Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu”

“Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu”

“Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu”

Gazeti Excelsior la Septemba 25, 2002, la Mexico City, lilikuwa na makala ya mhariri yenye kichwa kilicho hapa juu. Iliandikwa na Carlo Coccioli, msomi maarufu na mwandishi nchini Mexico. Makala hiyo ilianza hivi:

“Nimemaliza tu kusoma—au niseme kusoma tena, au ni afadhali niseme kusoma tena na tena—kitabu kidogo chekundu cha kustaajabisha—na si kile kilichokuwa maarufu wakati wa Mao Tse-tung. Kitabu hicho [Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu *] si kitabu cha kustaajabisha tu, bali tofauti na ‘Kitabu Kidogo Chekundu’ cha Mao Tse-tung ambacho kimepitwa na wakati, hiki kitaendelea kutumiwa daima. Kwa ufupi, kitabu hicho ni zawadi ambayo Mashahidi wa Yehova wameupa ulimwengu. Kikilinganishwa na vingine, ni kidogo lakini kina thamani kubwa zaidi. Kinaweza kubebwa mfukoni, lakini kama kingepatikana katika maktaba yenye vitabu 90,000, huenda kingekuwa muhimu kuliko vyote.”

Bwana Coccioli aliendelea kueleza kwamba alipokuwa kijana alichagua kazi ambayo atafanya maishani. Alisema hivi: “Katika chuo kikuu, niliamua kusomea jambo ambalo linachochea akili yangu na kunipendeza, yaani somo la dini, hasa zile za Mashariki.” Alieleza kwamba somo la dini lilimvutia na wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu alitunukiwa shahada ya tatu ya mambo yanayohusiana na dini.

Anasema hivi: “Hivyo ninaona ninastahili kusema kwamba kitabu kidogo chekundu nilichopokea kina mambo mazito na muhimu kuhusu mambo ya ajabu ya dini. . . . Kila familia inapaswa kuwa na [kitabu hicho] ili kisomwe tena na tena mara kwa mara. Hakipendekezi dini yoyote, bali ni habari za pekee kuhusu utamaduni wa mwanadamu ambaye anapenda kuchunguza mambo magumu kumhusu Mungu.”

Mwishoni mwa makala yake, Bwana Coccioli aliandika nambari ya simu ya Shahidi aliyempa kitabu hicho. Shahidi huyo amepigiwa simu na watu wengi ambao wanaomba kitabu hicho, hivyo ofisi ya tawi ya Mexico imehakikisha kwamba wale ambao wameomba kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu wamekipata. Mmoja ambaye aliomba vitabu 20 kwa ajili ya familia na marafiki zake anaendelea kufundishwa Biblia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Matoleo ya karibuni ya kitabu hiki yana jalada jepesi na si jekundu.