Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kuchagua Video za Muziki Zinazofaa?

Ninawezaje Kuchagua Video za Muziki Zinazofaa?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kuchagua Video za Muziki Zinazofaa?

“Ninapoona jina la kikundi au wimbo wenye kutilika shaka, ndipo ninapobadili kituo cha televisheni.”—Casey.

VIJANA wengi hufurahia sana video za muziki. Lakini kama makala iliyotangulia katika mfululizo huu inavyosema, video nyingi za muziki huonyesha picha chafu sana za ngono na jeuri. * Bila shaka, Mkristo anapaswa kuepuka kitumbuizo chochote ambacho kinachochea mambo ambayo Mungu amekataza. Hata hivyo, si video zote za muziki zinazoonyesha mambo machafu waziwazi. Huenda nyingine zikawa nzuri kiasi fulani. Na huenda nyingine zisionekane kuwa na ubaya wowote. Hata hivyo, kwa werevu zinaonyesha mambo yanayopingana na Neno la Mungu.

Wazazi wako wakikuruhusu utazame video za muziki, utahitaji kuteua zinazofaa. Kwa hiyo utahitaji kutumia ‘nguvu zako za ufahamu’ zilizozoezwa na Biblia ili uweze kutofautisha video zinazofaa na zisizofaa. (Waebrania 5:14) Ni kanuni zipi za Biblia zinazoweza kukusaidia kufanya hivyo? Yafuatayo ni maandiko ya Biblia na maelezo yanayoweza kukusaidia.

Mithali 4:23: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” Je una kifaa cha kuchezea au ala ya muziki unayothamini sana? Bila shaka wewe hujitahidi sana kuitunza na kuiweka mahali panapofaa. Kwa kweli huwezi kuiacha tu barabarani, hata kwa muda mfupi, kwa kuwa inaweza kuharibiwa au kuibiwa. Naam, unailinda. Vivyo hivyo, ni lazima uazimie kuulinda moyo wako. Hupaswi kuuhatarisha hata kwa muda mfupi kwa kutazama vitumbuizo visivyofaa.

Waefeso 2:1, 2: “Ni nyinyi Mungu aliowafanya kuwa hai ingawa mlikuwa wafu katika makosa na dhambi zenu, ambazo katika hizo wakati fulani nyinyi mlitembea kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” Hewa hiyo ni roho ya ulimwengu, njia ya kufikiri na mitazamo ambayo huchochea mwenendo usio wa kimungu. Roho hiyo inaonekana kupitia video nyingi za muziki na inapingana kabisa na roho ya Mungu, ambayo hutokeza sifa kama shangwe, amani, na kujidhibiti.—Wagalatia 5:22, 23.

2 Timotheo 2:22: “Kimbia tamaa zenye kutukia ujanani.” Kutazama picha zinazoonyesha ngono—hata kwa muda mfupi—kutazidisha tamaa. Vijana wengi hukiri kwamba picha hizo hubaki akilini; huenda hata wakazikumbuka tena na tena. Kijana mmoja anayeitwa Dave, ambaye alitazama video chafu, anakiri hivi: “Tangu wakati huo, kila mara niliposikia wimbo huo nilifikiri kuhusu video hiyo.” Kutazama video kama hizo kunaweza kumfanya mtu atamani kufanya uasherati.—1 Wakorintho 6:18; Wakolosai 3:5.

Mithali 13:20: “Rafiki ya wapumbavu ataumia.” Jiulize, ‘Je, ninaweza kuwaalika watu wajeuri, wanaowasiliana na roho waovu, walevi, au waasherati nyumbani mwangu?’ Kushirikiana na watu kama hao kupitia televisheni ni sawa na kuwaalika nyumbani mwako. Je, ‘hutaumia’ kwa kufanya hivyo? Kimberly anaeleza hivi: “Nimewahi kuwaona wasichana kwenye karamu wakiiga mavazi au mitindo michafu ya kucheza dansi waliyotazama kwenye video.” Labda umeona hivyo pia. Kwa kuiga wale ambao hawaheshimu kanuni za Mungu, vijana hao huonyesha kwamba tayari wameanza ‘kuumia.’ Kwa vyovyote vile, epuka ‘mashirika yoyote mabaya.’—1 Wakorintho 15:33.

Zaburi 11:5: “BWANA humjaribu mwenye haki; bali nafsi yake humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu [“jeuri,” NW].” Tukitazama video zinazochochea jeuri, je, huenda tukaonekana kama ‘tunapenda jeuri’ kwa njia fulani?

