Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kusitawisha Tamaa ya Kujifunza

Jinsi ya Kusitawisha Tamaa ya Kujifunza

Jinsi ya Kusitawisha Tamaa ya Kujifunza

“Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.”—METHALI 22:6, BIBLIA HABARI NJEMA.

JE, UMEWAHI kuwaambia watoto walale wakati jambo la kupendeza linapotukia? Ijapokuwa wamechoka, wanalia, na hata kukasirika, watajitahidi juu chini kukaa macho na kushiriki jambo hilo. Mwandishi John Holt aliandika hivi: “Uhitaji [wao] wa kutaka kufahamu mambo na kuwa na ustadi wa kuyafanya ni mkubwa sana kama vile uhitaji wao wa kula, kupumzika, au kulala. Nyakati nyingine, uhitaji huo unaweza kuwa mkubwa hata zaidi.”

Tatizo ni kwamba ni vigumu kwa watoto kudumisha tamaa ya kujifunza katika maisha yao yote, kutia ndani miaka yao ya shule. Ingawa hakuna siri hususa ya mafanikio, kuna njia kadhaa ambazo zimefaulu zinazoweza kutumiwa na wazazi, walimu, na watoto. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni upendo.

Upendo Utaboresha Uwezo wa Kujifunza

Watoto hutamani kupendwa na wazazi wao. Upendo huo huwafanya wahisi wakiwa salama na kuwa tayari zaidi kuwasiliana, kuuliza maswali, na kuchunguza mambo. Upendo huwachochea wazazi kuzungumza na watoto wao kwa ukawaida na kupendezwa na elimu yao. Kulingana na kitabu Eager to Learn—Helping Children Become Motivated and Love Learning, utafiti unaonyesha kwamba “inaonekana wazazi hasa ndio wanaowachochea watoto kujifunza.” Matokeo mazuri zaidi hupatikana wazazi wanaposhirikiana na walimu. Kitabu hicho kinasema: “Tamaa ya watoto ya kujifunza huchochewa sana kunapokuwa na ushirikiano kati ya wazazi na walimu.”

Wazazi pia huchochea uwezo wa watoto wa kujifunza. Katika uchunguzi wa familia 43, uliofanywa kwa muda mrefu na kuripotiwa katika kitabu Inside the Brain, watafiti “waligundua kwamba watoto waliozungumziwa mara nyingi [katika miaka yao mitatu ya kwanza], walikuwa na akili sana kuliko wale ambao hawakuzungumziwa na wazazi wao mara nyingi.” Kitabu hicho kinaongeza kwamba “wazazi wanaozungumza na watoto wao mara nyingi huwasifu kwa mafanikio yao, hujibu maswali yao, huwapa mwongozo badala ya kuwaamuru, na hutumia maneno mengi kwa njia mbalimbali.” Ikiwa wewe ni mzazi, je, unazungumza na watoto wako kwa ukawaida na kwa njia yenye kujenga?

Upendo Ni Wenye Fadhili na Wenye Kuelewa

Uwezo na vipawa vya watoto hutofautiana. Bila shaka, haitafaa wazazi waruhusu tofauti hizo ziathiri upendo wao kwa watoto wao. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, watu hutambuliwa kwa sababu ya uwezo wao, na hilo linaweza kuwafanya watoto fulani “wafikiri kwamba ili watambuliwe, ni lazima wafanye mambo vizuri kuliko wengine,” chasema kitabu Thinking and Learning Skills. Licha ya kuwafanya watoto “waogope sana kutofanikiwa,” maoni hayo yanaweza pia kuwafanya wahangaike na kufadhaika bila sababu. Gazeti India Today linasema kwamba visa vya vijana kujiua huko India vimeongezeka mara tatu katika miaka 25 iliyopita, hasa kwa sababu ya mahangaiko yanayotokana na mkazo wa kufanya vizuri shuleni na kutotegemezwa na familia.

