Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Watoto Huvutiwa na Muziki

Jarida Scientific American linasema hivi: “Hata kabla watoto hawajajifunza kuzungumza, wao huwa na uwezo wa kuvutiwa na muziki.” Kulingana na ripoti hiyo, watoto wanaweza kutambua muziki mbalimbali na mdundo unapobadilika. Pia wanaweza kutambua muziki mwororo hata unapochezwa kwa njia tofauti. Watoto wachanga wenye umri wa miezi miwili hupendelea muziki wenye upatano kuliko sauti zisizopatana. Ripoti hiyo inasema, “Peter Hepper wa Chuo Kikuu cha Queen, huko Belfast aligundua kwamba majuma mawili hivi kabla ya kuzaliwa, vijusi vilitofautisha muziki wa kipindi fulani [maarufu] cha televisheni ambao mama zao walisikiliza kwa majuma mengi na muziki ambao hawajawahi kuusikia.”

Amani Ndani ya Gari Huzuia Aksidenti

Gazeti Berliner Morgenpost linaripoti kwamba shirika la Ujerumani linalosimamia mambo ya kiufundi la TÜV linaonya hivi: “Watu walio ndani ya gari wanapaswa kuepuka mabishano kabisa. Bila kutambua dereva huanza kuendesha gari vibaya na hivyo kuongeza uwezekano wa kupata aksidenti.” Gazeti hilo linasema kwamba “ugomvi” unapotokea ndani ya gari unaweza kuwa mbaya sana, hasa kwa sababu hakuna mahali pa kuuondokea. Kwa hiyo, inapendekezwa kwamba watu walio ndani ya gari waepuke mazungumzo yanayoweza kutokeza mabishano. Wote ndani ya gari wanapaswa kushirikiana ili kutimiza lengo moja. Makala hiyo inashauri hivi: “Kabla ya kuanza safari, inapaswa kuamuliwa jinsi yule atakayeketi karibu na dereva atakavyomsaidia kwa kumwonyesha njia, kubadili kituo cha redio, au kushughulikia matatizo yanayotokea.”

Bahari Nyeusi Inarudia Hali Yake

Gazeti la Ukrainia, Demokratychna Ukraina linasema kwamba sasa Bahari Nyeusi ina pomboo, kaa, na uduvi wengi zaidi kuliko ilivyokuwa awali. Kwa kawaida viumbe hao hawaishi katika maji yaliyochafuliwa. Hata katika bandari ya Odessa, ambayo kwa kawaida huonwa kuwa sehemu iliyochafuliwa zaidi katika Bahari Nyeusi, farasi-maji wameongezeka sana. Borys Aleksandrov, msimamizi wa tawi la Odessa la Taasisi ya Biolojia ya Bahari za Kusini alisema hivi: “Mimea na wanyama wanaoishi katika Bahari Nyeusi na Bahari Azov wanaanza kuongezeka polepole baada ya kupungua kwa muda mrefu.” Kwa nini wanaongezeka? Gazeti Science News linasema: “Baada ya kuanguka kwa Ukomunisti, matatizo ya kiuchumi huko Urusi, Ukrainia, Moldova, Rumania, na Bulgaria yalipunguza sana matumizi ya mbolea katika kilimo. Kwa hiyo, maji ya mvua yenye mbolea ambayo huelekea kwenye Bahari Nyeusi yalipungua sana katika miaka ya 1990.” Gazeti Science News linasema kwamba ingawa kupungua kwa matumizi ya mbolea kumeifaidi Bahari Nyeusi, “kuanguka kwa uchumi au kupungua kwa kilimo ni mbinu isiyofaa ya kurekebisha sehemu za [bahari] ambazo hazina viumbe hai.” Laurence Mee, profesa wa utunzaji wa maeneo ya pwani na viumbe wa baharini wa Chuo Kikuu cha Plymouth, Uingereza anapendekeza mbinu nyingine. Anasema: “Tunapaswa kuwa na ujuzi zaidi kuhusu jinsi tunavyolima, ili tupunguze maji yenye mbolea yanayoingia baharini.”