Ugumu wa Kuchagua Video

Kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu,” imekuwa vigumu sana kupata vitumbuizo visivyo na mawazo na mitazamo ya ulimwengu. (1 Yohana 5:19) Vituo fulani vya muziki huenda vikaonyesha vipindi vingi visivyofaa. Hata kama kipindi fulani hakionyeshi mambo machafu au jeuri waziwazi, mara nyingi bado huchochea roho ya ulimwengu. Mwanamuziki mmoja mashuhuri alisema kwamba kituo kimoja maarufu cha muziki “kimekuwa kituo cha ‘mtindo wa maisha’ badala ya kituo cha muziki.”

Huenda suluhisho likaonekana kuwa rahisi: Kama video ni chafu, badili kituo. Tatizo ni kwamba, huenda ukahitaji kuwa chonjo unapotazama vituo vingine vya televisheni. Vituo vingi huonyesha vipindi vyenye jeuri na uasherati wa waziwazi au huonyesha watu wanaotenda mambo ya aibu. Ama kwa hakika, ni jambo lenye kuudhi—labda hata lenye kusumbua—kujaribu kufurahia kitumbuizo fulani huku ukiwa chonjo kubadili kituo. Na nyakati nyingine, mtu huwa ameathiriwa tayari kabla ya kubadili kituo. Tayari picha chafu huwa zimehifadhiwa akilini. Hata hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu atakuthawabisha kwa jitihada zozote unazofanya ili kuulinda moyo wako.—2 Samweli 22:21.

Kuna hatua nyinginezo zinazoweza kukusaidia. Casey, aliyetajwa mwanzoni, alieleza jambo linalomsaidia: “Kwa kawaida jina la bendi na kichwa cha wimbo huonyeshwa mwanzoni mwa video. Kila bendi ina sifa yake, kwa hiyo mara nyingi utajua ni vikundi na nyimbo gani ambazo huenda si nzuri. Kwa hiyo ninapoona jina la kikundi au wimbo wenye kutilika shaka, ndipo ninapobadili kituo cha televisheni mara moja.”

‘Kusema Kweli kwa Moyo Wako’

Hata kama unajua kanuni za Biblia, unaweza kuanza kukubali mambo machafu. Jinsi gani? Kwa kutoa udhuru. (Yakobo 1:22) Biblia hutuambia kwamba rafiki ya Yehova ni yule “asemaye kweli kwa moyo wake.” (Zaburi 15:2) Basi, jichunguze kwa unyofu. Usijidanganye. Ukigundua kwamba una zoea la kutoa udhuru ili utazame kipindi kinachotilika shaka, jiulize, ‘Je, kweli Yehova atafurahi kuniona nikikitazama?’ Kumbuka kwamba, mara nyingi tatizo si kujua jambo lililo sawa au lisilo sawa, bali ni kuazimia kufanya lililo sawa! Ni lazima uuone uhusiano wako pamoja na Yehova kuwa wenye thamani zaidi kuliko kitumbuizo chochote.—2 Wakorintho 6:17, 18.

Kwa kawaida haitoshi kuazimia kwa moyo nusu-nusu kutotazama video zisizofaa. Azimio lako linaweza kudhoofika haraka usipokuwa imara. Biblia hutuambia jinsi mwanamume mcha-Mungu aliyeitwa Ayubu alivyoazimia kubaki mwaminifu kwa mke wake. Alisema hivi: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana?” (Ayubu 31:1) Hebu wazia hilo! Ayubu alifanya agano, au mkataba thabiti, na nafsi yake kuwa mwangalifu kuhusu yale aliyotazama. Unaweza kufanya vivyo hivyo. Azimia kwa uthabiti—jiwekee ahadi—kutotazama mambo mabaya. Weka mipaka hususa. Sali kuhusu jambo hilo. Kisha uwe mwaminifu kwa ahadi yako, unaweza hata kuiandika kama kufanya hivyo kutasaidia. Ukihitaji msaada wa ziada, kwa nini usiongee na mtu mwenye umri mkubwa zaidi unayemtumaini, kama wazazi wako?

Baadhi ya vijana Wakristo wameamua kutotazama kabisa video za muziki ili kuepuka hatari. Hata uamuzi wako uwe nini, tumia nguvu zako za ufahamu. Dumisha dhamiri safi. Ukitazama tu vitumbuizo vinavyofaa unaweza kuepuka kujiumiza na unaweza kudumisha urafiki wako na Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Inafaa Nitazame Video za Muziki?” katika toleo letu la Februari 22, 2003.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ingawa video fulani hazionyeshi ukosefu wa adili waziwazi bado zinachochea mawazo mabaya

[Picha katika ukurasa wa 13]

Azimia kutotazama kitumbuizo chochote kisichompendeza Mungu