Pia watoto wanaweza kuathiriwa kihisia wanapoitwa “wapumbavu” au “wajinga.” Maneno hayo ya ukatili huwavunja moyo kujifunza. Hata hivyo, mzazi anapaswa kuonyesha upendo wenye fadhili nyakati zote na kuendeleza tamaa ya mtoto ya kiasili ya kujifunza kulingana na uwezo wake, bila kumfanya aogope kuaibishwa. (1 Wakorintho 13:4) Ikiwa mtoto ana tatizo la kujifunza, wazazi wenye upendo hujaribu kusaidia bila kumfanya mtoto ahisi kwamba yeye ni mjinga au hafai. Ni kweli kwamba hilo linahitaji subira na busara, lakini matokeo huwa mazuri. Upendo huo unaweza kusitawishwaje? Hatua ya kwanza muhimu ni kuwa na mtazamo wa kiroho.

Mtazamo wa Kiroho Hutokeza Usawaziko

Hali ya kiroho inayotokana na Biblia ni muhimu kwa sababu mbalimbali. Kwanza, inatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu elimu ya kilimwengu, yaani, kuiona kuwa muhimu lakini si muhimu zaidi. Kwa mfano, hesabu ina matumizi mengi, lakini haiwezi kumfanya mtu awe na maadili.

Biblia pia hututia moyo tuwe wenye usawaziko kuhusu wakati tunaotumia katika elimu ya kilimwengu, inaposema hivi: “Hakuna mwisho wa kutungwa kwa vitabu vingi, na kushughulika navyo sana huuchosha mwili.” (Mhubiri 12:12) Ni kweli kwamba watoto wanahitaji elimu nzuri ya msingi, lakini haipaswi kuchukua muda wao wote. Pia wanahitaji wakati wa kufanya mambo mengine yanayofaa, hasa mambo ya kiroho yanayoboresha utu wao.

Sifa nyingine ya kiroho inayotajwa katika Biblia ni kiasi. (Mika 6:8) Watu wenye kiasi hutambua mipaka yao, nao hawaathiriwi na tamaa ya makuu na mashindano ya ukatili yanayoonekana katika taasisi nyingi za elimu. Gazeti India Today linasema kwamba sifa hizo mbaya “huwafanya watu washuke moyo.” Tuwe vijana au wazee, sisi hufanikiwa zaidi tunapotii mashauri haya ya Biblia yaliyoongozwa na Mungu: “Na tusiwe wenye kujisifu, wenye kuchochea mashindano juu ya mtu na mwenzake, tukioneana wivu.” “Lakini kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 5:26; 6:4.

Wazazi wanawezaje kutumia kanuni hizo katika elimu ya watoto wao? Njia moja ni kumtia moyo kila mtoto ajiwekee miradi ya kibinafsi na kuchunguza maendeleo yake mwenyewe. Kwa mfano, ikiwa hivi karibuni mwana wako alifanya mtihani wa hesabu au wa kuandika maneno kwa usahihi, mwombe alinganishe matokeo yake na ya mtihani wa awali. Kisha msifu au umtie moyo inapofaa. Kwa kufanya hivyo, utamsaidia kujiwekea miradi anayoweza kutimiza, kuchunguza maendeleo yake, na kushughulikia udhaifu wowote bila kumlinganisha na wengine.

Hata hivyo, siku hizi vijana wengi wenye vipawa huamua kutofanya vizuri shuleni kwa sababu ya kuogopa kudhihakiwa. Vijana wengine husema: “Kufanya vizuri shuleni ni ushamba.” Je, mtazamo wa kiroho unaweza kusaidia katika hali hiyo? Bila shaka! Fikiria andiko la Wakolosai 3:23, linalosema: “Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu.” (BHN) Je, kweli kuna sababu nyingine kubwa zaidi ya kutuchochea kufanya kazi kwa bidii kuliko kumpendeza Mungu? Mtazamo huo mzuri humwezesha mtu kushinda uvutano usiofaa wa marika.