Kunyunyizia Mashamba Maji Machafu

Gazeti Der Standard, la Austria, linaripoti hivi: “Sehemu moja ya kumi ya mimea yote inayotokeza faida ya kiuchumi ulimwenguni hukuzwa kwa kutumia maji machafu.” Mimea kama vile nyanya na nazi inakuzwa kwa njia hiyo. Gazeti hilo linasema: “Maji hayo hayajasafishwa, nayo hutiririka moja kwa moja kutoka kwenye majiji makubwa sana na kuingia kwenye mfumo wa kunyunyizia maji.” Chris Scott, wa Taasisi ya Kimataifa ya Usimamizi wa Maji huko Sri Lanka, anaeleza hivi: “Katika maeneo mengi yaliyo karibu na majiji makubwa sana yanayokua haraka, hiyo ndiyo njia pekee ya kukabiliana na ukosefu wa maji.” Ripoti hiyo inasema kwamba katika ekari milioni 50 hivi za mashamba ulimwenguni, wakulima hawana njia nyingine ila kutumia maji machafu ambayo huwapa mbolea ya bure na pia maji hayo hupatikana kwa urahisi.

Biashara ya Kuuza Watu

Toleo la kimataifa la gazeti The Miami Herald linaripoti kwamba, “biashara ya kuuza watu imekuwa chanzo kikubwa cha tatu cha kupata pesa kwa vikundi vya wahalifu baada ya biashara ya dawa za kulevya na silaha, kwani inakadiriwa kwamba inaleta dola bilioni 6 hadi bilioni 9 kwa mwaka.” Katika mkutano wa waandishi-habari uliofanywa hivi karibuni huko Mexico City, John Miller, mkurugenzi wa Idara ya Kusimamia na Kuzuia Uuzaji wa Watu katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, aliwaambia ripota kwamba watu 17,500 hivi huuzwa na kupelekwa Marekani kila mwaka, thuluthi ya watu hao hutoka au hupitia Mexico. Miller alisema: “Sizungumzi kuhusu watu wanaohamia Marekani isivyo halali, bali kuhusu wanaume, wanawake, na watoto wanaolazimishwa na watu wengine kuwa katika hali ya utumwa.” Alitaja uuzaji wa watu ili kuwatumia vibaya kingono na kuwalazimisha kufanya kazi kuwa “mojawapo ya masuala ya msingi ya haki za wanadamu katika karne ya 21.”

Jua na Wanawake Waja-Wazito

Gazeti Sun-Herald la Australia linaripoti hivi: “Uchunguzi wa kiwango cha vitamini D katika wanawake waja-wazito unaonyesha kwamba wanawake wengi hawana vitamini D ya kutosha na hivyo wanahatarisha afya ya watoto walio tumboni.” Watoto ambao hawana vitamini D ya kutosha huenda wakapatwa na ugonjwa wa mifupa wa matege na ugonjwa wa kifafa. Uchunguzi uliofanyiwa wanawake waja-wazito 1,000 katika hospitali ya St. George huko Sydney, ulionyesha kwamba “mwanamke mmoja kati ya kumi wenye ngozi nyeupe na mmoja kati ya watano wenye ngozi nyeusi hawana vitamini D ya kutosha.” Suluhisho la tatizo hilo ni rahisi. Wanadamu hutokeza asilimia 90 hivi ya vitamini D wanayohitaji kwa kuota jua wakati ambapo si kali. Gazeti hilo linasema: “Wanawake wengi [wanahitaji] kuota jua kwa muda wa dakika 10 tu kwa siku ama angalau saa moja kwa juma ili kupata vitamini D ya kutosha.”

Wanawake Wanaokuwa Wagonjwa kwa Kufanya Mazoezi Kupita Kiasi

Gazeti Folha, la Brazili liliripoti kwamba wanawake wanaofanya mazoezi magumu kupita kiasi kwa ukawaida wanaweza kupatwa na ugonjwa wa mifupa, matatizo ya kula, na kutopata hedhi. Turíbio Leite de Barros Neto, mratibu wa Kituo cha Mazoezi na Dawa za Michezo katika Chuo Kikuu cha São Paulo, alisema: “Kwa kufaa, mwanamke anapaswa kuwa na asilimia 10 zaidi ya mafuta ya mwili kuliko mwanamume. Yaani, hapaswi kuwa na chini ya asilimia 15 ya mafuta ya mwili.” Gazeti Folha, lilisema kwamba mwanamke akiwa na mafuta yanayopungua kiwango hicho, huenda ikawa vigumu kwa mwili wake kutokeza homoni zinazohitajika ili kudhibiti hedhi na kalisi iliyo mifupani mwake inaweza kupungua na hivyo apatwe na ugonjwa wa mifupa.