelle Marshall.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

Visababishi vya Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua

Mbali na mabadiliko ya viwango vya homoni, mambo mengine yanaweza kusababisha ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua. Baadhi ya visababishi hivyo ni:

1. Maoni yasiyofaa ya mwanamke mwenyewe kuhusu daraka lake akiwa mama, ambayo huenda yakasababishwa na maisha ya utotoni ambayo hayakuwa yenye furaha na kutokuwa na uhusiano mzuri pamoja na wazazi.

2. Kulemewa na mambo mengi ambayo akina mama hutarajiwa kufanya.

3. Uwezekano wa kupata ugonjwa huo kwa kuwa watu wengine wa jamaa wana ugonjwa huo.

4. Kukosa furaha katika ndoa, na kutojali kwa watu wa familia na wa ukoo.

5. Kutojiheshimu.

6. Kulemewa na kazi nyingi na madaraka mazito ya kuwatunza watoto wachanga wakati wote.

Hatujataja visababishi vyote. Kuna mambo mengine yanayoweza kusababisha ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua. Naam, visababishi vyake vyote havijatambuliwa bado.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

Hiyo Si Huzuni ya Kawaida Baada ya Kujifungua

Ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua si sawa na huzuni ya kiasi ambayo wanawake wengi huhisi baada ya kujifungua. Dakt. Laura J. Miller anasema hivi: ‘Kwa kawaida wanawake waliojifungua karibuni huhisi huzuni kidogo. Asilimia 50 hivi ya wanawake waliojifungua hupatwa na hali hii ambayo inawafanya walie. Hali hiyo hutokea hasa kati ya siku ya tatu na ya tano baada ya kujifungua. Kisha huzuni hiyo ya kiasi hupungua polepole na kuisha baada ya majuma machache.’ Watafiti wanadhani kwamba huzuni hiyo husababishwa na mabadiliko katika viwango vya homoni baada ya kuzaa.

Tofauti na huzuni hiyo ya kiasi, ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua unahusisha hisia za kushuka moyo kwa muda mrefu zinazoweza kuanza baada tu ya kujifungua au hata majuma au miezi kadhaa baadaye. Mama aliye na ugonjwa huo anaweza kuwa mchangamfu sana dakika moja na kushuka moyo kufikia kutaka kujiua muda mfupi baadaye. Isitoshe, huenda akakasirika na kuudhika upesi. Anaweza kuhisi kwamba hafai kuwa mama au kukosa kumpenda mtoto wake. Dakt. Miller anasema hivi: ‘Baadhi ya akina mama walio na ugonjwa wa kushuka moyo hujua akilini kwamba wanawapenda watoto wao. Hata hivyo, wao huudhika, huwakasirikia watoto wao, na kuchukizwa nao. Wengine hufikiria kuwaumiza au hata kuwaua watoto wao.’

Ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua umekuwapo tangu zamani za kale. Daktari Mgiriki Hippocrates, aliyeishi katika karne ya nne K.W.K., alitambua mabadiliko makubwa katika mtazamo wa wanawake waliojifungua. Uchunguzi uliochapishwa katika jarida la Brazilian Journal of Medical and Biological Research unasema hivi: “Asilimia 10-15 ya akina mama katika nchi nyingi hushuka moyo baada ya kujifungua.” Hata hivyo, jambo la kuhuzunisha ni kwamba “ugonjwa huo hautambuliwi mara nyingi na wanawake wengi hawapati matibabu yanayofaa,” jarida hilo likasema.

Hali mbaya hata zaidi inayoweza kutokea baada ya kujifungua ni ugonjwa wa akili, ijapokuwa huo si wa kawaida sana. Mgonjwa anaweza kuona maono, kusikia sauti akilini, na kutoweza kutofautisha mambo halisi na yale yasiyo halisi, huku akirudia hali ya utimamu kwa muda wa saa chache au siku kadhaa. Visababishi vya ugonjwa huo wa akili havijulikani, lakini Dakt. Miller anasema kwamba “kisababishi kikuu kinaweza kuwa udhaifu uliorithiwa ambao unasababisha ugonjwa wakati viwango vya homoni vinapobadilika.” Daktari mwenye ujuzi anaweza kutibu ugonjwa wa akili unaotokea baada ya kujifungua.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

Jinsi ya Kujisaidia Kupona *

1. Ikiwa hali ya kushuka moyo inaendelea, mwone daktari. Enda ukamwone daktari haraka iwezekanavyo, ili upone upesi. Tafuta daktari anayejali ambaye anaelewa ugonjwa huo. Usihisi aibu kwa sababu ya ugonjwa wako wala usione haya ukihitaji kutumia dawa.

2. Fanya mazoezi kwa ukawaida. Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba mazoezi yanayofanywa kwa ukawaida yanaweza kupunguza kushuka moyo.

3. Waambie watu wa familia na rafiki wa karibu jinsi unavyohisi. Usijitenge na watu wala kuficha hisia zako.

4. Kumbuka kwamba kuna kazi nyingine za nyumbani ambazo si lazima ufanye sikuzote. Rahisisha maisha yako kwa kushughulikia tu mambo muhimu.

5. Sali ili upate nguvu ya kuvumilia. Omba mtu mwingine atoe sala pamoja nawe ukiona vigumu kusali peke yako. Ili upone haraka jitahidi kuondoa hisia za hatia au kuhisi kwamba hufai kitu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 39 Gazeti la Amkeni! halipendekezi matibabu yoyote hususa. Mapendekezo ambayo yametolewa kwa wanawake na wanaume katika makala hii hayazungumzii hali zote, na huenda hoja nyingine haziwahusu wagonjwa fulani.

[SAnduku katika ukurasa wa 23]

Mapendekezo kwa Wanaume

1. Tambua kwamba mke wako hakujiletea ugonjwa huo wa kushuka moyo. Ikiwa haponi, mnaweza kusaidiana kutafuta daktari anayejali ambaye anaelewa ugonjwa huo.

2. Msikilize mke wako kwa subira. Tambua hisia zake. Usimkasirikie kwa sababu hawezi kutambua mambo mazuri yaliyopo, na ujitahidi kwa upendo kumsaidia ayatambue. Mhakikishie kwamba atapona. Usifikiri ni lazima uwe na masuluhisho ya matatizo yote anayotaja. Huenda ikawa anataka tu kufarijiwa, bali si kupata masuluhisho. (1 Wathesalonike 5:14) Kumbuka kwamba ni vigumu kwa wagonjwa hao kufikiri vizuri.

3. Punguza shughuli zisizo muhimu ili uwe na wakati mwingi zaidi wa kumsaidia mke wako. Ukifanya hivyo huenda akapata nafuu upesi.

4. Usisahau kupumzika vya kutosha. Ukiwa na afya nzuri ya kimwili na akili, na hali nzuri ya kiroho utaweza kumsaidia mke wako vizuri zaidi.

5. Zungumza na mtu fulani anayeweza kukusaidia, kama vile mwanamume mwingine aliye mkomavu kiroho ambaye mke wake amekuwa na ugonjwa huo.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Familia ya Marshall