Wafundishe Watoto Wapende Kusoma

Kusoma na kuandika ni mambo ya msingi yanayohitajiwa ili kupata elimu nzuri ya kilimwengu na pia ya kiroho. Wazazi wanaweza kuwachochea watoto wao wapende vitabu kwa kuwasomea tangu utotoni. Daphne, anayefanya kazi ya kusahihisha makala zilizoandikwa, anashukuru kwamba wazazi wake walimsomea kwa ukawaida alipokuwa mtoto. Anasema hivi: “Walinisaidia kupenda kusoma. Kwa hiyo, nilijua kusoma kabla sijaanza shule. Wazazi wangu pia walinifundisha kufanya utafiti ili nijitafutie majibu ya maswali yangu. Mpaka sasa mazoezi hayo yananisaidia sana.”

Kwa upande mwingine, Holt, aliyenukuliwa awali, anaonya kwamba kuwasomea watoto tu “hakutoshi.” Anaongeza hivi: “Ikiwa mzazi na mtoto hawafurahii usomaji huo, basi mtoto hatafaidika. . . . Hata watoto wanaopenda kusomewa kwa sauti . . . hawawezi kufurahia usomaji ikiwa mzazi hafurahii kuwasomea.” Hivyo, Holt anapendekeza kwamba wazazi wachague vitabu wanavyovipenda pia, huku wakikumbuka kwamba huenda watoto wakataka kusomewa vitabu hivyo mara nyingi! Mamilioni ya wazazi ulimwenguni pote hufurahia kuwasomea watoto wao vitabu hivi viwili, Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Vimeandikwa hasa kwa ajili ya watoto na vina picha nyingi, vinawachochea kufikiri, na kuwafundisha kanuni za Mungu.

Timotheo, Mkristo wa karne ya kwanza, alibarikiwa kuwa na mama na nyanya waliopendezwa sana na elimu yake, hasa ya kiroho. (2 Timotheo 1:5; 3:15) Timotheo akawa mwenye kuwajibika na kutegemeka—sifa ambazo haziwezi kutokezwa na elimu ya kilimwengu pekee. (Wafilipi 2:19, 20; 1 Timotheo 4:12-15) Leo, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kuna vijana wengi wa kiume na wa kike walio kama Timotheo kwa sababu wamezoezwa na wazazi wa kiroho wenye upendo.

Fundisha kwa Uchangamfu!

Kitabu Eager to Learn kinasema kwamba mwalimu anayetaka kuwasaidia wengine kupenda kujifunza anapaswa kuwa na “sifa moja, yaani uchangamfu. Walimu wenye uchangamfu huwaonyesha wanafunzi kwamba wanafurahia yale wanayofundisha na jambo hilo huonekana wazi kabisa.”

Hata hivyo, ni wazi kwamba si wazazi au walimu wote walio wachangamfu. Kwa hiyo, wanafunzi wenye hekima hujaribu kujichochea kwa kuona kujifunza kuwa daraka lao. Kitabu kilichotajwa mapema kinasema, “hakuna mtu atakayekuwa na watoto wetu daima ili kuwasaidia kujifunza, kufanya kazi vizuri, kufikiri, na kujitahidi kuboresha stadi zao.”

Kwa mara nyingine tena, hilo linakazia kwamba maadili ambayo watoto hujifunza nyumbani ni muhimu kuliko wanayojifunza shuleni. Je, wazazi mnafurahia kujifunza? Je, hali za nyumbani zinawawezesha watoto kujifunza na kukazia mambo ya kiroho? (Waefeso 6:4) Kumbuka kwamba mfano wako na mafundisho yako yatawachochea watoto wako muda mrefu baada ya wao kumaliza shule na kuondoka nyumbani.—Ona sanduku “Familia Zinazofaulu Kujifunza,” kwenye ukurasa wa 7.

