Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kutamani Makuu?

Je, Ni Vibaya Kutamani Makuu?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Vibaya Kutamani Makuu?

“KUNA ubaya gani kupata umashuhuri, utajiri, na mamlaka?” Swali hilo lilichapishwa katika ripoti moja ya shirika fulani la kidini chini ya kichwa, “Masuala ya Kiadili Yenye Kutatanisha.” Ripoti hiyo ilirejelea maneno haya ambayo Mungu alimwambia Abrahamu: “Nitafanya taifa kubwa kutokana nawe, nitakubariki na kulifanya jina lako kuwa kuu.”—Mwanzo 12:2.

Ingawa ilitaja kwamba “mtu hapaswi kutamani makuu kwa kuwadhuru wengine,” ripoti hiyo ilimnukuu rabi mashuhuri wa karne ya kwanza, aliyesema hivi: “Nisipojitukuza, ni nani atakayenitukuza?” kisha akamalizia kusema: “Tusipotambua na kutumia uwezo tulio nao, hakuna mtu atakayeutambua.” Je, kutamani makuu kunaweza kutokeza tatizo kwa wale wanaotaka kumtumikia Mungu? Ni nini kinachohusika katika kutambua na kutumia uwezo wetu? Je, ni vibaya kutamani makuu? Biblia ina maoni gani?

Je, Abrahamu Alitamani Makuu?

Biblia inamtaja Abrahamu kuwa mtu mwenye imani yenye kutokeza. (Waebrania 11:8, 17) Mungu hakuwa akimtia moyo Abrahamu atamani makuu alipomwahidi kwamba angetokeza taifa kubwa kutoka kwake na kufanya jina lake liwe kuu. Mungu alikuwa anataja kusudi lake la kuwabariki wanadamu kupitia Abrahamu, kusudi ambalo lilikuwa muhimu zaidi kuliko tamaa ya makuu ya wanadamu.—Wagalatia 3:14.

Katika kujitoa kwa Mungu, Abrahamu aliacha maisha yaliyoonekana kuwa yenye ufanisi huko Uru. (Mwanzo 11:31) Baadaye, ili kudumisha amani, Abrahamu alimwambia mpwa wake Loti achague sehemu bora zaidi ya nchi licha ya kwamba Abrahamu ndiye aliyekuwa na mamlaka na uwezo. (Mwanzo 13:8, 9) Biblia haitaji jambo lolote linaloonyesha kwamba Abrahamu alitamani makuu. Badala yake, imani, utii, na unyenyekevu wake ndio uliofanya Mungu apendezwe naye kama “rafiki” wa kweli.—Isaya 41:8.

Maoni Tofauti Kuhusu Cheo, Umashuhuri, na Mamlaka

Kutamani makuu kumefafanuliwa kuwa “tamaa kubwa ya kupata cheo, umashuhuri, au mamlaka.” Nyakati za kale, Mfalme Sulemani alikuwa na cheo, umashuhuri, mamlaka pamoja na mali nyingi. (Mhubiri 2:3-9) Hata hivyo, jambo la kupendeza ni kwamba mwanzoni yeye hakuwa na tamaa ya mambo hayo. Sulemani aliporithi kiti cha ufalme, Mungu alimwambia aombe chochote alichotaka. Kwa unyenyekevu, Sulemani aliomba moyo mtiifu na utambuzi uliohitajiwa ili kuwatawala watu wa Mungu waliochaguliwa. (1 Wafalme 3:5-9) Baadaye, akizungumzia kiasi cha mali na mamlaka aliyopata, Sulemani alisema kwamba “kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:11.

Je, Sulemani alisema chochote kuhusu wanadamu kutumia uwezo wao? Alisema hivyo kwa njia fulani. Baada ya kuchunguza mambo mengi yaliyompata maishani, alikata kauli hivi: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.” (Mhubiri 12:13) Wanadamu hutumia uwezo wao kwa kufanya mapenzi ya Mungu bali si kupata cheo, utajiri, umashuhuri, au mamlaka.

Unyenyekevu Hufanya Mtu Ainuliwe

Ni kweli kwamba, hakuna ubaya wowote kujipenda kwa kiasi. Biblia hutuamuru tupende jirani yetu kama sisi wenyewe. (Mathayo 22:39) Ni jambo la kawaida kutamani starehe na furaha. Lakini Biblia pia hututia moyo tufanye kazi kwa bidii, tuwe wanyenyekevu na wenye kiasi. (Methali 15:33; Mhubiri 3:13; Mika 6:8) Mara nyingi, watu wanyoofu na wenye kutegemeka na ambao hufanya kazi kwa bidii hutambuliwa, hupata kazi nzuri, na kuheshimiwa. Bila shaka, ni afadhali kuwa na sifa hizo badala ya kuwatumia wengine vibaya kwa faida yetu au kushindana na wengine ili kupata mamlaka.

Yesu aliwaonya wasikilizaji wake kuhusu kujichagulia viti vya mbele kwenye karamu ya ndoa. Aliwashauri waketi mahali pa chini zaidi na kungoja hadi mtu aliyewaalika aamue kuwahamisha hadi mahali penye kuonekana. Akitaja waziwazi kanuni inayohusika, Yesu alisema: “Kila mtu anayejiinua atanyenyekezwa na yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Luka 14:7-11.

Wakristo wa Kweli Huepuka Tamaa ya Makuu

Biblia inaonyesha kwamba kutamani makuu kwa kiburi huhusianishwa na kutokamilika kwa kibinadamu. (Yakobo 4:5, 6) Pindi moja, mtume Yohana alitamani makuu. Alitamani sana cheo hivi kwamba yeye pamoja na ndugu yake, walimwuliza Yesu kwa ujasiri awape cheo kikubwa katika Ufalme. (Marko 10:37) Baadaye, Yohana alibadili mtazamo wake. Kwa kweli, katika barua yake ya tatu, alimkaripia Diotrefe, na kusema kwamba ‘anapenda kuwa na mahali pa kwanza.’ (3 Yohana 9, 10) Leo Wakristo hutii maneno ya Yesu na kujinyenyekeza, huku wakifuata kielelezo cha mtume Yohana mzee, ambaye alijifunza kuepuka tamaa ya makuu.

Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba vipawa, uwezo, matendo mazuri, na kufanya kazi kwa bidii si uhakikisho wa kwamba mtu atakuwa mashuhuri. Nyakati nyingine watu kama hao huthawabishwa na wanadamu wenzao, na nyakati nyingine hawathawabishwi. (Methali 22:29; Mhubiri 10:7) Nyakati nyingine, huenda watu ambao hawastahili sana wakapewa vyeo vyenye mamlaka, huku watu wenye uwezo wakipuuzwa. Katika ulimwengu huu usio mkamilifu, watu ambao hupata vyeo na mamlaka huenda wakawa hawastahili.

Kwa Wakristo wa kweli kutamani makuu hakutokezi masuala ya kiadili yenye kutatanisha. Dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia huwasaidia kuepuka tamaa ya makuu. Wao hujitahidi kufanya mema katika hali zote kadiri wawezavyo, kwa utukufu wa Mungu, na kuacha mambo mikononi mwake. (1 Wakorintho 10:31) Wakristo hujitahidi kutumia uwezo wao kwa kumwogopa Mungu na kushika amri zake.

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Je, Mungu alimtia moyo Abrahamu atamani makuu?