Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujifunza Kutokana na Wakristo wa Karne ya Kwanza

Kujifunza Kutokana na Wakristo wa Karne ya Kwanza

Kujifunza Kutokana na Wakristo wa Karne ya Kwanza

“Jihadharini: labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.

HIVYO ndivyo mtume Paulo alivyowaonya Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu hatari za kufuata falsafa za wanadamu bila kufikiri. Wangeweza kushikamana na mwongozo wenye kutegemeka ambao Yesu na mitume wake waliwapa, mafundisho ambayo tayari yalikuwa yamewaletea faida nyingi, au wangedanganywa na maoni ya wanadamu yenye kubadilika-badilika, ambayo yalikuwa yamewaletea mamilioni ya watu fadhaa na taabu.—1 Wakorintho 1:19-21; 3:18-20.

Kuishi “Kulingana na Kristo”

Wapiganaji waliohusika katika zile Vita za Dini miaka ipatayo elfu moja iliyopita hawakutambua kwamba kuishi “kulingana na Kristo” kunahusisha mengi zaidi ya kudai kumwamini Yesu Kristo. (Mathayo 7:21-23) Kunahusisha kufuata kabisa mafundisho ya Yesu yanayopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. (Mathayo 7:15-20; Yohana 17:17) Yesu Kristo alisema hivi: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.” (Yohana 8:31) Alisema kwamba “wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—Yohana 13:35.

Kwa kweli, wapiganaji wa zile Vita za Dini walipotoshwa na “udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.” Na haishangazi kwamba watu wa kawaida walidanganywa wakati viongozi wao wa kidini, naam, maaskofu wao, “walipojulikana wazi kuwa wanajeshi.” Kitabu Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature, cha McClintock na Strong, kinasema kwamba “roho ya vita ilikuwepo sana miongoni mwa makasisi hivi kwamba wakati wowote ambapo faida yoyote ingeweza kupatikana [kupitia vita], walikuwa tayari kupigana.”

Ni nini kilichosababisha hali hiyo ya kuhuzunisha? Baada ya kifo cha mitume Wakristo wa karne ya kwanza, viongozi wa kidini waasi-imani walizidi kupotosha mafundisho ya Kristo, kama vile Neno la Mungu lilivyokuwa limetabiri. (Matendo 20:29, 30) Dini iliyopotoka ikazidi kujihusisha na serikali hatua kwa hatua. Katika karne ya nne, yasemekana kwamba Maliki Mroma Konstantino alibadili dini na kuwa Mkristo alipokuwa karibu kufa. Halafu, kitabu Cyclopedia kinasema kwamba, “kubadili zile bendera zenye sanamu kuwa bendera yenye Msalaba kuliwawajibisha Wakristo wote kuwa wanajeshi.”

Ni wazi kwamba Wakristo hawakuwa kamwe na wajibu huo. Lakini “hoja zenye kushawishi” za falsafa za wanadamu ziliwakengeusha wasifuate kabisa mfano wa Kristo. (Wakolosai 2:4) Hoja fulani zenye udanganyifu mwingi zimetumiwa kwa muda mrefu ili kuthibitisha uhalali wa vita na mapambano ya wanadamu. Hata hivyo, kama vile kitabu Cyclopedia kinavyosema, mtu mwenye huruma au mtu wa Mungu anayejihusisha na ‘matendo ya ukatili ya vita, kama ilivyokuwa katika nyakati za kale au katika nyakati zetu, hawezi hata kidogo kusemwa kuwa anafuata kanuni za Ukristo.’

Mbali na dini zinazodai kuwa za Kikristo, dini nyingine pia zimejihusisha katika vita katika karne zote zilizopita. Sawa na makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo, watu wa dini hizo pia wamewachinja watu wa dini zao na wa dini nyingine kwa sababu ya tofauti za kitaifa, kisiasa, na za kidini. Dini hizo zimetumia ujeuri au vitisho ili kubadili imani ya watu. Baadhi ya dini hizo zimeshiriki katika mauaji makubwa ili kujaribu kutimiza malengo yake. Dini hizo hazitofautiani hata kidogo na dini zinazodai kuwa za Kikristo.

Kujitenga na Ulimwengu

Wakristo wa karne ya kwanza waliwezaje kujitenga na vita vyenye ukatili na siasa za wakati wao? Kanuni mbili kuu ziliwasaidia. Jambo la kwanza lilikuwa lile agizo ambalo Yesu alimpa mtume Petro wakati Petro alipotumia upanga kujikinga: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Na la pili lilikuwa yale maneno ya Yesu kwa Pilato wakati alipomwuliza Yesu kuhusu ufalme wake: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangalipigana ili nisikabidhiwe kwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.”—Yohana 18:36.

Wakristo wa karne ya kwanza walitumiaje kanuni hizo? Walijitenga kabisa na ulimwengu, wakidumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa na wa kijeshi. (Yohana 15:17-19; 17:14-16; Yakobo 4:4) Walikataa kutumia silaha dhidi ya wanadamu wenzao. Historia inaonyesha wazi kwamba Wakristo wa karne ya kwanza hawakujiunga na harakati za Kiyahudi za uzalendo wala majeshi ya milki ya Roma. Zaidi ya hayo, hawakujaribu kuwaambia viongozi wa kisiasa mambo waliyopaswa kufanya, kwani hilo lilikuwa daraka la viongozi hao wa serikali.—Wagalatia 6:5.