Tambua Kwamba Watu Hujifunza kwa Njia Tofauti

Ubongo wa kila mtu hufanya kazi kwa njia tofauti; kila mtu ana njia yake ya kujifunza. Mtu mmoja anaweza kufanikiwa anapotumia njia fulani, na huenda mwingine asifanikiwe anapoitumia. Hivyo, Dakt. Mel Levine anasema hivi katika kitabu chake A Mind at a Time: “Tukishughulika na watoto kwa njia ileile, hatuwatendei vizuri. Kila mtoto ana mahitaji yake ya kujifunza; na ana haki ya kutimiziwa mahitaji hayo.”

Kwa mfano, watu fulani huelewa na kukumbuka mambo vizuri wanapoona picha au michoro. Wengine hupendelea maandishi au mazungumzo, au yote mawili. Levine anasema: “Njia bora ya kukumbuka habari fulani ni kuibadilisha kwa njia fulani. Ikiwa ni picha, ieleze kwa maneno, ikiwa ni maneno, piga picha akilini.” Njia hiyo hufanya kujifunza kunufaishe na kufurahisha pia.

Ni wazi kwamba huenda ukahitaji kuchunguza njia itakayokufaa. Hans, mhudumu Mkristo wa wakati wote, alimfundisha Biblia mwanamume mmoja mzee anayeitwa George ambaye alikuwa na elimu ya msingi tu. George hakuelewa na kukumbuka mambo kwa urahisi. Hivyo, Hans akajaribu kukazia mambo makuu kwa kuchora picha sahili. Hans anasema hivi: “George alianza kufanya maendeleo. Hata alianza kuelewa na kukumbuka mambo vizuri sana hivi kwamba yeye mwenyewe akashangaa! Nilipogundua jinsi akili yake inavyofanya kazi, nilitambua kwamba alikuwa mwenye akili kuliko nilivyokuwa nimedhania. Punde si punde akaanza kujiamini na kutazamia kwa hamu pindi za kujifunza kuliko ilivyokuwa mwanzoni.”

Hata Wazee Wanaweza Kujifunza

Kitabu Inside the Brain kinasema: “Uwezo wa ubongo unategemea ikiwa unatumiwa au hautumiwi. Ubongo ni kama mashine ambayo mtu anapaswa kutumia ili iendelee kufanya kazi vizuri, nao uko tayari kujifunza mambo mapya.” Pia kinasema: “Kama vile mazoezi ya mwili yanavyowasaidia watu walio katika miaka ya 70 na 80 kuwa wenye nguvu, watafiti wanaonyesha kwamba mazoezi ya akili yanaweza pia kusaidia ubongo wa wazee. Kwa muda mrefu imedhaniwa kwamba uzee hufanya ubongo uzorote na kuchanganyikiwa. Lakini uchunguzi wa karibuni umeonyesha kwamba mambo hayo hutukia mtu anapokuwa na maoni hayo na anapoacha kuutumia ubongo. Isitoshe, watu hawapotezi chembe nyingi za ubongo kila siku wanapozidi kuzeeka kama ilivyodhaniwa.” Kwa kawaida kuzorota sana kwa uwezo wa ubongo ni dalili ya ugonjwa fulani, kama vile ugonjwa wa moyo.

Ni kweli kwamba uwezo wa ubongo unaweza kupungua kwa kiasi fulani mtu anapozidi kuzeeka lakini si lazima upungue sana. Watafiti wanasema kwamba ubongo unaozoezwa hauzoroti hasa ikiwa mtu anafanya mazoezi ya mwili kwa ukawaida. Kitabu Elderlearning—New Frontier in an Aging Society kinasema: “Kadiri mtu anavyojifunza, ndivyo uwezo wake wa kujifunza unavyoongezeka. Watu wanaoendelea kujifunza ndio wanafunzi bora.”

Jambo hilo lilionyeshwa katika uchunguzi wa miaka 20 uliofanywa huko Australia kuhusu watu wenye umri wa miaka 60 mpaka 98. Maksi ambazo wahusika wengi walipata katika mitihani ya kupima akili zilipungua kwa karibu asilimia 1 tu kila mwaka. Hata hivyo, “maksi za wahusika fulani kutia ndani wale wenye umri wa miaka 90 hazikupungua hata kidogo,” yasema ripoti hiyo. “Wengi wao walizoea kujifunza kwa utaratibu maalum, kama vile kujifunza lugha ya kigeni na/au kucheza ala ya muziki.”

