Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Wapi Tumaini la Kweli?

Unaweza Kupata Wapi Tumaini la Kweli?

Unaweza Kupata Wapi Tumaini la Kweli?

SAA yako imesimama na inaonekana imeharibika. Unapotaka itengenezwe, inakubidi uchague kati ya mafundi wengi. Unaona matangazo mengi ya biashara, yote yakidai kwa uthabiti kwamba kuna mafundi wanaoweza kutengeneza saa, na madai mengine yanapingana. Namna gani ukitambua kwamba jirani yako ndiye aliyeibuni saa hiyo miaka mingi iliyopita? Isitoshe, anakuambia kwamba yuko tayari kukutengenezea bila malipo. Ni wazi kwamba utamchagua yeye aitengeneze, sivyo?

Sasa linganisha saa hiyo na uwezo wako wa kutumaini. Ukigundua kwamba unapoteza tumaini, kama vile watu wengi wamepoteza tumaini wakati huu wenye taabu, utapata wapi msaada? Watu wengi wanadai kwamba wanaweza kusuluhisha tatizo hilo lakini mapendekezo mengi wanayotoa yanavuruga na yanapingana. Basi mbona usimwendee Yule aliyewaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kutumaini? Biblia inasema kwamba “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu” na kwamba yuko tayari sana kusaidia.—Matendo 17:27; 1 Petro 5:7.

Maana Halisi ya Tumaini

Maoni ya Biblia kuhusu tumaini yanahusisha mengi zaidi kuliko maoni ya kawaida ya madaktari, wanasayansi, na wanasaikolojia wa leo. Maneno ya lugha ya awali yaliyotumiwa katika Biblia ambayo yametafsiriwa “tumaini” yanamaanisha kungojea kwa hamu na kutarajia mema. Tumaini linahusisha mambo mawili. Linatia ndani kutamani mema na pia kuwa na msingi wa kuamini kwamba yatapatikana. Tumaini linalotokana na Biblia si ndoto tu. Linategemea mambo ya hakika na uthibitisho.

Kwa njia hiyo, tumaini ni sawa na imani, ambayo lazima itegemee uthibitisho wala si imani isiyo na msingi. (Waebrania 11:1) Hata hivyo, Biblia inatofautisha kati ya imani na tumaini.—1 Wakorintho 13:13.

Kwa mfano: Unapomwomba rafiki mpendwa akufanyie jambo fulani, unaweza kutumaini kwamba atakusaidia. Tumaini lako lina msingi kwa sababu unamwamini rafiki yako, unamjua vizuri, naye hukutendea kwa fadhili na ukarimu. Kuna uhusiano wa karibu kati ya imani na tumaini lako, na sifa hizo zinategemeana ingawa ni tofauti. Unawezaje kumtumaini Mungu jinsi hiyo?

Msingi wa Tumaini

Mungu ndiye chanzo cha tumaini la kweli. Katika nyakati za Biblia Yehova aliitwa “tumaini la Israeli.” (Yeremia 14:8) Tumaini lolote lenye kutegemeka ambalo watu wake walikuwa nalo lilitoka kwake; hivyo alikuwa tumaini lao. Tumaini hilo halikutegemea kutamani tu. Mungu aliwapa msingi thabiti wa tumaini. Kwa kushughulika nao kwa karne nyingi, alitoa ahadi nyingi na kuzitimiza. Kiongozi wao Yoshua aliwaambia hivi Waisraeli: “Mnajua vema . . . kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi.”—Yoshua 23:14.

Miaka mingi imepita na bado Mungu anatimiza ahadi zake. Biblia ina ahadi nyingi za Mungu za kupendeza na inaeleza kwa usahihi jinsi zilivyotimia. Ahadi zake zilizotabiriwa zinategemeka sana hivi kwamba nyakati nyingine husemwa kana kwamba zilitimia tu wakati zilipotabiriwa.

Ndiyo sababu tunaweza kuiita Biblia kitabu cha tumaini. Unapojifunza jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu, sababu zako za kumtumaini zinaimarishwa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.”—Waroma 15:4.

Mungu Hutupatia Tumaini Gani?

