Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Laiti Wangejua!”

“Laiti Wangejua!”

“Laiti Wangejua!”

DAVID alipomaliza shule aliamua kutenda tofauti na vijana wengine ambao huwa na miradi ya kimwili. Katika Septemba 2003, yeye na rafiki yake walihama Illinois, Marekani kwenda Jamhuri ya Dominika. * Familia yao na rafiki zake walimwita Davey. Alijifunza Kihispania na kushirikiana na Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Navas katika kazi ya kuhubiri. Kutaniko hilo lilimkaribisha. Juan, ambaye ndiye mzee peke yake katika kutaniko hilo, alisema hivi: “Davey alifanya kila kitu alichoombwa kufanya. Kila wakati alijitolea kuwatumikia wengine, na akina ndugu walimpenda.”

Davey alipenda mgawo wake. Alimwandikia hivi rafiki yake anayeishi kule Marekani: “Ninafurahia maisha kabisa huku. Utumishi unaburudisha sana! Sisi huzungumza kwa dakika 20 hivi na wenye nyumba kwani wao hutaka kusikia ujumbe wetu. Tayari ninaongoza mafunzo sita ya Biblia, lakini bado tunahitaji msaada. Pindi moja watu 103 walihudhuria mkutano katika kutaniko letu lenye wahubiri 30 wa Ufalme!”

Kwa kusikitisha, mnamo Aprili 24, 2004, Davey na kijana mwingine katika kutaniko letu walikufa katika msiba. Hadi wakati wa kifo chake, Davey alifurahia sana kazi yake, na aliwatia moyo vijana wengine wa kwao wajiunge naye. Alimwambia hivi kijana mmoja Shahidi: “Utumishi huo utabadili maoni yako.”

Davey alibadili maoni yake kuhusu mambo ya kimwili. Baba yake anakumbuka: “Wakati mmoja alipotutembelea nyumbani, alialikwa kwenda kuteleza kwenye barafu. Aliuliza ingemgharimu pesa ngapi. Alipoambiwa gharama yake, Davey alisema hawezi kutumia kiasi hicho ili tu kuteleza kwenye barafu, kwani kingeweza kumtegemeza kwa miezi kadhaa katika Jamhuri ya Dominika!”

Bidii ya Davey iliwachochea wengine. Kijana mmoja kutoka kwao alisema hivi: “Niliposikia yale ambayo Davey alikuwa anafanya na furaha aliyokuwa nayo, nilitambua kwamba mimi pia ninaweza kufanya mambo kama hayo. Kifo cha Davey kimenifanya nifikirie yale ambayo watu wangesema iwapo ningekufa na ikiwa maisha yangu yanaweza kuwachochea watu jinsi hiyo.”

Kwa kuwa wazazi wa Davey na ndugu na dada zake wadogo ni Mashahidi wa Yehova, wanasadiki kwamba hivi karibuni Mungu atamfufua Davey katika dunia mpya yenye uadilifu. (Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:1-4) Kwa sasa, wanafarijiwa kujua kwamba Davey alitumia maisha yake kwa njia bora kabisa kumtumikia Muumba wake. (Mhubiri 12:1) Wakati mmoja, Davey alisema hivi kuhusu uamuzi wake wa kutumikia mahali ambapo pana uhitaji mkubwa: “Laiti vijana wote wangefanya jambo kama hilo na kupata uradhi. Hakuna jambo bora kuliko kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Laiti wangejua!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kama vile David, Mashahidi wengi wa Yehova wamejitolea kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, na hata baadhi yao wamejifunza lugha ya kigeni ili wawafundishe wengine kweli za Neno la Mungu. Zaidi ya Mashahidi 400 wamejitolea kuhamia katika Jamhuri ya Dominika.