Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Daraka Lako Ukiwa Mzazi

Daraka Lako Ukiwa Mzazi

Daraka Lako Ukiwa Mzazi

“UKIMFANYA mtoto ahisi kwamba anapendwa, kwamba yeye ni sehemu ya familia, kwamba yeye ni mtu wa maana, na kumchochea kuuliza maswali, ubongo wake utasitawi,” asema Peter Gorski wa Chuo cha Kitiba cha Harvard. “Daraka letu tukiwa wazazi si kufanya ubongo uwe mkamilifu, bali ni kumsaidia mtoto awe mtu mwenye afya, timamu, na anayejali.”

Inaridhisha kwa mzazi kuona mtoto wake akikua na kuwa mtu mwenye maadili ambaye anawajali wengine. Ili ufanikiwe kufanya hivyo, unahitaji kuwa mfano mzuri kwa mtoto wako, kuwa rafiki yake, kuwasiliana naye, na kumfundisha. Ingawa watoto wote huzaliwa na uwezo wa kuwa na maadili, ni lazima wazazi wawafundishe watoto kanuni za maadili hatua kwa hatua kadiri wanavyoendelea kukua.

Utu wa Mtoto Hutegemea Nani?

Watafiti wana maoni mbalimbali kuhusu yule ambaye anahusika zaidi katika kusitawisha utu wa mtoto. Baadhi yao huona kwamba utu wa mtoto husitawishwa hasa na marafiki zake. Lakini, Dakt. T. Berry Brazelton na Dakt. Stanley Greenspan, ambao ni wataalamu wanaoshughulikia ukuzi wa watoto, wanaona kwamba mzazi ana daraka kubwa zaidi la kumfundisha mtoto mchanga kwa huruma.

Zaidi ya mazoezi ambayo mtoto hupata akiwa mchanga, mambo yanayompata baadaye maishani na uvutano wa marafiki zake, huchangia ukuzi wa utu wake. Ni muhimu watoto waonyeshwe huruma na wajue kwamba wengine katika familia wanawajali. Wanahitaji pia kufundishwa jinsi ya kushughulikia hisia zao vizuri. Kwa kawaida, watoto ambao huzoezwa kwa njia hiyo huwa tayari kushirikiana, huwa wenye huruma, na wenye fadhili zaidi kuwaelekea wengine.

Ni kazi ngumu kumzoeza mtoto tangu utotoni. Ili mfanikiwe, hasa ikiwa nyinyi ni wazazi wapya, ni muhimu mwombe mashauri kutoka kwa wengine wenye ujuzi na kuendelea kuyafuata. Wataalamu wameandika vitabu vingi sana kuhusu ukuzi wa mtoto. Mara nyingi, yale wanayosema yanapatana na mashauri yenye kutegemeka yanayopatikana katika Biblia. Wazazi ambao wametumia kanuni za Neno la Mungu wamefanikiwa kuwalea watoto wao vizuri. Kwa mfano, fikiria mwongozo ufuatao.

Onyesha Upendo Mwingi

Watoto ni kama mimea midogo ambayo hukua na kusitawi inapotunzwa vizuri na kwa ukawaida. Maji na mwangaza wa jua husitawisha mmea mdogo na kuufanya ukue vizuri na kuimarika. Vivyo hivyo, wazazi ambao mara nyingi huwaambia na kuwaonyesha watoto wao kwamba wanawapenda watasitawisha ukuzi wa akili na wa kihisia wa watoto na kuwaimarisha.

Biblia husema hivi kwa ufupi: “Upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Wazazi wanaowaonyesha watoto wao upendo mwingi, wanamwiga Muumba wao, Yehova Mungu. Biblia husema kwamba Yesu alipobatizwa, alimsikia Baba yake akisema kwamba anamkubali na kumpenda akiwa Mwana Wake. Ijapokuwa Yesu alikuwa mtu mzima, jambo hilo lilimtia moyo sana!—Luka 3:22.