Ni wakati gani tunapohitaji tumaini zaidi? Je, si wakati tunapokabili kifo? Hata hivyo, wakati ambapo mpendwa amekufa ndipo tumaini la wengi hudidimia. Ama kweli kifo hukatisha tamaa zaidi. Kinaandama kila mmoja wetu. Tunaweza kukiepuka kwa muda fulani lakini hatuwezi kukiondoa. Kwa kufaa, Biblia inakiita “adui wa mwisho.”—1 Wakorintho 15:26.

Basi, tunawezaje kuwa na tumaini mpendwa wetu anapokufa? Mstari wa Biblia unaokiita kifo adui wa mwisho, unasema pia kwamba adui huyo ‘ataangamizwa.’ Yehova Mungu ana nguvu kuliko kifo. Amethibitisha hilo mara nyingi. Vipi? Kwa kuwafufua wafu. Biblia inazungumzia pindi tisa ambapo Mungu alitumia nguvu zake kuwafufua wafu.

Katika kisa cha kupendeza, Yehova alimpa Mwana wake Yesu nguvu za kumfufua rafiki yake mpendwa, Lazaro, ambaye alikuwa amekufa kwa siku nne. Yesu hakufanya hivyo kisiri bali alifanya hivyo hadharani, mbele ya umati.—Yohana 11:38-48, 53; 12:9, 10.

Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini watu walifufuliwa? Je, hawakuzeeka na kufa tena baadaye?’ Bila shaka. Hata hivyo, kutokana na masimulizi hayo yenye kutegemeka kuhusu ufufuo, hatutamani tu kuwaona wapendwa wetu wakiwa hai tena; bali pia tuna sababu ya kuamini kwamba watafufuliwa. Kwa ufupi, tuna tumaini la kweli.

Yesu alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yohana 11:25) Yeye ndiye atakayepewa nguvu na Yehova za kufufua wafu ulimwenguni pote. Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Kristo].” (Yohana 5:28, 29) Naam, wote waliomo makaburini wana tumaini la kufufuliwa na kuishi katika paradiso duniani.

Nabii Isaya alieleza ufufuo kwa njia nzuri sana. Alisema: “Wafu wako wataishi. Maiti wangu—wataamka. Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini! Kwa maana umande wako ni kama umande wa miholi, na dunia itawaacha hata wale wasiojiweza katika kifo waanguke katika kuzaliwa.”—Isaya 26:19.

Je, hilo halifariji? Wafu wako katika hali salama kabisa, jinsi mtoto alivyo salama katika tumbo la uzazi la mama yake. Kwa kweli wale walio makaburini wamehifadhiwa vizuri katika kumbukumbu lisiloweza kujaa la Mungu Mweza-Yote. (Luka 20:37, 38) Na karibuni watarudishwa kwenye uhai, waingie katika ulimwengu wenye furaha na uchangamfu kama vile mtoto anayezaliwa anavyokaribishwa na familia yenye upendo! Kwa hiyo, kuna tumaini hata tukikabili kifo.

Jinsi Tumaini Linavyoweza Kukusaidia

Paulo anatufundisha mengi kuhusu umuhimu wa tumaini. Alisema kwamba tumaini ni sehemu muhimu ya mavazi ya silaha za kiroho, yaani, kofia ya chuma. (1 Wathesalonike 5:8) Alimaanisha nini? Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida askari-jeshi alivaa kofia ya chuma juu ya kofia ya sufu au ya ngozi alipoenda vitani. Kofia hiyo ilimsaidia kukinga kichwa chake kisijeruhiwe na kusababisha kifo. Paulo alikuwa akikazia nini? Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa, ndivyo tumaini linavyolinda akili, yaani, uwezo wetu wa kufikiri. Ikiwa una tumaini thabiti linalopatana na makusudi ya Mungu, utakuwa na amani ya akili hata unapopatwa na magumu. Ni nani asiyehitaji kofia hiyo ya chuma?

