Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku za Wageni Zilizofana Sana

Siku za Wageni Zilizofana Sana

Siku za Wageni Zilizofana Sana

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI MEXICO

MNAMO Machi 15, 2003, wageni kutoka zaidi ya nchi 40 walikusanyika karibu na Mexico City kuhudhuria sherehe ya kuwekwa wakfu kwa majengo mapya yanayoonyeshwa hapa chini. Majengo haya ya makazi na ya matbaa ni sehemu ya upanuzi wa hivi karibuni zaidi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico.

Mwaka wa 1974, kulipokuwa na Mashahidi 65,000 hivi nchini Mexico, majengo ya kwanza ya ofisi ya tawi katika uwanja huu yaliwekwa wakfu. Idadi ya Mashahidi nchini Mexico ilipoongezeka haraka, majengo mengine yalijengwa na kuwekwa wakfu katika mwaka wa 1985 na 1989. Majengo zaidi ya 12 yalijengwa hivi karibuni na yanatia ndani matbaa kubwa na jengo la makazi ambalo litatumiwa na wafanyakazi wapatao 1,300.

Majuma mawili baada ya sherehe ya kuwekwa wakfu, siku fulani zilitengwa ili watu wanaoishi karibu watembelee ofisi hiyo. Kati ya wale waliokaribishwa, ni maafisa wa jiji, wanafunzi, na walimu wa chuo kikuu kilichoanzishwa hivi majuzi karibu na ofisi ya tawi. Wengi katika ofisi ya tawi walitaka sana kuona ni watu wangapi wangekubali mwaliko huo.

Wengi Walikuja

Jumla ya watu 272 walikuja, kutia ndani wanafunzi, maafisa wa serikali na wa jiji. Wageni hao walieleza maoni yao kuhusu uzuri na usafi wa majengo hayo na kutoa shukrani kwa ukarimu walioonyeshwa. Mmoja wao aliandika hivi katika kitabu cha wageni: “Ni mara yangu ya kwanza kutembelea majengo yenu. Yanapendeza sana. Zamani nilivutiwa nanyi na kuwaheshimu, lakini sasa ni zaidi.”

Mgeni mwingine alisema: “Tulikuwa na maoni mabaya kuhusu mambo yanayofanywa hapa. Mambo mbalimbali yalisemwa juu yenu. . . . Lakini yale ambayo nimeona yamenisadikisha. Nitawakaribisha kwa furaha nyumbani kwangu kwa kuwa mnafanya mambo ya maana.”

Mhadhiri mmoja wa chuo kikuu ambaye mama yake ni Shahidi, alikuja na wanafunzi wa madarasa mawili. Alisema hivi: “Nilitaka vijana hawa wajue kile ambacho Mashahidi wa Yehova wanafanya ulimwenguni pote. Wanaweza kujifunza mambo fulani.” Wanafunzi walikuwa na maoni gani?

Mmoja aliandika: “Asanteni kwa ukarimu wenu. Mimi na wenzangu hatuwezi kusahau siku hii.” Mwingine alisema kwamba watu ambao hawawasikilizi Mashahidi wanapowatembelea, huwaelewa vibaya. Alikata kauli hii: “Tunapaswa kusikiliza maoni ya wengine.” Kijana mmoja alisema: “Nilikuwa na maoni tofauti kabisa, lakini sasa nimeona mnasaidiana. Mnafanya kazi kwa bidii kama chungu.”

Maafisa wanne wa polisi pia walikuja. Polisi mmoja mwanamke alisema: “Inavutia sana. Hamna ubaguzi. Anayesafisha, mtunzaji wa bustani, wote ni sawa. . . . Inapendeza sana.”

Wavulana wawili majirani wenye umri wa miaka tisa na kumi, walisema: “Majengo haya yanapendeza sana na ni makubwa sana.” “Nilifurahia hasa mashine. Zinafanya kazi haraka sana. Nilipendezwa hasa na mashine ya kukata karatasi.”

Daktari mmoja, ambaye ni mtaalamu wa majeraha, mke wake, na binti yake ambaye ni mwanafunzi wa chuo kikuu walikuja pia. Mke wa daktari huyo aliuliza maswali mengi ya Biblia walipokuwa wakitembezwa. Alisema kwamba alipendezwa na Mashahidi walipomtembelea baba yake ambaye ni mshiriki wa dini ya kiinjilisti. Baba yake aliwakasirikia Mashahidi lakini walibaki watulivu. Mwanamke huyo alisema: “Sasa ninajua sababu.”

Daktari huyo na familia yake walisema kwamba wamebadili maoni yao kuwaelekea Mashahidi baada ya ziara yao. José, aliyewatembeza, alipoona kwamba wanapendezwa, aliwaalika kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo na kuwatia moyo wajifunze Biblia. Walikubali, wakasema kwamba watakuja kwenye ofisi ya tawi kujifunza.

Juma lililofuata walikuja, na José na mkewe Beatriz waliwakaribisha kwa uchangamfu chumbani mwao. Walikuwa na maswali mengi sana hivi kwamba funzo la kwanza lilichukua saa tatu na nusu! Mnamo Aprili 16, familia hiyo ilihudhuria Ukumbusho pamoja na baba ya mwanamke huyo—yuleyule aliyekuwa akiwakasirikia Mashahidi!

Jambo lililovutia zaidi ni idadi ya vichapo vya Biblia ambavyo wageni walichukua—vichapo 500 hasa Biblia. Baadhi yao walisema kwamba hawajawahi kuwa na Biblia.

Mwanamke mmoja jirani, alimwambia Armando ambaye alikuwa akigawa vichapo: “Kuanzia leo, nitajiunga nanyi Mashahidi kwenye mikutano yenu, kwa kuwa ninajua kwamba huu ndio ukweli.” Majuma machache baadaye, Armando alifurahi kumwona mwanamke huyo katika Jumba la Ufalme. Armando anasema: “Alikuja na kitabu alichopata alipotembelea ofisi ya tawi. Nilipomsalimia, aliniambia: ‘Unaona, ninatimiza ahadi yangu.’”

Siku hizo tatu zilikwisha upesi. Lakini zilitia moyo sana. Wafanyakazi wa ofisi ya tawi walithamini zaidi pendeleo lao la kutumikia katika mojawapo ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova waliposikia maoni ya wageni waliokuja kutembelea majengo hayo mara ya kwanza.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

1. Majengo ya urekebishaji wa magari, 2. jengo la utumishi, 3. jengo la karakana, 4. jengo la makazi, 5. jengo la matbaa, 6. ukumbi, 7. jengo la wageni

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mamia ya watu walikubali kuja kutembelea ofisi ya tawi, kutia ndani wanafunzi na polisi