Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Watu Wengi Wana Deni la Usingizi?

Je, Watu Wengi Wana Deni la Usingizi?

Je, Watu Wengi Wana Deni la Usingizi?

MAMILIONI ya watu leo wana “deni” kubwa. Deni hilo linaweza kuwa ndicho kisababishi kikubwa cha kuharibu magari yao, kazi, na hata ndoa zao. Linaweza kudhuru afya na kupunguza sana maisha yao. Linachangia kudhoofika kwa mfumo wa kinga, na hivyo mtu anaweza kupata maambukizo kwa urahisi. Magonjwa kama vile kisukari, ugonjwa wa moyo, kunenepa kupita kiasi, na matatizo mengine ya afya yamesababishwa na deni hilo. Hata hivyo, watu wengi hawafahamu kwamba wana deni hilo.

Tunazungumzia deni la usingizi, ambalo hutokea wakati mtu anapokosa usingizi anaohitaji ili awe na afya bora. Deni hilo linaweza kusababishwa na kukosa kulala kimakusudi kwa sababu ya mtindo wa mtu wa maisha au kwa sababu ya ugonjwa.

Watafiti wa tiba wanakadiria kwamba watu duniani leo wamepunguza muda wao wa kulala kwa saa moja hivi kila siku kuliko inavyohitajika. Ingawa huenda jambo hilo likaonekana kuwa dogo, deni hilo la usingizi la saa bilioni sita kila siku ulimwenguni pote limechochea watu wafanye utafiti wa magonjwa mbalimbali ya usingizi na jinsi yanavyoathiri maisha.

Hapo zamani wanatiba walifikiri kwamba kuna ugonjwa mmoja tu wa usingizi, yaani, kukosa usingizi. Hata hivyo, tume moja iliyoteuliwa na Bunge la Marekani ilitambulisha magonjwa 17 ya usingizi. Kwa vyovyote vile, tatizo la kukosa usingizi husababishwa na mambo mengi hivi kwamba mara nyingi linaonwa kuwa dalili ya magonjwa mengine, kama vile homa ilivyo dalili ya ugonjwa fulani.

Hata kukosa usingizi mara mojamoja kunaweza kuwa hatari. Kwa mfano, ingawa Tom ni dereva wa lori mwenye uzoefu, aligongesha lori kubwa kwenye ukuta ulio kando ya barabara kuu na kumwaga lita 400 za asidi ya sulfuriki. Tom anakubali hivi: “Nilikuwa nimelala.” Uchunguzi kuhusu barabara mbili kuu za Marekani ulikadiria kwamba madereva wanaosinzia walisababisha nusu ya misiba katika barabara hizo.

Pia, fikiria hatari za kufanya kazi pamoja na mtu mwenye usingizi. Mtafiti wa Australia, Ann Williamson, anasema hivi: “Watu waliokuwa na deni la usingizi la saa 17 mpaka 19 walipochunguzwa, walitenda kama watu wenye asilimia 0.05 [ya kileo katika damu] au hata vibaya zaidi.” Hiyo inamaanisha kwamba watu hao walikuwa kama watu waliokunywa kileo kingi au kama watu waliopitisha kiwango cha ulevi kinachoruhusika kisheria katika nchi fulani! Kwa kuwa kila mwaka mamia ya maelfu ya misiba inayotukia barabarani na kazini inasababishwa na usingizi, hilo husababisha hasara kubwa kazini na nyumbani. *

Ni mambo gani yanayoweza kusababisha deni la usingizi? Sababu moja ni kufanya kazi kila siku kwa saa 24. Gazeti USA Today linaeleza kwamba hilo ni “tatizo baya sana la kijamii ambalo linaharibu maisha yetu,” na kwamba “wauzaji wa rejareja na watoaji wa huduma wanapata faida kubwa kwa kufanya kazi mchana na usiku.” Katika nchi nyingi, watu hutazama televisheni usiku kucha na kutumia Internet wakati ambapo wanapaswa kulala. Pia, deni hilo linaongezwa na matatizo ya kihisia, ambayo mara nyingi husababishwa na mahangaiko na kuongezwa na mfadhaiko na hekaheka za maisha. Mwishowe, magonjwa fulani husababisha deni la usingizi.

Madaktari wengi hushindwa kuwasadikisha wagonjwa kuchukua tatizo la usingizi kwa uzito. Daktari mmoja alisema kwamba watu fulani huona kwamba kuchoka kila wakati ni “jambo la kuheshimika.” Na kwa kuwa tatizo lao huongezeka polepole, huenda watu wanaokosa usingizi wasitambue kwamba wana ugonjwa hatari wa usingizi. Wengine husema, ‘Nimeanza kuzeeka’ au, ‘Maisha ni magumu, kwa hiyo siwezi kufanya mengi’ au, ‘Sikuzote mimi huwa mchovu kwa sababu sipati wakati wa kutosha wa kupumzika.’

Ni vigumu kulipa deni la usingizi. Hata hivyo, kuelewa hatua za usingizi na kujua dalili za deni la usingizi kunaweza kukuchochea ubadilike. Kutambua dalili za magonjwa hatari ya usingizi kunaweza kuokoa uhai.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Inaaminika kwamba uchovu ulichangia misiba mingi mikubwa ya karne ya 20. Ona gazeti la Amkeni! la Februari 8, 2001, ukurasa wa 6.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Hata kukosa usingizi mara mojamoja kunaweza kusababisha misiba mikubwa