Paulo alitumia mfano mwingine unaohusianisha tumaini na mapenzi ya Mungu. Aliandika hivi: “Tumaini hilo tunalo kama nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara.” (Waebrania 6:19) Paulo alikuwa amevunjikiwa meli mara kadhaa, hivyo alijua umuhimu wa nanga. Mabaharia walipokumbwa na dhoruba walishusha nanga. Ikiwa nanga ingeshikamana kabisa na sakafu ya bahari, huenda meli ingeokoka dhoruba hiyo badala ya kusukumwa hadi ufuoni na kugonga miamba.

Vivyo hivyo, ikiwa tunaona ahadi za Mungu kuwa tumaini “hakika na imara,” zinaweza kutusaidia kushinda matatizo ya nyakati zetu zenye taabu. Yehova anaahidi kwamba karibuni wanadamu hawatakumbwa na vita, uhalifu, huzuni, au hata kifo. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 10.) Kushikilia tumaini hilo kwaweza kutusaidia kuepuka msiba na kutuchochea kuishi kulingana na kanuni za Mungu badala ya kufuata roho ya ukosefu wa adili iliyoenea sana ulimwenguni leo.

Tumaini ambalo Yehova anatoa linakuhusu wewe binafsi pia. Anataka uishi kama vile alivyokusudia. Anataka “watu wa namna zote waokolewe.” Jinsi gani? Kwanza kila mtu anapaswa “kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Wachapishaji wa gazeti hili wanakusihi upate ujuzi kuhusu kweli ya Neno la Mungu, ujuzi ambao utakuwezesha kupata uzima. Tumaini ambalo Mungu atakupa linapita matumaini yoyote yale ambayo ulimwengu unaweza kukupa.

Ukiwa na tumaini hilo hutakata tamaa kamwe kwa kuwa Mungu anaweza kukupa nguvu unazohitaji kutimiza miradi yoyote uliyoweka ambayo inapatana na kusudi lake. (2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13) Je, huhitaji tumaini kama hilo? Kwa hiyo, ikiwa unahitaji tumaini, au umekuwa ukilitafuta, jipe moyo. Tumaini liko karibu. Unaweza kulipata!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Sababu za Kuwa na Tumaini

Habari hizi zilizo katika Biblia zinaweza kuimarisha tumaini lako:

▪ Mungu anaahidi wakati ujao wenye furaha.

Neno lake linasema kwamba dunia yote itakuwa paradiso itakayokaliwa na familia ya wanadamu yenye umoja na furaha.—Zaburi 37:11, 29; Isaya 25:8; Ufunuo 21:3, 4.

▪ Mungu hawezi kusema uwongo.

Anachukia uwongo wa kila aina. Yehova ni mtakatifu wala hana hatia hata kidogo, kwa hiyo hawezi kusema uwongo.—Methali 6:16-19; Isaya 6:2, 3; Tito 1:2; Waebrania 6:18.

▪ Mungu ana nguvu zisizo na kikomo.

Yehova pekee ndiye mweza-yote. Hakuna kitu chochote ulimwenguni kinachoweza kumzuia kutimiza ahadi zake.—Kutoka 15:11; Isaya 40:25, 26.

▪ Mungu anataka uishi milele.

Yohana 3:16; 1 Timotheo 2:3, 4.

▪ Mungu anatutakia mema.

Yeye hazingatii kasoro na makosa yetu, bali anaangalia sifa zetu nzuri na jitihada zetu. (Zaburi 103:12-14; 130:3; Waebrania 6:10) Anatumaini kwamba tutafanya mema naye hufurahi tunapofanya hivyo.—Methali 27:11.

▪ Mungu anaahidi kukusaidia kutimiza miradi inayopatana na kusudi lake.

Watumishi wake hawapaswi kukata tamaa. Mungu hutoa kwa ukarimu roho yake takatifu, ambayo ndiyo kani yenye nguvu zaidi, ili itusaidie.—Wafilipi 4:13.

▪ Mungu anapaswa kutumainiwa.

Kwa kuwa yeye hutegemeka na ni mwaminifu kabisa, hatakutamausha kamwe.—Zaburi 25:3.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa, ndivyo tumaini linavyolinda akili

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kama nanga, tumaini thabiti linaweza kukuimarisha

[Hisani]

Courtesy René Seindal/Su concessione del Museo Archeologico Regionale A. Salinas di Palermo