Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kushinda Maoni Mabaya

Unaweza Kushinda Maoni Mabaya

Unaweza Kushinda Maoni Mabaya

UNAYAONAJE magumu unayokabili? Wataalamu wengi leo wanasema kwamba jibu la swali hilo linaonyesha kwa kiasi kikubwa ikiwa una maoni mazuri au mabaya. Sisi sote hukabili matatizo makubwa maishani, na baadhi yetu hukabili matatizo makubwa kuliko wengine. Hata hivyo, kwa nini watu wengine hushinda magumu, huwa tayari kujaribu tena hali wengine hukata tamaa baada ya kukumbwa na matatizo madogo tu?

Kwa mfano, wazia unatafuta kazi. Unaenda kuhojiwa na hufanikiwi. Unalionaje jambo hilo baadaye? Huenda ukafikiri kwamba hutakikani na kuona kwamba ni tatizo la kudumu, labda ukisema, ‘Hakuna mtu anayeweza kuajiri mtu kama mimi. Sitapata kazi kamwe.’ Au hata unaweza kuruhusu hali hiyo iathiri maoni yako kuhusu mambo yote maishani na kukata kauli kwamba: ‘Siwezi kufanikiwa kamwe. Mimi ni bure kabisa.’ Hayo ni maoni mabaya sana.

Kushinda Maoni Mabaya

Unawezaje kushinda maoni mabaya? Hatua ya kwanza muhimu ni kutambua maoni hayo mabaya. Hatua inayofuata ni kupambana nayo. Tafuta sababu nyingine zinazoonyesha kwa nini hukupata kazi. Kwa mfano, je, ni kweli kwamba hukupata kazi kwa sababu hakuna mtu anayeweza kukuajiri? Au inawezekana kwamba mwajiri alikuwa anatafuta mtu mwenye sifa tofauti na zako?

Ukichanganua hali kwa njia hiyo, utaondolea mbali maoni mabaya. Je, usipofaulu katika jambo moja, hiyo inamaanisha kwamba huwezi kufaulu kamwe? Au je, unaweza kufikiria sehemu nyingine za maisha yako ambapo umefaulu kwa kiasi fulani, kama vile katika mambo ya kiroho, uhusiano katika familia, au kudumisha marafiki? Jifunze kuondoa akilini mwako maoni mabaya na uyaone kuwa yenye kudhuru. Hata hivyo, je, kweli unaweza kuwa na hakika kwamba hutapata kazi kamwe? Kuna mambo mengine unayoweza kufanya ili kuondolea mbali maoni mabaya.

Miradi Inayoweza Kukusaidia Kuwa na Maoni Mazuri

Katika miaka ya karibuni, watafiti wamekuwa na maoni finyu na ya ajabu kuhusu maana ya tumaini. Wanasema kwamba tumaini linahusisha kuamini kwamba utatimiza miradi yako. Kama makala inayofuata inavyoonyesha, tumaini linahusisha mengi zaidi, lakini ufafanuzi huo unaweza kusaidia kwa njia kadhaa. Kuwa na maoni hayo kutatufanya kuwa na miradi inayoweza kutusaidia tuwe na maoni mazuri zaidi.

Ili tuamini kwamba tunaweza kutimiza miradi ya wakati ujao, tunahitaji kuwa tumefanikiwa kufikia miradi fulani. Ikiwa unahisi kwamba hujafanikiwa, huenda ikafaa ufikirie kwa uzito kuhusu miradi unayojiwekea. Kwanza, una miradi yoyote? Ni rahisi sana kuwa na shughuli nyingi maishani kiasi cha kukosa kufikiria mambo muhimu tunayotaka kutimiza maishani. Kuhusiana na kanuni hiyo muhimu ya kutanguliza mambo fulani, Biblia pia ilisema hivi zamani: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”—Wafilipi 1:10.

Tukitambua mambo tunayopaswa kutanguliza, inakuwa rahisi kuweka miradi mbalimbali muhimu kama vile ya kiroho, katika familia, na katika maisha ya kawaida. Hata hivyo, ni muhimu kutoweka miradi mingi sana na kuwa na miradi ambayo tunaweza kutimiza kwa urahisi. Ikiwa ni vigumu sana kufikia mradi fulani, tunaweza kuvunjika moyo na kukata tamaa. Hivyo, ni bora kuugawanya mradi mmoja mkubwa uwe miradi midogo inayoweza kufikiwa kwa muda mfupi.

“Penye nia pana njia.” Huo ni msemo wa kale na una ukweli fulani. Tunapoweka miradi fulani, tunahitaji nia, yaani tamaa na azimio la kuitimiza. Tunaweza kuimarisha azimio hilo kwa kufikiria faida za miradi yetu na thawabu tutakazopata tunapoitimiza. Bila shaka, matatizo yatatokea lakini tunapaswa kuyaona kama mambo tunayohitaji kukabili wala si vizuizi.

Hata hivyo, tunahitaji pia kufikiria njia zinazofaa za kutimiza miradi yetu. Mwandishi C. R. Snyder, ambaye amefanya uchunguzi mwingi kuhusu umuhimu wa tumaini anadokeza kwamba mtu anapaswa kufikiria njia mbalimbali za kutimiza mradi fulani. Kwa hiyo njia moja isipofaulu tunaweza kutumia njia ya pili, ya tatu, na kadhalika.

Snyder pia anapendekeza kujua wakati wa kubadilisha mradi. Ikiwa hatujafaulu kufikia mradi mmoja, tutavunjika moyo tukiendelea kuuhangaikia. Kwa upande mwingine, tukiubadili na mradi mwingine tunaoweza kufikia, tutapata tumaini.

Biblia ina mfano unaoweza kutusaidia. Mfalme Daudi alikuwa na mradi wa kumjengea Mungu wake Yehova hekalu. Lakini Mungu alimwambia Daudi kwamba mwana wake Sulemani ndiye angepata pendeleo hilo. Badala ya kufuatilia mradi huo juu chini au kununa kwa sababu ya jambo hilo lenye kukatisha tamaa, Daudi alibadili mradi wake. Alitumia nguvu zake kukusanya pesa na vifaa vya ujenzi ambavyo mwana wake alihitaji ili kuukamilisha mradi huo.—1 Wafalme 8:17-19; 1 Mambo ya Nyakati 29:3-7.

Hata tukifaulu kuimarisha tumaini letu kwa kushinda maoni mabaya na kuwa na miradi inayotusaidia kusitawisha maoni mazuri, huenda bado tukakosa tumaini. Jinsi gani? Mara nyingi sisi hukosa tumaini kwa sababu zisizoepukika. Tunapofikiria matatizo mengi yanayowapata wanadamu—umaskini, vita, ukosefu wa haki, uwezekano wa kuwa wagonjwa na kufa—tunawezaje kudumisha tumaini?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ikiwa hukupata kazi uliyotaka, je, unafikiri hutapata kazi kamwe?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mfalme Daudi alibadili mradi