George, aliyetajwa awali, alianza kujifunza Neno la Mungu alipokuwa na umri wa miaka 70 na kitu. Vivyo hivyo, Virginia, ambaye sasa ana miaka 80 na kitu, na mume wake, Robert, ambaye sasa amekufa, walianza kujifunza Biblia katika miaka yao ya uzeeni. Virginia anasema: “Ingawa Robert hakuweza kuona vizuri, alitoa hotuba fupi za Biblia kwenye Jumba la Ufalme akitumia mihtasari aliyokuwa amekariri. Kwa upande wangu, sikufurahia kusoma, lakini sasa ninapenda kusoma. Leo asubuhi nilisoma toleo zima la Amkeni!”

George, Robert, na Virginia ni mifano mitatu tu ya wazee wengi ambao wamekataa maoni mabaya na kutumia akili zao vizuri. Utafiti unaonyesha kwamba ubongo uliopata ujuzi kwa miaka 70 au 80 ni kama pipa kubwa lenye tone moja tu la maji—ujuzi mdogo kama nini! Kwa nini ubongo una uwezo mkubwa hivyo?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Intaneti na Televisheni—Je, Zinasaidia au Zinadhuru?

Kitabu A Mind at a Time kinasema: “Kuna faida na hasara za kutumia Intaneti.” Kujifunza kupata habari kunaweza kusaidia sana, lakini kulingana na kitabu hicho, wanafunzi fulani “hutoa habari kwenye Intaneti bila kuzielewa kikamili wala kuzihusianisha na mambo wanayojua. Basi, huenda hiyo ikawa njia mpya ya kujifunza mambo kijuujuu tu au hata ya kuwafundisha watu mbinu za kuiba ujuzi wa wengine.”

Watafiti wanasema kwamba kutumia muda mwingi sana kutazama televisheni kunaweza kudhoofisha uwezo wako wa kutatua matatizo, stadi za kusikiliza, uwezo wa kufikiri, na hakufundishi maadili. Kitabu Eager to Learn kinasema kwamba “televisheni zinapaswa kuwa na maandishi yenye kuonya kuhusu hatari zake kama yale maonyo yaliyo kwenye pakiti za sigara.”

Chanzo kingine kinasema kwamba kile ambacho watoto wanahitaji hasa ni “kujifunza lugha (kwa kusoma na kuzungumza), kupendwa, na kukumbatiwa kwa uchangamfu mara nyingi.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Familia Zinazofaulu Kujifunza

Mambo yafuatayo yanaweza kuisaidia familia yako kufaulu kujifunza:

▪ Wajulishe watoto wako mara nyingi na kwa upendo kwamba unawatarajia wajiendeshe vyema na kufanya vizuri shuleni

▪ Watoto wanapaswa kufahamu kwamba mafanikio yanatokana na kufanya kazi kwa bidii

▪ Kujishughulisha wala si kukaa kitako tu

▪ Watoto watumie wakati mwingi kila juma kujifunza nyumbani na vilevile kufanya kazi za shule, kusoma ili kujifurahisha, kufanya mambo wanayopenda, kufanya kazi pamoja na familia, kuzoezwa kazi za nyumbani, na kupewa migawo

▪ Watoto wanapaswa kuiona familia yao kuwa mahali ambapo wanaweza kutegemezwa na kupata suluhisho la matatizo yao

▪ Watoto waelezwe sheria za nyumbani waziwazi na zitekelezwe kwa uthabiti

▪ Wazazi wawasiliane na walimu mara nyingi

▪ Wazazi wahangaikie hasa maendeleo ya kiroho ya watoto wao

[Picha]

Wazazi, je, mnawafundisha watoto kufurahia kujifunza?