Katika karne ya pili W.K., Justin Martyr aliandika kwamba Wakristo walikuwa ‘wamefua panga zao ziwe majembe.’ (Mika 4:3) Akiwajibu wale waliopinga msimamo wa Wakristo, Tertullian aliuliza hivi: “Je, inapaswa kuonwa kuwa halali kuwa mwanajeshi, ilhali Bwana anatangaza kwamba yule anayetumia upanga ataangamia kwa upanga?”

‘Mtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu’

Wakristo wa mapema walikabili magumu walipokataa kwenda vitani. Jambo hilo halikupatana na maoni yaliyokubaliwa na watu wa wakati huo. Celsus, adui mmoja wa Ukristo, alidhihaki msimamo wao. Alionelea kwamba watu wote walipaswa kwenda vitani walipoamriwa na wenye mamlaka. Licha ya ukatili mwingi, Wakristo wa mapema walikataa kufuata falsafa zozote za wanadamu ambazo zilipinga mafundisho ya Kristo. Walisema hivi: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 4:19; 5:29.

Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa wamefuata mfano wao. Kwa mfano, katika Ujerumani ya Nazi walikataa katakata kujihusisha katika vita za Hitler zenye mauaji mengi. Walikuwa tayari kuvumilia mnyanyaso mkali, hata kufa ikiwa lazima, badala ya kubadili msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Inaripotiwa kwamba “nusu ya idadi yao walifungwa gerezani na robo moja ya idadi yao waliuawa” na Wanazi kwa sababu ya kutii kanuni za Biblia. (Kitabu Of Gods and Men) Hivyo, kati ya makumi ya mamilioni ya watu waliokufa katika Vita ya Pili ya Ulimwengu, hakuna hata mmoja aliyeuawa na Shahidi wa Yehova. Badala ya kuwaua wengine, Mashahidi walikuwa tayari kufa, na wengi wao waliuawa kwa sababu hiyo.

Somo Tunaloweza Kujifunza

Ni masomo gani tunayoweza kujifunza kutokana na mambo yaliyopita? Hapana shaka, somo moja tunalojifunza ni hili: Falsafa za wanadamu zimeendelea kusababisha chuki na mauaji kati ya mataifa na makabila. Andiko la Mhubiri 8:9 linasema hivi kwa kufaa: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Chapa ya 1989) Na sababu ya jambo hilo inaonyeshwa kwenye Yeremia 10:23, ambapo Neno la Mungu linasema hivi: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Naam, Mungu hakuwaumba wanadamu wasimamie shughuli zao wenyewe kwa mafanikio, bila kumtegemea. Hawakupewa uwezo huo. Historia yote imethibitisha hilo.

Kwa hiyo, tukiwa watu mmoja-mmoja hatuwezi kubadili mambo ambayo viongozi wa mataifa hufanya wanaposababisha tena misiba ya zamani, wala hatujaruhusiwa kujaribu kuwashawishi kufanya mambo kwa njia fulani. Lakini si lazima tushawishiwe kuhusika na kushiriki katika mapambano yao. Yesu alisema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14) Ili kuepuka kushiriki katika mapambano ya ulimwengu huu, ni sharti tukubali Neno la Mungu, Biblia, liongoze maisha yetu wala si falsafa za wanadamu zenye kubadilika-badilika.—Mathayo 7:24-27; 2 Timotheo 3:16, 17.

Wakati Ujao Mzuri Ajabu

Neno la Mungu lenye kutegemeka halitufahamishi tu kuhusu mambo yaliyopita na yanayotukia sasa. Linatupa mwongozo hakika kuhusu wakati ujao. (Zaburi 119:105; Isaya 46:9-11) Pia, linatuonyesha waziwazi kusudi la Mungu kwa ajili ya sayari hii. Hatawaruhusu wanadamu kuharibu dunia kwa kutumia vibaya uwezo mwingi sana ambao wamepata kutokana na sayansi na tekinolojia. Atahakikisha kwamba dunia itakuwa Paradiso kama alivyokusudia awali.—Luka 23:43.

Kwa habari hiyo, Neno la Mungu linasema hivi: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” (Mithali 2:21, 22) Hilo litatukia hivi punde kwa kuwa hizi siku zenye msukosuko zinaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Na kwa hakika, hizi siku za mwisho zimehesabiwa; zinakaribia kwisha. Unabii wa Biblia hutufundisha hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17; Danieli 2:44.

Karibuni Mungu ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia’ na ataondoa ulimwengu huu wa sasa wenye jeuri na kuleta ulimwengu mpya ambamo “uadilifu utakaa.” (Ufunuo 11:18; 2 Petro 3:10-13) Kisha, kwa habari ya wale watakaobaki, “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” (Ufunuo 21:1-4) Vita na jeuri hazitakuwapo tena kamwe, kwani unabii ulio kwenye Isaya 2:4 utatimizwa kikamili: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Wewe pia unaweza kufurahia wakati ujao mzuri ajabu wa milele ukijifunza kutokana na yaliyopita.—Yohana 17:3.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Mashahidi wa Yehova wamejifunza kutokana na Wakristo wa karne ya kwanza

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yesu alisema kwamba Ufalme wake si sehemu ya ulimwengu huu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Neno la Mungu linaahidi uhai udumuo milele katika hali kamilifu katika dunia paradiso