Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Mahitaji Yangu ya Kiroho Yalivyotoshelezwa

Jinsi Mahitaji Yangu ya Kiroho Yalivyotoshelezwa

Jinsi Mahitaji Yangu ya Kiroho Yalivyotoshelezwa

SIMULIZI LA LUCIA MOUSSANETT

ENEO la Valle d’Aosta liko katikati ya milima iliyoko kwenye pembe ya kaskazini-magharibi mwa Italia, karibu na Milima ya Alps ya Uswisi na karibu na mlima maarufu nchini Ufaransa unaoitwa Mont Blanc. Nilizaliwa katika eneo hilo mnamo mwaka wa 1941 katika kijiji cha Challant St. Anselme.

Nilikuwa na ndugu wanne na nilikuwa mkubwa wao. Mama alifanya kazi kwa bidii na alikuwa Mkatoliki mwenye juhudi nyingi. Baba naye alizaliwa katika familia iliyopenda dini. Dada zake wawili walikuwa watawa wa kike. Wazazi wangu walijinyima mambo mengi kwa ajili yangu, hata walinielimisha. Kwa kuwa hakukuwa na shule katika kijiji chetu, nilipokuwa na umri wa miaka 11, walinipeleka katika shule ya bweni iliyosimamiwa na watawa wa kike.

Huko nilijifunza Kilatini na Kifaransa, na masomo mengine. Kisha, nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilianza kufikiri sana kuhusu kumtumikia Mungu. Niliona njia bora ya kufanya hivyo ingekuwa kujiunga na makao ya watawa. Mama hakuunga jambo hilo mkono kwa kuwa ingembidi awatunze ndugu zangu akiwa peke yake. Wazazi wangu walitazamia kwamba elimu yangu ingenisaidia kupata kazi nzuri ambayo ingefaidi familia yetu kifedha.

Ingawa nilifadhaishwa na itikio la wazazi wangu, nilitaka kuwa na kusudi halisi maishani, na niliona kwamba nilipaswa kumtanguliza Mungu. Hivyo, mnamo mwaka wa 1961, nilijiunga na makao ya watawa wa kike ya Kanisa Katoliki.

Maisha Yangu Nikiwa Mtawa wa Kike

Miezi ya kwanza-kwanza, nilijifunza sheria na kanuni za kanisa na nikafanya kazi za mikono katika makao ya watawa. Mnamo Agosti 1961, nilianza kufundishwa kazi ya watawa, na nikaanza kuvalia mavazi ya watawa. Pia nilitaka niitwe jina jipya, Ines, ambalo lilikuwa jina la mama yangu. Jina hilo lilipokubaliwa, nilianza kuitwa Sista Ines.

Ingawa wote waliokuwa wakifundishwa walifanya kazi katika makao hayo ya watawa, nilifanya kazi ya ualimu katika shule ya msingi kwa sababu nilikuwa na elimu. Miaka miwili baadaye, mnamo Agosti 1963, nilianza rasmi maisha ya utawa katika makao ya watawa ya Sista wa San Giuseppe huko Aosta, Italia. Baadaye, makao hayo yalinipeleka katika Chuo Kikuu cha Maria Santissima Assunta huko Roma ili nipate elimu zaidi.

Niliporudi Aosta mnamo mwaka wa 1967 baada ya kumaliza masomo yangu huko Roma, nilianza kufundisha katika shule ya upili. Mnamo mwaka wa 1976, nilipata cheo cha msimamizi wa shule hiyo. Ingawa nilifunza masomo kadhaa, kazi yangu hasa ilikuwa ya usimamizi wa shule na nikawa mwanachama wa kamati ya shule ya eneo la Valle, d’Aosta.

Nilitamani sana kuwasaidia maskini. Niliwahurumia sana. Hivyo, nilianzisha miradi ya kuwasaidia, kama vile kuwasaidia watu waliougua magonjwa yasiyokuwa na tiba ambao hawakuwa na watu wa ukoo. Pia nilianzisha miradi ya kuwafundisha watoto wa wageni. Isitoshe, niliwatafutia maskini kazi na makao, na kuwalipia gharama za matibabu wale waliokuwa na uhitaji. Nilijitahidi kutii sheria za kanisa.

