Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kwani Nina Shida Gani?’

‘Kwani Nina Shida Gani?’

‘Kwani Nina Shida Gani?’

“Ni kana kwamba maisha yangu yote yalikuwa yamebadilika nilipoamka asubuhi moja. Nilijihisi kuwa mtu tofauti kabisa.”—Sam.

KIPINDI cha kubalehe ni nini? Kwa ufupi, ni kipindi kati ya utoto na utu uzima. Ni wakati unapopatwa na mabadiliko makubwa—kimwili, kihisia, na hata kitabia. Kwa upande mmoja, mwanzo wa kipindi cha kubalehe husisimua. Ama kwa hakika, hilo linaonyesha kwamba karibuni utakuwa mtu mzima. Kwa upande mwingine, mtu huanza kuwa na hisia mpya wakati huo, na nyingine zinaweza kumvuruga na hata kumwogopesha.

Hata hivyo, hupaswi kuogopa kipindi cha kubalehe. Ni kweli kwamba kinaweza kusababisha mahangaiko. Lakini kinakuwezesha kubadilika kuwa mtu mzima kwa njia yenye kufurahisha. Hebu tuone jinsi hilo linavyowezekana kwa kuchunguza kwanza baadhi ya magumu ambayo vijana wanaobalehe hukabili.

Mwanzo wa Kubalehe

Katika kipindi cha kubalehe, mabadiliko hutokea mwilini mwako ili kukutayarisha kwa ajili ya uzazi. Kipindi hicho huchukua miaka kadhaa na hakihusishi tu ukuzi wa viungo vyako vya uzazi kama vile tutakavyoona.

Kwa kawaida wasichana huanza kubalehe wanapokuwa kati ya umri wa miaka 10 na 12, hali wavulana wengi huanza kubalehe wanapokuwa kati ya miaka 12 na 14. Hata hivyo, huo ni wastani tu. Kulingana na kitabu The New Teenage Body Book, “mwili wa kila mtu hutenda kazi kwa utaratibu wake maalumu ambao huamua wakati mabadiliko mbalimbali ya kubalehe yatakapotokea.” Kinaongezea hivi: “Kipindi cha kubalehe hutofautiana sana.” Kwa hiyo, ukianza kubalehe kabla au baada ya marika wako, hiyo haimaanishi kwamba una kasoro.

Vyovyote vile, kubalehe kunaweza kubadili sura yako, hisia zako, na maoni yako kuhusu mambo. Fikiria baadhi ya magumu na mambo yenye kupendeza kuhusu kipindi hiki cha pekee maishani.

‘Kwani Mwili Wangu Una Shida Gani?’

Kubalehe huanza kwa kuongezeka kwa viwango vya homoni, hasa homoni ya estrojeni kwa wasichana na testosteroni kwa wavulana. Mabadiliko ya homoni huchangia kwa kadiri fulani mabadiliko ya kimwili yanayoanza kutukia ghafula. Kwa hakika, kubalehe kukishaanza, mwili wako hukua haraka kuliko ilivyokuwa ulipokuwa mtoto.

Wakati huo viungo vyako vya uzazi huanza kukomaa, lakini hiyo ni sehemu moja tu ya ukuzi wa kimwili. Huenda pia ukarefuka haraka. Ingawa ulipokuwa mtoto ulikuwa ukirefuka kwa sentimeta tano hivi kila mwaka, si ajabu kurefuka mara mbili zaidi ya kiwango hicho unapobalehe.

Katika kipindi hicho, huenda ukaaibikia kwa kiasi fulani mabadiliko ya mwili wako. Hiyo ni kawaida. Kumbuka, huenda sehemu mbalimbali za mwili wako zinakua kwa viwango tofauti-tofauti. Huenda ukafanya mambo kama goigoi kwa kiasi fulani. Lakini uwe na subira, hutakuwa hivyo milele. Hali hiyo inayotukia wakati wa kubalehe itabadilika.

Wakati wa kubalehe wasichana huanza kupata kipindi cha hedhi, ambacho hutukia kila mwezi na kinahusisha kutokwa damu, umajimaji, na mabaki ya chembe kutoka kwenye tumbo la uzazi. * Kwa kawaida katika kipindi cha hedhi mtu huwa na mkakamao na viwango vyake vya homoni hupungua. Kwa kuwa hilo huathiri mwili na hisia, mwanzo wa kipindi cha hedhi unaweza kusababisha wasiwasi mwingi. Teresa, ambaye sasa ana umri wa miaka 17, anakumbuka hivi: “Ghafula, nililazimika kukabiliana na hali mpya. Ilivuruga hisia zangu na kuniumiza. Na ilitukia kila mwezi!”