[Hisani]

Mapendekezo haya yametolewa katika kitabu Eager to Learn—Helping Children Become Motivated and Love Learning.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Njia za Kuboresha na Kufanya Kujifunza Kufurahishe

Kupendezwa Ukipendezwa na jambo fulani utajifunza jambo hilo kwa hamu. Kitabu Motivated Minds—Raising Children to Love Learning kinasema hivi: “Watafiti wameonyesha wazi kwamba watoto wanapofurahia kujifunza, wanajifunza kwa undani, wanafaidika, na wanajifunza kwa muda mrefu. Pia wao hutaka kuendelea kujifunza, huwa wabunifu zaidi, na huwa tayari kufanya kazi ngumu zaidi.”

Husianisha Mambo Unayojifunza na Maisha Mwandishi na mwalimu Richard L. Weaver II anaandika hivi: “Wanafunzi wanapohusianisha mambo wanayojifunza darasani na mambo ya kawaida maishani, hilo huwachochea kuyaelewa kama vile cheche ya umeme inavyowasha taa.”

Jaribu Kuelewa Watu wanapojaribu kuelewa jambo fulani, wao huchochea uwezo wao wa kufikiri na kumbukumbu yao. Kujifunza kwa kukariri mambo hufaa nyakati nyingine, lakini hakupaswi kuchukua mahali pa kuelewa. Methali 4:7, 8 inasema, ‘Pamoja na vyote unavyojipatia, jipatie uelewaji. Uheshimu sana, nao utakuinua.’

Kaza Fikira “Kukaza fikira ni muhimu sana katika kujifunza,” chaeleza kitabu Teaching Your Child Concentration. “Kukaza fikira ni muhimu sana hivi kwamba imesemwa kuwa ili mtu awe mwenye akili ni lazima akaze fikira, na hata kukaza fikira kumelinganishwa na kuwa na akili.” Mtu anaweza kufundishwa kukaza fikira. Njia moja muhimu ni kuanza kwa vipindi vifupi vya kujifunza, kisha kuvirefusha hatua kwa hatua.

Fafanua Mambo Dakt. Mel Levine anasema hivi katika kitabu chake A Mind at a Time: “Wanafunzi bora ni wale wanaofafanua mambo vizuri.” Kufafanua mambo hugawanya habari katika visehemu vidogo vinavyoweza kukumbukwa kwa urahisi. Watu wenye ustadi wa kuandika maandishi mafupi hutumia kanuni hiyo badala ya kuandika kila kitu neno kwa neno.

Husianisha Habari Katika kitabu The Brain Book, Peter Russell anasema kwamba mambo unayokumbuka hutegemea habari ulizojifunza zamani. Mtu huboresha kumbukumbu yake anapohusianisha vizuri mambo mapya na mambo ambayo tayari anajua. Kadiri unavyohusianisha habari, ndivyo utakavyokumbuka vizuri zaidi.

Piga Picha Akilini Mtu hukumbuka mambo anayoyaona kihalisi. Kwa hiyo, ikiwezekana, jaribu kuwazia mambo unayojifunza. Watu wanaochunguza kumbukumbu hutumia njia hiyo na mara nyingi wao huwazia mambo ya kuchekesha yanayowasaidia kukumbuka.

Pitia Habari Ulizojifunza Katika kipindi cha saa 24, tunaweza ku- sahau asilimia 80 hivi ya yale ambayo tumejifunza. Kwa kupitia kwa ufupi habari tulizojifunza baa- da ya kila kipindi cha kujifunza, ki- sha kuyapitia tena baada ya siku moja, juma moja, mwezi mmoja, na hata miezi sita, tutaboresha kumbukumbu yetu sana, na hata kukumbuka karibu mambo yote tuliyojifunza.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wazazi na walimu wanapaswa kushirikiana kuwasaidia watoto kujifunza

[Picha katika ukurasa wa 10]

Uzee si kizuizi cha kujifunza