Upendo unaowaonyesha watoto wako, muda unaotumia pamoja nao kabla hawajalala, na pia michezo mnayocheza pamoja nao ni muhimu katika ukuzi wao. Dakt. J. Fraser Mustard anasema: ‘Ujuzi wa mtoto huongezeka kila mara anapofanya kitu. Ikiwa mtoto anajifunza kutambaa, jinsi unavyomtia moyo na kuitikia ni muhimu.’ Upendo na uangalifu unaoonyesha ukiwa mzazi humwekea mtoto msingi mzuri wa kusitawi na kuwa mtu mzima mkomavu, anayetimiza madaraka yake.

Uwe Rafiki ya Mtoto na Uwasiliane Naye

Kuwa pamoja na watoto wako huimarisha uhusiano wenu. Isitoshe, hilo hukuza ustadi wa kuwasiliana. Maandiko hutuhimiza kuwa na uhusiano huo wa karibu, iwe ni nyumbani au mahali pengine popote au wakati wowote ule.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; 11:18-21.

Wataalamu wanaoshughulikia ukuzi wa watoto husema kwamba wakati ambao wazazi hutumia na watoto wao ni muhimu kuliko vitu vya kuchezea vya bei ghali au kufanya shughuli nyingine yoyote ya pekee. Unaweza kuwasiliana na watoto wako mnapofanya shughuli za kawaida na zisizogharimu sana. Kwa mfano, wazazi wanaweza kuzungumza na watoto wao na kuwauliza maswali muhimu wanapotembelea mbuga ya wanyama.

Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kurukaruka.” (Mhubiri 3:1, 4) Kucheza kwa njia ya kawaida ni muhimu ili kusitawisha uwezo wa akili wa mtoto, hisia zake, na uwezo wake wa kushirikiana na wengine. Dakt. Mustard anasema ni lazima mtoto acheze. Anasema hivi: “Watoto huwezesha ubongo wao kufanya mambo mbalimbali hasa wanapocheza.” Mtoto anaweza kutumia vitu vya kawaida anapocheza, kama vile boksi tupu. Watoto wanaweza kuvutiwa kucheza na vitu vya kawaida vya nyumbani vilivyo salama sawa na vile wanavyovutiwa na vitu vya kuchezea vya bei ghali. *

Wataalamu wanaona kwamba kumpangia mtoto shughuli nyingi zinazoongozwa na watu wazima kunaweza kuathiri uwezo wao wa kuwazia na kubuni mambo. Kiasi kinahitajiwa. Acha mtoto wako agundue mambo mwenyewe na ajaribu kutumia uwezo wake. Mara nyingi mtoto atapata jambo la kufanya litakalomfurahisha. Hata hivyo, bado una daraka la kujua kile ambacho mtoto wako anafanya na mahali anapochezea ili asijiumize.

Tenga Wakati wa Kumfundisha Mtoto

Kufundisha ni sehemu muhimu ya kuzoeza na kulea watoto ili wawe na sifa nzuri. Wazazi wengi hutenga wakati kila siku ili kuwasomea watoto wao kwa sauti. Hilo huwapa nafasi ya kuwafundisha watoto wao tabia nzuri na maadili yanayotegemea maagizo ya Muumba wetu. Biblia inasema kwamba ‘tangu utoto mchanga’ mwalimu mwaminifu na mishonari aliyeitwa Timotheo ‘aliyajua maandishi matakatifu.’—2 Timotheo 3:15.

Kumsomea mtoto wako kunaweza kuchochea ubongo wake. Ni muhimu mtoto asomewe na mtu aliye chonjo na anayejali. Profesa wa elimu, Linda Siegel anatoa tahadhari hii kuhusu habari ambayo mtoto anapaswa kusomewa: “Inapaswa impendeze mtoto.” Pia, jitahidi kumsomea wakati uleule kila siku. Kwa kufanya hivyo, mtoto atakuwa akitarajia kwa hamu kusomewa.

Kufundisha kunatia ndani kutia nidhamu. Watoto wanaweza kunufaika wanapotiwa nidhamu kwa upendo. Methali 13:1 inasema: “Mwana ni mwenye hekima palipo na nidhamu ya baba.” Hata hivyo, unapaswa kukumbuka kwamba nidhamu inahusisha mambo mengi. Kwa mfano, inaweza kutia ndani kumrekebisha mtoto kwa maneno au kumnyima mapendeleo fulani. Dakt. Brazelton, aliyenukuliwa mapema, anasema kwamba nidhamu inahusisha “kumfundisha mtoto jinsi ya kudhibiti hisia zake na tabia nyingine zinazopita kiasi. Kila mtoto hutaka kujua ikiwa kuna mipaka. Nidhamu ndilo jambo la pili muhimu unalopaswa kumpa mtoto, baada ya upendo.”

