Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Watu Wanazidi Kuchukia Kodi?

Je, Watu Wanazidi Kuchukia Kodi?

Je, Watu Wanazidi Kuchukia Kodi?

“Ninapochuma kwa jasho, mimi hupokonywa.”—Methali ya Babiloni, karibu mwaka wa 2300 K.W.K.

“Katika ulimwengu huu, hakuna kitu kilicho hakika kama kifo na kodi.”Mwanasiasa Mmarekani, Benjamin Franklin, mwaka wa 1789.

REUBEN ni afisa wa mauzo. Kila mwaka karibu thuluthi moja ya mshahara wake ambao ameutolea jasho huishia katika kodi. Analalamika hivi: “Sijui pesa hizo huenda wapi. Kwa kuwa serikali imepunguza matumizi yake, sasa tunapata huduma chache kuliko wakati mwingine wowote.”

Hata hivyo, tupende tusipende, kodi ni sehemu ya maisha. Mwandishi Charles Adams anasema: “Serikali zimetoza kodi ya mapato kwa njia nyingi tangu jamii ilipostaarabika.” Kodi zimewachukiza watu mara nyingi na nyakati nyingine zimechochea uasi. Waingereza wa kale walipigana na Waroma, wakisema hivi: “Ni afadhali tuuawe kuliko kulemezwa na kodi!” Nchini Ufaransa, watu walichukizwa na kodi ya chumvi na hilo likasababisha Mapinduzi ya Ufaransa, ambapo watoza-kodi waliuawa. Pia, vita vya uhuru vya Marekani dhidi ya Uingereza vilisababishwa kwa kadiri fulani na kodi.

Haishangazi kwamba watu wanachukia kodi hata leo. Wataalamu wanasema kwamba katika nchi zinazoendelea, mara nyingi sheria za kodi “hazifanyi kazi vizuri” na “zinakandamiza.” Kulingana na mtafiti mmoja, nchi moja maskini ya Afrika ilikuwa na “zaidi ya kodi 300, na ilikuwa vigumu kutoza kodi hizo hata kukiwa na wafanyakazi stadi. Huenda hakuna mfumo bora wa kukusanya kodi na kuhakikisha inatumiwa vizuri ama mfumo huo hautumiwi ipasavyo, . . . na hivyo pesa zinatumiwa vibaya.” Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) liliripoti kwamba katika nchi moja ya Asia “maafisa wa serikali walitoza . . . kodi nyingi zisizo halali kwa wakulima wa ndizi na hata kwa kuchinja nguruwe ili kuongeza mapato ya serikali au kuingiza pesa mifukoni mwao.”

Tofauti kati ya matajiri na maskini huwafanya wengi wachukie kodi. Gazeti Africa Recovery la Umoja wa Mataifa linasema: “Mojawapo ya tofauti nyingi za kiuchumi kati ya nchi zilizoendelea na zinazoendelea ni kwamba nchi zilizoendelea huwapa wakulima msaada wa kifedha hali zile zinazoendelea huwatoza wakulima kodi. . . . Uchunguzi uliofanywa na Benki ya Dunia unadokeza kwamba misaada ya kifedha inayotolewa kwa wakulima wa Marekani pekee hupunguza mapato ambayo Afrika Magharibi hupata kila mwaka kwa kuuza pamba kwa dola [milioni] 250.” Kwa hiyo, huenda wakulima katika nchi zinazoendelea wakaudhika wakati serikali zinapowatoza kodi na kupunguza mapato yao madogo sana. Mkulima mmoja huko Asia anasema: “Kila mara tulipowaona [maafisa wa serikali] hapa tulijua kwamba wanatafuta pesa.”

Hivi majuzi pia, watu waliudhika nchini Afrika Kusini wakati serikali ilipoanza kuwatoza wakulima kodi ya shamba. Wakulima walitisha kwenda mahakamani. Msemaji wa wakulima hao alisema kwamba kodi hiyo “itawafilisisha wakulima na wafanyakazi wengi zaidi wa mashambani watakosa kazi.” Hata leo, jeuri hutokea nyakati nyingine kwa sababu ya kuchukia kodi. Shirika la BBC linasema: “Wakulima wawili [Waasia] waliuawa mwaka uliopita wakati polisi walipovuruga maandamano katika kijiji kimoja ambako wakulima walipinga kodi za juu.”

Lakini, si maskini tu wanaochukia kodi. Uchunguzi uliofanywa nchini Afrika Kusini ulionyesha kwamba matajiri wengi wanaolipa kodi “hawataki kulipa kodi zaidi hata kama jambo hilo litasababisha serikali ishindwe kuboresha huduma zinazowafaidi.” Imeripotiwa kwamba mabingwa wa muziki, sinema, michezo, na wanasiasa mashuhuri wamehepa kodi. Kitabu The Decline (and Fall?) of the Income Tax kinasema: “Inasikitisha kwamba hata maafisa wakuu serikalini, marais, hawajawawekea raia mfano mzuri wa kulipa kodi.”

Labda unahisi kwamba kodi zenu ni za juu mno, zinakandamiza, na kulemea. Basi, unapaswa kuwa na maoni gani juu ya kulipa kodi? Je, zinatimiza kusudi lolote? Ni kwa nini mara nyingi mifumo ya kodi huwa tata sana na huonekana kuwa inakandamiza? Makala zinazofuata zitazungumzia maswali hayo.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Katika nchi zinazoendelea maskini wanaweza kulemewa na kodi

[Hisani]

Godo-Foto