Wakati huo, niliamini mafundisho ya Kanisa Katoliki, kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi, na imani kuhusu tumaini la wakati ujao wa milele. Vilevile, kanisa liliwaruhusu watu wawe na imani mbalimbali, kama vile kukubali imani za dini nyingine na kushirikiana nazo.

Mambo Yaliyoanza Kunikera

Hata hivyo, mambo fulani katika Kanisa Katoliki yalinikera. Kwa mfano, kabla ya kubatizwa na kupewa kipaimara, wazazi na watoto wao walipaswa kujifunza maana ya mambo hayo. Lakini watu wengi hawakuhudhuria masomo, na wengine hawakujifunza hata kidogo. Isitoshe, wale ambao hawakuruhusiwa kubatizwa na kupewa kipaimara katika kanisa la eneo moja walienda kwenye kanisa la eneo jingine ili wabatizwe na kupewa kipaimara huko. Niliona hilo likiwa jambo lisilofaa na la unafiki.

Wakati mwingine niliwaza na kuwauliza watawa wenzangu wa kike, “Je, tusingepaswa kuhubiri Injili badala ya kufanya mambo mengine kwa bidii?” Walinijibu hivi: “Tunahubiri kwa matendo yetu mazuri.”

Isitoshe, ilikuwa vigumu kwangu kuamini kwamba nilipaswa kumwendea kasisi ili nitubu dhambi zangu. Nilidhani ningeweza kuzungumza na Mungu kuhusu mambo hayo ya kibinafsi. Pia niliona kwamba haifai kukumbuka sala na kuzikariri, na sikuamini kwamba papa hawezi kukosea. Baadaye, niliwaza kwamba ningeendelea tu kushikilia imani yangu kuhusu mambo hayo na bado niendelee na shughuli zangu za kanisa.

Tamaa ya Kujifunza Biblia

Sikuzote niliiheshimu Biblia sana na nilitaka kuifahamu. Wakati wowote nilipohitaji kuamua jambo fulani au nilipotaka mwongozo wa Mungu, nilisoma Biblia. Ingawa hatukuisoma Biblia katika makao ya watawa, niliisoma peke yangu. Sikuzote nilipendezwa na andiko la Isaya 43:10-12, ambapo Yehova Mungu alisema hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu.” Lakini wakati huo sikuelewa maana kamili ya maneno hayo.

Nilipokuwa katika chuo kikuu huko Roma katikati ya miaka ya 1960, nilijifunza somo la dini kwa miaka minne lililokuwa limedhaminiwa na Vatikani. Lakini Biblia haikuwa mojawapo ya vitabu vya mafundisho. Hata niliporudi Aosta, nilihudhuria makongamano mengi ya dini mbalimbali, hata yale yaliyokuwa yamedhaminiwa na makanisa mbalimbali na mashirika yasiyo ya Kikatoliki. Hiyo ilinifanya niwe na kiu zaidi ya kufahamu mafundisho ya Biblia. Kulikuwa na mvurugo mwingi sana katika makundi yaliyodai kwamba yanafundisha Biblia!

Kujua Mengi Kuhusu Biblia

Mnamo mwaka wa 1982, Shahidi mmoja wa Yehova alifika kwenye kituo ambako nilifanya kazi ya kutoa huduma za jamii na akajaribu kuzungumza nami kuhusu Biblia. Ingawa sikuwa na nafasi, nilitaka kujifunza Biblia. Hivyo nilimwambia, “Tafadhali njoo shuleni mwetu, na nikiwa na wakati, tutazungumza.”