Ukiwa mzazi, unawezaje kujua ikiwa nidhamu yako ina matokeo? Kwanza, watoto wako wanapaswa kujua sababu ya kutiwa nidhamu. Wakati wowote unapowarekebisha watoto wako, fanya hivyo kwa njia itakayowaonyesha kwamba unawajali na kuwapenda.

Jitihada Zinazofanikiwa

Baba mmoja anayeitwa Fred alimsomea binti yake kwa ukawaida kabla ya kulala tangu akiwa mchanga. Baada ya muda, alitambua kwamba binti yake anakumbuka hadithi nyingi, anafuatana naye anaposoma, na kupatanisha maneno na sauti. Chris pia ni mzazi mwingine aliyejitahidi sana kuwasomea watoto wake. Alijitahidi kusoma habari tofauti-tofauti. Watoto walipokuwa wachanga sana, alitumia picha zilizomo katika vitabu kama vile Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kufundisha masomo ya kiadili na ya kiroho. *

Mbali na kuwasomea watoto, wazazi fulani huwahusisha watoto wao katika shughuli mbalimbali kama kuchora, kupaka rangi, kucheza muziki, na kutembelea maeneo mbalimbali kama vile mbuga za wanyama. Wazazi wanaweza kutumia pindi hizo kufundisha na kukazia kanuni za maadili na tabia njema ndani ya mioyo na akili ya mtoto.

Je, kazi na jitihada hizo zina matokeo yoyote? Wazazi wanapojitahidi kufuata mashauri ambayo tumezungumzia katika familia yenye amani na usalama, inaelekea watoto wao watasitawisha maoni yanayofaa. Ukiwazoeza watoto wako wachanga na kusitawisha uwezo wao wa akili na ustadi wa kuwasiliana, utakuwa umewasaidia sana kusitawi kiroho na kiadili.

Karne nyingi zilizopita, Biblia ilisema hivi katika Methali 22:6: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” Bila shaka, wazazi wana daraka muhimu la kumzoeza mtoto. Waonyeshe watoto wako upendo mwingi. Tumia wakati mwingi pamoja nao, wazoeze, na uwafundishe. Ukifanya hivyo, wewe na watoto wako mtapata furaha.—Methali 15:20.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ona makala “Vitu vya Kuchezea vya Afrika Bila Malipo,” katika gazeti la Amkeni! la Machi 22, 1993.

^ fu. 23 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, ambacho pia kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova, kinatumiwa kuwafundisha watoto wachanga.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Kucheza na Mtoto Wako Mchanga

▪ Watoto wachanga hawawezi kuwa makini kwa muda mrefu, hivyo cheza nao wakati tu wanapofurahia mchezo.

▪ Ikiwa atatumia vitu vya kuchezea, hakikisha kwamba vitu hivyo ni salama na vinachochea akili.

▪ Chezeni michezo ambayo itawapa watoto nafasi ya kufanya mambo. Watoto wachanga hufurahia sana kukuona ukifanya jambo lilelile tena na tena kama vile kuokota kitu cha kuchezea ambacho wameangusha.

[Hisani]

Source: Clinical Reference Systems

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Madokezo Kuhusu Kuwasomea Watoto Wako

▪ Sema kwa njia inayoeleweka wazi na utamke maneno vizuri. Mtoto hujifunza lugha kwa kuwasikiliza wazazi wakiongea.

▪ Waonyeshe watoto kwa kidole na utaje majina ya watu na vitu vinavyotajwa katika hadithi mnayosoma.

▪ Mtoto anapoendelea kukua chagua vitabu vinavyofaa mahitaji yake ya wakati huo.

[Hisani]

Source: Pediatrics for Parents

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Furahia pindi za burudani pamoja na watoto wako