Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Furaha ya Kweli!

Unaweza Kupata Furaha ya Kweli!

Unaweza Kupata Furaha ya Kweli!

WATU wengi ulimwenguni pote wanaamini kwamba ili mtu awe na furaha anahitaji gari zuri, akaunti nono ya benki, kazi nzuri, nyumba kubwa, na vifaa vya kisasa vya elektroniki, pamoja na sura au umbo zuri. Lakini, je, furaha inategemea kuwa na vitu hivyo vya kimwili?

Ripoti moja ya pekee katika gazeti Time inasema kwamba “utafiti mwingi sana umefanywa kuhusu furaha, kutazamia mema, na sifa zinazochangia maadili mema, afya nzuri ya kimwili na kiakili.” Wengi wameshangazwa na matokeo ya utafiti huo. Uthibitisho unaonyesha kwamba watu wanaofikiri kwamba watakuwa wenye furaha kwa kuwa na pesa, umashuhuri, au urembo wanajidanganya wenyewe. Kwa kweli, wanategemeza maisha yao juu ya mambo ambayo huenda yakadhuru afya yao ya kiakili na hata kufanya washuke moyo.

Watu wengi nchini Marekani ni matajiri zaidi kuliko wakati mwingine wowote. “Lakini hilo halijafanya tuwe wenye furaha zaidi,” linasema gazeti Time. Hali iko hivyo katika nchi nyingine. Licha ya ukuzi wa haraka wa kiuchumi nchini China, kumekuwa na watu wengi zaidi wasio na furaha. Gazeti Access Asia linalochapishwa mara nne kwa mwaka linasema kwamba nchini humo, kujiua kumekuwa “kisababishi kikubwa zaidi cha vifo kati ya watu wenye umri wa miaka 15 na 34.” Sababu moja inayochangia jambo hilo ni mikazo ambayo vijana wanakabili wanapojaribu kupata mafanikio katika mazingira ya kazi yenye ushindani mwingi.

Ni wazi kwamba kuwa na mali hakupunguzi mahangaiko na mfadhaiko; badala yake kunaongeza mambo hayo. Uchunguzi mmoja wa chuo kikuu unaonyesha kwamba, “Mtindo wetu wa maisha sasa umekuwa chanzo kikuu cha mahangaiko ya kihisia na kiakili.” Mchanganuzi wa mambo ya kijamii Van Wishard anasema kwamba “kampuni nyingi hutumia bima ya afya kulipia hasa matibabu ya kiakili na kihisia.”

Hata watoto wanaathiriwa na ulimwengu huu unaobadilika haraka-haraka. Sasa kuna vitabu vya watoto wenye umri wa miaka minane vinavyowashauri kuhusu “jinsi ya kutambua dalili za mfadhaiko na jinsi ya kukabiliana nao,” anasema Wishard. Na kulingana na orodha moja kuhusu kushuka moyo, katika nchi kadhaa za Magharibi, idadi ya watoto walio na mshuko-moyo inaongezeka kwa asilimia 23 kwa mwaka. Isitoshe “watoto ambao hawajaanza kwenda shule ndio wanaotumia zaidi dawa za kukabiliana na mshuko-moyo.”

Pia woga unaongezeka, na si woga unaosababishwa tu na mahangaiko ya kiuchumi. Huku ushupavu wa kisiasa na wa kidini ukiongezeka, watu wengi wanaogopa mambo mabaya ambayo huenda yakatokea wakati ujao. Je, kuna msaada wowote?

Karibu miaka elfu mbili iliyopita, Yesu Kristo alifundisha njia ya maisha ambayo huburudisha na kupunguza mfadhaiko. Ukweli aliofundisha ulikuwa rahisi lakini wenye nguvu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Naam, Yesu aliwatia moyo wasikilizaji wake wakazie fikira uhitaji mkubwa zaidi wa wanadamu, yaani, kweli ya kiroho kuhusu Muumba wetu na kusudi Lake kutuelekea.

Kama tutakavyoona katika makala zinazofuata, kweli hiyo inaweza kutusaidia kutambua mambo muhimu zaidi, na hivyo kufanya tuwe na maisha yenye furaha na yenye kusudi. Pia ukweli huo wa kiroho hutupa tumaini zuri ajabu.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Je, furaha inategemea kuwa na vitu vya kimwili?