Ingawa mwanamke huyo alinitembelea, sikupata “wakati.” Kisha mama yangu akafahamu kwamba anaugua kansa, hivyo nilichukua likizo ili nimsaidie. Alipokufa mnamo Aprili 1983, nilirudi kazini, lakini Mashahidi hawakujua nilikoenda. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, Shahidi mwingine mwenye umri wa miaka 20 na kitu, alikuja kuzungumza nami kuhusu Biblia. Nilikuwa ninasoma kitabu cha Ufunuo. Hivyo nilimwuliza, “Watu 144,000 wanaotajwa hapa katika Ufunuo sura ya 14 ni akina nani?”

Nilikuwa nimefundishwa kwamba watu wote wema wataenda mbinguni, hivyo sikuona ni kwa nini hao 144,000 walikuwa wanatenganishwa na wengine mbinguni. Niliwaza kuhusu watu hao. ‘Watakuwa na kazi gani?’ Niliendelea kuwaza kuhusu mambo hayo. Shahidi huyo aliendelea kunitafuta, lakini hakufaulu kwani sikupatikana nyumbani mara nyingi.

Hatimaye, Shahidi huyo alimpa Marco, mzee katika kutaniko lake, anwani yangu. Mwishowe, mnamo Februari 1985, mzee huyo alinipata. Tulizungumza kwa dakika chache kwa kuwa nilikuwa na shughuli, lakini tulipanga kukutana baadaye. Baadaye, yeye na mkewe, Lina, walinitembelea kwa ukawaida, na wakanisaidia kuelewa Biblia. Kwa muda mfupi, niligundua kwamba mafundisho ya msingi ya Katoliki kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi, na moto wa mateso hayaungwi mkono na Biblia hata kidogo.

Kushirikiana na Mashahidi

Nilipohudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova katika Jumba la Ufalme, niliona wazi kwamba mambo yalikuwa tofauti kabisa na Kanisa Katoliki. Kila mtu aliimba, bali si kwaya yenye watu wachache tu. Kisha walishiriki kutoa maelezo katika mkutano. Halafu nikatambua kwamba tengenezo lote lilikuwa na “akina ndugu” na “akina dada.” Wote walipendana. Mambo hayo yalinipendeza.

Wakati huo nilihudhuria mikutano nikiwa nimevalia mavazi ya watawa. Wengine walipendezwa kuona mtawa wa kike akiwa kwenye Jumba la Ufalme. Nilifurahi na kuridhika kuwa sehemu ya familia kubwa yenye upendo. Pia, kadiri nilivyoendelea kujifunza, nilitambua kwamba kanuni nyingi ambazo nilikuwa ninaamini hazikuungwa mkono na Neno la Mungu. Kwa mfano, Biblia haifundishi kwamba watumishi wa Mungu wanapaswa kuvalia mavazi ya pekee. Vyeo vya kanisa na desturi mbalimbali za kanisa zilikiuka mafundisho ya Biblia kuhusu wazee wanyenyekevu wanaoongoza kutanikoni.

Nilihisi kana kwamba nilikuwa nikizama. Sikuamini nilikuwa nimeamini mafundisho yenye kosa kwa muda wa miaka 24. Hata hivyo, nilijua nilikuwa nimepata kweli ya Biblia. Nilishikwa na wasiwasi nilipotambua kwamba nikiwa na umri wa miaka 44 nilihitaji kubadili maisha yangu upya. Hata hivyo, singeendelea kutembea nikiwa nimefunga macho huku nikiwa nimetambua kweli ya Biblia.

Uamuzi Muhimu

Nilitambua kwamba ikiwa ningeondoka kwenye makao ya watawa, ningepoteza mali zangu zote. Hata hivyo, nilikumbuka maneno ya Daudi yanayosema kwamba hakumwona mwenye haki “ameachwa wala mzao wake akiomba chakula.” (Zaburi 37:25) Nilijua ningepoteza mali za kimwili, lakini nilimtumaini Mungu na kusema, ‘Kwa nini niogope?’

