Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Mungu Anawajali Watoto?

Je, Kweli Mungu Anawajali Watoto?

Maoni ya Biblia

Je, Kweli Mungu Anawajali Watoto?

MAMIA ya mamilioni ya watoto wanatendewa vibaya, wanadhulumiwa na kushambuliwa kijeuri kila mwaka. Wengi hufanya kazi kama watumwa katika hali zenye hatari. Wengine wanatekwa nyara na kulazimishwa kuwa wanajeshi au makahaba. Watoto wengi wameacha kuwatumaini watu kwa sababu watu fulani wa ukoo wamefanya ngono nao na pia wametendewa matendo mengine ya kikatili.

Inaeleweka kwamba watu wenye nia nzuri na wanaojali huhangaikia hali yenye kusikitisha ya watoto. Ijapokuwa wanakubali kwamba pupa na upotovu ndivyo visababishi vikuu vya hali hiyo, huenda watu fulani wasielewe kwa nini Mungu mwenye upendo anaweza kuruhusu ukosefu huo wa haki. Huenda wakahisi kwamba Mungu amewaacha watoto hao na kwamba labda hawajali. Je, ni kweli? Je, uhakika wa kwamba mara nyingi watoto wanatendewa vibaya na kudhulumiwa wamaanisha kwamba Mungu hawajali? Biblia ina maoni gani?

Mungu Huwashutumu Wanaowadhulumu Watoto

Yehova Mungu hakukusudia kamwe watoto wadhulumiwe na watu wakatili. Kudhulumiwa kwa watoto ni mojawapo ya matokeo mabaya zaidi ya uasi wa wanadamu katika bustani ya Edeni. Kukataa utawala wa Mungu kuliwafanya wanadamu wawadhulumu wenzao kikatili.—Mwanzo 3:11-13, 16; Mhubiri 8:9.

Mungu huwachukia watu wanaowadhulumu wadhaifu na wasio na uwezo. Mataifa mengi ya kale ambayo hayakumtumikia Yehova yalizoea kuwatoa watoto wao kuwa dhabihu, lakini Yehova alisema kwamba hilo ni ‘jambo ambalo hakuliamuru wala halikuingia moyoni mwake.’ (Yeremia 7:31) Mungu aliwaonya hivi watu wake wa kale: “Mkimtesa hata kidogo [mvulana asiye na baba], naye anililie hata kidogo, sitakosa kukisikia kilio chake; nayo hasira yangu itawaka kwelikweli.”—Kutoka 22:22-24.

Yehova Anawapenda Watoto

Mwongozo wa hekima ambao Mungu anawapa wazazi unaonyesha kwamba anawajali watoto. Kuna uwezekano mkubwa kwamba watoto waliolelewa katika familia zenye upendo watakuwa watu wazima walio wakomavu na wenye nidhamu. Hivyo, Muumba wetu alianzisha mpango wa kudumu wa ndoa ambamo “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Katika Biblia, mahusiano ya ngono yanakubaliwa tu katika ndoa ili watoto wanaozaliwa watunzwe chini ya hali nzuri.—Waebrania 13:4.

Pia Maandiko hukazia umuhimu wa wazazi kuwazoeza watoto. Biblia inasema: “Wana ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu. Kama mishale mkononi mwa mwanamume mwenye nguvu, ndivyo walivyo wana wa ujanani.” (Zaburi 127:3, 4) Watoto ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu naye anataka wafanikiwe. Kama vile mtu anayetupa mishale anavyopima kwa uangalifu kabla ya kuitupa, ndivyo Mungu anavyowahimiza wazazi kuwaongoza watoto vizuri maishani. Neno la Mungu linaagiza hivi: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

Pia Yehova ameonyesha upendo wake kwa watoto kwa kuwafundisha wazazi jinsi ya kuwalinda watoto wao dhidi ya watu wakatili. Katika Israeli ya kale hata “watoto wadogo” waliamuriwa kusikiliza Sheria ambayo ilitambulisha wazi mwenendo unaofaa na usiofaa kuhusu ngono. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Mambo ya Walawi 18:6-24) Mungu anataka wazazi wajitahidi wawezavyo kuwalinda watoto wao kutokana na mtu yeyote anayeweza kuwadhulumu au kuwatenda vibaya.

Tumaini kwa Watoto

Upendo mkubwa wa Yehova kwa watoto ulionyeshwa wazi na Yesu Kristo anayefananisha kikamili utu wa Baba yake. (Yohana 5:19) Wakati mitume wake walipojaribu kimakosa kumsaidia Yesu kwa kuwazuia wazazi wasimletee watoto wao, Yesu aliwasahihisha kwa ukali. Alisema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu.” Kisha, “akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki.” (Marko 10:13-16) Yehova Mungu na Mwana wake wanawathamini watoto.

Kupitia Mfalme wake aliyewekwa rasmi, Yesu Kristo, karibuni Mungu atachukua hatua ya kuwasaidia watoto wanaodhulumiwa. Watu wanaowadhulumu watoto kwa pupa na ukatili katika ulimwengu huu, wataharibiwa kabisa. (Zaburi 37:10, 11) Kwa habari ya wapole wanaomtafuta Yehova, Biblia inasema: “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

Kwa sasa, Mungu anaonyesha upendo wake kwa kutoa msaada wa kiroho na wa kihisia kwa wote wanaodhulumiwa. Anaahidi hivi: “Aliyepotea nitamtafuta, na aliyefukuzwa nitamrudisha, na aliyevunjika nitamfunga na anayeugua nitamtia nguvu.” (Ezekieli 34:16) Kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na kutaniko la Kikristo, Yehova huwafariji watoto wanaokandamizwa na wenye uhitaji. Ni shangwe iliyoje kujua kwamba sasa na wakati ujao, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, . . . hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

© Mikkel Ostergaard /Panos Pictures