Hakuna haja ya kuogopa unapoanza kupata vipindi vya hedhi. Vipindi hivyo vinaonyesha kwamba mwili wako unafanya kazi vizuri. Muda si muda, utajua jinsi ya kukabiliana na magumu ya vipindi hivyo. Kwa mfano, wengine wameona kwamba kufanya mazoezi kwa ukawaida hupunguza hali ya kukakamaa. Lakini kila mtu ni tofauti. Huenda ukagundua kwamba unahitaji kupunguza sana utendaji wako wa kimwili wakati wa vipindi hivyo. Jifunze kutambua mahitaji ya mwili wako na kuyatosheleza.

Katika kipindi cha kubalehe, wasichana na wavulana huhangaikia sana sura yao. Teresa anasema: “Wakati huo ndipo nilipoanza kuhangaikia na kujali jinsi watu walivyofikiri kuhusu sura yangu.” Anaongeza hivi: “Na bado mara nyingi mimi huchukia sura yangu. Sipendi jinsi nywele zangu zilivyo, nguo zangu hazinitoshi, na ni vigumu kupata nguo zinazonipendeza!”

Pia unaweza kusumbuliwa na mwili wako kwa njia nyingine. Kwa mfano, tezi za jasho hufanya kazi zaidi katika kipindi cha kubalehe, na hilo linaweza kusababisha utokwe na jasho sana. Kuoga kwa ukawaida na kuhakikisha kwamba nguo zako ni safi, kunaweza kuzuia mwili wako usinuke. Pia, unaweza kutumia marashi.

Vilevile, katika kipindi cha kubalehe tezi za mafuta ngozini mwako hufanya kazi zaidi, na hilo linaweza kusababisha chunusi. Msichana anayeitwa Ann analalamika hivi: “Kila ninapotaka kuonekana mrembo, ninapata chunusi. Huenda haya ni maoni yangu tu, lakini ni kana kwamba chunusi hutokea wakati ambapo mtu hazitaki kabisa.” Teresa amesumbuliwa na chunusi pia. Anasema: “Chunusi hunifanya nihisi kwamba nina sura mbaya na kuona haya kwa kuwa watu wanaponitazama, mimi hudhania kwamba wanatazama chunusi hizo!”

Bila shaka, wavulana pia wanaweza kupata matatizo ya ngozi. Kwa hakika, wataalamu fulani husema kwamba wavulana hupatwa na matatizo ya ngozi zaidi ya wasichana. Iwe wewe ni mvulana au msichana, unaweza kufaidika kwa kuosha sehemu za mwili zenye mafuta mengi kwa ukawaida, kama vile uso, shingo, mabega, mgongo, na kifua. Isitoshe, kuosha nywele kwa sabuni mara nyingi kunaweza kuzuia mafuta yasienee ngozini. Pia, kuna vitu fulani vinavyozuia chunusi. Teresa anasema: “Wazazi wangu walinisaidia kupata dawa za kujipaka. Pia walinishauri nisile sana vyakula visivyofaidi mwili. Ninapokunywa maji mengi na kuepuka vyakula visivyofaidi mwili, chunusi zangu huisha.”

Jambo lingine ambalo huwapata hasa wavulana ni badiliko la sauti. Yaelekea viungo vyako vya sauti vitakuwa vinene na kurefuka wakati wa kubalehe, na hivyo kufanya sauti yako iwe nzito hatua kwa hatua. Jambo hilo lilimpata Bill bila yeye kujua. Anasema: “Sikutambua kwamba sauti yangu ilikuwa imebadilika, ila nilipojibu simu watu walitambua kwamba hawazungumzi na mama yangu wala dada yangu.”

Nyakati nyingine, sauti inayobadilika hukwaruza. Akikumbuka kipindi cha kubalehe, Tyrone anasema: “Hilo ndilo jambo lililoniaibisha zaidi. Wakati wowote nilipokuwa na wasiwasi au kusisimuka, sauti yangu ilikwaruza. Nilijaribu kuzuia hisia zangu, lakini nilishindwa.” Tyrone anaongezea: “Baada ya mwaka mmoja au miwili hivi, hali hiyo iliisha.” Ikiwa hilo linakupata, usifadhaike! Sauti yako pia itaacha kukwaruza na kudumu ikiwa nzito.

‘Kwa Nini Ninahisi Hivi?’