Watu wetu wa ukoo walifikiri nilikuwa na kichaa. Ingawa jambo hilo lilinihangaisha, nilikumbuka maneno ya Yesu yanayosema: ‘Anayempenda baba au mama kuliko mimi hanistahili.’ (Mathayo 10:37) Wakati huohuo upendo nilioonyeshwa na Mashahidi ulinitia moyo na kuniimarisha. Nilipotembea barabarani nikiwa na mavazi ya watawa, walinijia na kunisalimu. Hilo lilinifanya niwe karibu zaidi na akina ndugu na nijihisi nikiwa sehemu ya udugu huo.

Mwishowe nilimwendea msimamizi wa makao ya watawa na nikamwambia sababu iliyonifanya nitake kuondoka katika makao hayo. Ingawa nilitaka kutumia Biblia kumwelezea sababu ya kufanya uamuzi huo, alikataa kunisikiliza, akisema: “Nikitaka kuelewa jambo lolote katika Biblia, ninaweza kumuuliza mtaalamu wa Biblia!”

Kanisa Katoliki halikupenda uamuzi niliofanya. Walisema kwamba mimi ni mtovu wa maadili na kwamba nimerukwa na akili. Lakini wale walionijua walifahamu kwamba huo ulikuwa uwongo. Watu niliofanya kazi pamoja nao walikuwa na maoni tofauti-tofauti. Wengine waliniona kuwa mtu jasiri kwa kufanya uamuzi huo. Wengine walikasirika, wakadhani nilifanya uamuzi mbaya. Wengine hata walinihurumia.

Mnamo Julai 4, 1985, nilijiuzulu kutoka Kanisa Katoliki. Mashahidi walijua mambo yaliyowapata wengine waliochukua hatua hiyo, hivyo walinificha kwa mwezi mmoja hivi wakihofia usalama wangu. Walinichukua kutoka mahali nilipoishi na kunipeleka kwa gari hadi mikutanoni na kunirudisha. Niliepuka kujitokeza hadharani hadi hali ilipokuwa shwari. Halafu, mnamo Agosti 1, 1985, nilianza kuhubiri pamoja na Mashahidi wa Yehova.

Nilipohudhuria Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova baadaye mwezi huo, vyombo vya habari viligundua kwamba nilijiuzulu kutoka kanisani na vikatangaza jambo hilo. Hatimaye nilipobatizwa mnamo Desemba 14, 1985, kituo kimoja cha televisheni na gazeti moja liliona kwamba kuondoka kanisani kulikuwa jambo baya sana hivi kwamba walitangaza jambo hilo tena. Walihakikisha kwamba kila mtu amesikia yale niliyofanya.

Nilipotoka kwenye makao ya watawa, sikuwa na kitu chochote. Sikuwa na kazi, nyumba, wala marupurupu yoyote. Kwa hiyo, kwa mwaka mmoja, nilimtunza mtu mmoja aliyepooza. Mnamo Julai 1986, nilianza utumishi wa wakati wote, ambao Mashahidi wa Yehova huuita upainia. Nilihamia eneo lenye kutaniko dogo, ambalo lilikuwa limeanzishwa karibuni. Nikiwa huko nilifundisha lugha na masomo mengine, hivyo nikatumia elimu yangu kujiruzuku. Kwa hiyo, ningeweza kubadili ratiba yangu kulingana na hali.

Kutumikia Katika Nchi Nyingine

Kwa kuwa sasa nilikuwa nimejifunza kweli ya Biblia, nilitaka kuitangaza kwa watu wengi inavyowezekana. Nilijua Kifaransa, hivyo nilifikiri ningetumika katika nchi moja ya Afrika ambapo Kifaransa huzungumzwa. Lakini mnamo mwaka wa 1992, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria katika nchi jirani ya Albania. Mwishoni mwa mwaka huo, kikundi kidogo cha mapainia kutoka Italia kilitumwa huko. Mario na Cristina Fazio wa kutaniko letu walikuwa miongoni mwao. Walinikaribisha kwao na wakanitia moyo nifikirie kutumikia nchini Albania. Hivyo baada ya kufikiria sana na kusali kuhusu jambo hilo, nikiwa na umri wa miaka 52, niliacha hali nzuri ya kifedha niliyokuwa nayo na nikahamia eneo tofauti kabisa.

