Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Mauaji ya Kijeuri Mfululizo wa makala wenye kichwa “Je, Mauaji ya Kijeuri Yatakwisha?” (Julai 8, 2003) uliandikwa vizuri sana. Nilifurahia jinsi makala ya kwanza inavyoeleza mambo ya hakika bila kutoa suluhisho. Inamalizia tu kwa maswali muhimu ya kutafakari yanayomwezesha msomaji kuelewa jinsi tatizo hilo lilivyoenea. Halafu masuluhisho ya Kimaandiko yanatolewa. Ama kweli makala hizo zinasisimua!

A. L., Marekani

Makala ya mwisho katika mfululizo huo, yenye kichwa “Je, Kuna Utatuzi wa Kudumu?,” ilinisaidia kujua kwamba watu wanahitaji kubadili maoni na mioyo yao ili kupenda uadilifu. Sote tunahitaji kufundishwa na Yehova Mungu, kama andiko la Isaya 54:13 linavyosema. Hata sasa, tukiwa na msaada wa Yehova, tunaweza kujizoeza kufanya yale ambayo Yehova anataka.

V. K., Marekani

Tour de France Nilifurahia sana makala yenye kichwa “Tour de France—Miaka 100 ya Mashindano Makali ya Baiskeli.” (Julai 8, 2003) Nilikuwa nikishiriki mashindano madogo ya baiskeli. Ijapokuwa kila mwaka mimi hutazama Mashindano ya Tour de France kwenye televisheni, sikujua mwanzo wake au kwamba mwaka wa 2003 ulikuwa mwaka wa 100 wa mashindano hayo. Makala hiyo ilitaja jinsi washiriki ‘wameonyesha uungwana katika michezo.’ Nafikiri hilo ndilo linalowapendeza watu wengi sana.

R. S., Japan

Nina umri wa miaka 10, na nilifurahia sana makala ya Tour de France. Asanteni kwa kueleza mambo mengi sana kuhusu historia ya mashindano ya baiskeli. Natumai mtachapisha makala nyingine kuhusu michezo.

J. F., Ufaransa

Mchanga Nilifurahia kusoma makala yenye kichwa “Maajabu ya Mchanga.” (Mei 8, 2003) Maelezo kuhusu jinsi mchanga unavyofanyizwa na viumbe wanaoishi humo yanapendeza sana. Nimeshangaa kuona kwamba mchanga una rangi nyingi. Lo! Bila mchanga hatungekuwa na bidhaa muhimu sana kama glasi na sementi. Asanteni kwa habari hizo za kufurahisha.

N. N., Afrika Kusini

Kisukari Asanteni sana kwa mfululizo wa makala “Kuishi na Kisukari.” (Mei 8, 2003) Kwa miaka 12 nimeugua ugonjwa wa kisukari wa Aina ya 1, na nimekuwa nikitibiwa mara nyingi kwa insulini. Mke wangu hunisaidia sana. Sote huendelea kujifunza kuhusu ugonjwa huo, sisi huenda kwa daktari pamoja, na ninajaribu kuwa na maoni mazuri. Kwa kuwa mimi ni mwangalizi anayesafiri, nimeona kwamba Wakristo wenzangu wanajua umuhimu wa kuwa wenye fadhili na wenye subira kuelekea mgonjwa ili kumsaidia akabiliane na magumu maishani. Maoni hayo hunisaidia kuendelea kuhudumia makutaniko. Makala hizo zilinifaa sana. Ninasema tena asanteni sana.

W. B., Poland

Nimeugua kisukari kwa miaka 28. Watu 10 katika familia yetu wanaugua ugonjwa huo. Makala zenu zina habari chungu nzima kuliko makala nyingine nilizopata kusoma. Tofauti na makala za kilimwengu, zinaonyesha upendo wa Muumba. Kwa kuwa sikutaka kuwa mzigo kwa familia yetu, nilijaribu kuwaficha wengine kwamba ninaugua. Nilifurahi kuwasaidia wengine. Lakini makala hizo zilinisaidia kuona kwamba ninapaswa kujitunza ili niwatunze wengine vizuri.

L. P., Ufaransa