Ni kawaida kwa vijana wanaobalehe kuwa na hisia zenye kufadhaisha. Kwa mfano, huenda huna urafiki wa karibu tena na vijana wengine ambao walikuwa rafiki zako sana mlipokuwa watoto. Huenda hamkukosana. Lakini labda unaona kwamba mapendezi yenu yanatofautiana. Hata huenda ukawaona wazazi wako kuwa wamepitwa na wakati na kushindwa kuwaeleza hisia zako kwa urahisi, ijapokuwa hapo awali uliwategemea sana ili kupata faraja na ulinzi.

Mambo hayo yanaweza kumfanya kijana ahisi upweke. Kitabu kimoja kinasema: “Watafiti fulani wamesema kwamba vijana wanaobalehe hukabili upweke mara nyingi na kwa kiasi kikubwa kuliko walipokuwa watoto au watakapokuwa watu wazima.” Huenda ukaamua kutowaeleza wengine maoni na hisia zako kwa kuogopa kwamba watakuona kuwa mtu wa ajabu. Au labda unasita kuzungumza na wengine kwa kuhisi kwamba hakuna mtu ambaye angependa kuwa rafiki yako.

Vijana wengi wanaobalehe huhisi upweke mara kwa mara na ndivyo ilivyo kwa watu wazima wengi pia. Ni muhimu kukumbuka kwamba baada ya muda hisia hizo zinaweza kwisha. * Kumbuka kwamba, kwa kuwa wewe ni kijana anayebalehe, karibu kila kitu maishani mwako kinabadilika. Maoni yako kuhusu maisha, watu wengine, na hata kujihusu, yanabadilika daima. Hata nyakati nyingine unapojiangalia kwenye kioo, huenda ukajiona kuwa mtu tofauti kabisa! Huenda ukahisi kama Steve, mwenye umri wa miaka 17, alivyosema: “Ni vigumu sana kusema kwamba unajijua hali unabadilika haraka sana.”

Njia bora ya kushinda upweke ni kuchukua hatua ya kuzungumza na wengine. Huenda hilo likahusisha kuwajua watu wengine ambao si wa rika lako. Je, kuna watu wenye umri mkubwa ambao wangependa uwatembelee? Je, unaweza kuwasaidia kazi za nyumbani, hasa ikiwa wanahitaji msaada? Biblia inawatia moyo wote, vijana kwa watu wazima, ‘kupanuka’ na kuwapenda wengine. (2 Wakorintho 6:11-13) Kufanya hivyo kunaweza kumpa mtu nafasi nzuri sana.

Andiko la Biblia lililonukuliwa juu ni mojawapo ya kanuni nyingi ambazo zimewasaidia vijana Wakristo kukabiliana na magumu ya kubalehe. Unaposoma makala inayofuata, fikiria jinsi Neno la Mungu linavyoweza kukusaidia sana maishani mwako unapoendelea kufikia kuwa mtu mzima.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Mwanzoni, vipindi vya hedhi vinaweza kutukia zaidi ya mara moja au chini ya mara moja kwa mwezi. Kiasi cha mtiririko kinaweza kutofautiana sana pia. Hali hizo hazipaswi kukushtua. Hata hivyo, vipindi vya hedhi visivyo vya kawaida vikiendelea kwa mwaka mmoja au miwili, huenda ikafaa kumwona daktari.

^ fu. 24 Ukihisi upweke kwa muda mrefu au ukiendelea kufikiria kujiua, unapaswa kutafuta msaada. Bila kukawia, zungumza na wazazi wako au mtu mzima aliyekomaa unayeweza kumweleza hisia zako.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Wazazi Si Wakamilifu

“Nilipokuwa mtoto, nilifikiri wazazi wangu ni wakamilifu. Lakini nilipobalehe, niliwaona kuwa washamba. Ninamaanisha kwamba nilitambua kuwa wazazi wangu si wakamilifu, na hilo lilinivuruga. Kwa kusikitisha, jambo hilo lilinifanya nishuku maoni na maamuzi yao. Lakini, baada ya kupatwa na hali ngumu, nimeanza kuwaheshimu sana. Naam, wao si wakamilifu, lakini mara nyingi maoni yao huwa sawa. Hata wakikosea, bado wao ni wazazi wangu. Hatua kwa hatua tumeanza kuwa marafiki, na nafikiri hivyo ndivyo inavyokuwa kawaida kati ya wazazi na watoto.”—Teresa, ana miaka 17.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Vijana wengi wamejenga uhusiano wa karibu na watu wenye umri mkubwa