Hiyo ilikuwa Machi 1993. Mara tu nilipowasili, nilitambua kwamba ingawa nchi hiyo haiko mbali sana na nchi niliyozaliwa, ilikuwa tofauti sana. Watu walitembea mahali popote walipotaka, na walizungumza Kialbania, lugha ambayo sikuielewa hata kidogo. Nchi hiyo ilikuwa katika kipindi cha mpito, kutoka utawala mmoja hadi mwingine. Hata hivyo, watu walikuwa na njaa ya kweli ya Biblia na walipenda kusoma na kujifunza. Wanafunzi wa Biblia walifanya maendeleo haraka, na jambo hilo lilinipendeza na kunisaidia nizoee mazingira hayo mapya.

Nilipowasili jiji kuu la Tiranë mnamo mwaka wa 1993, kulikuwa na kutaniko moja tu nchini Albania na Mashahidi waliozidi kidogo 100 walikuwa wametawanyika nchini kote. Mwezi huohuo, katika kusanyiko la kwanza la pekee lililofanywa Tiranë, watu 585 walihudhuria na 42 wakabatizwa. Ingawa sikuelewa chochote, nilisisimuka kuwasikia Mashahidi wakiimba na kuwaona wakisikiliza kwa makini. Mnamo Aprili, katika Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo, watu 1,318 walihudhuria! Tangu wakati huo, kazi ya Kikristo imeendelea kukua nchini Albania.

Nilikuwa nikitazama jiji la Tiranë kutoka roshani ya nyumba yangu katika orofa ya nne na kujiuliza, ‘Tutawezaje kuwahubiria watu wote hawa?’ Yehova Mungu alishughulikia jambo hilo. Leo kuna makutaniko 23 ya Mashahidi wa Yehova jijini Tiranë. Kuna makutaniko 68 na vikundi 22, na jumla ya Mashahidi 2,846 nchini kote. Huo ulikuwa ukuzi wa haraka kwa muda mfupi sana! Mnamo mwaka wa 2002, watu 12,795 walihudhuria Ukumbusho!

Katika kipindi cha miaka kumi ambacho nimekuwa nchini Albania, nimepata pendeleo la kuwasaidia angalau watu 40 kufikia ubatizo. Wengine ni mapainia au wako katika namna nyingine ya utumishi wa wakati wote. Kadiri miaka ilivyopita, vikundi sita vya mapainia kutoka Italia vilitumwa nchini Albania. Kila kikundi kilifundishwa lugha kwa miezi mitatu. Karibuni nimeombwa nisaidie kufundisha vikundi vinne.

Nilipoamua kuondoka katika makao ya watawa, marafiki zangu walikuwa na maoni mabaya sana. Hata hivyo, baada ya miaka hiyo yote, wamebadili mtazamo wao, kwani wametambua kwamba nina amani na utulivu. Familia yetu, kutia ndani shangazi yangu mwenye umri wa miaka 93 ambaye bado ni mtawa wa kike, wanashirikiana nami.

Yehova amenitegemeza katika hali mbalimbali tangu nilipomjua! Alinielekeza kwenye tengenezo lake. Ninapotafakari kuhusu maisha yangu, ninakumbuka wakati nilipotaka kuwasaidia maskini na wenye uhitaji, na jinsi nilivyotamani kumtumikia Mungu kwa moyo wote. Ndiyo sababu namshukuru Yehova, kwani amehakikisha kwamba mahitaji yangu ya kiroho yametoshelezwa.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Familia ya Kialbania ambayo niliifundisha Biblia. Watu 11 wamebatizwa katika familia hii

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wengi kati ya wanawake hawa ambao nilifundisha Biblia huku Albania wako katika utumishi wa wakati wote