Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Wakati Gani Urafiki Shuleni Huvuka Mipaka?

Ni Wakati Gani Urafiki Shuleni Huvuka Mipaka?

Vijana Huuliza . . .

Ni Wakati Gani Urafiki Shuleni Huvuka Mipaka?

“Niliwasikia watoto shuleni wakisimulia jinsi walivyofurahia mwisho-juma wakiwa pamoja. Nilijihisi mpweke.”—Michelle. *

“Nyakati nyingine mimi hutazama kikundi cha watoto na kujiambia, ‘wanaonekana kuwa marafiki sana. Nataka kuwa rafiki yao pia.’”—Joe.

“Ilikuwa rahisi sana kwangu kuanzisha urafiki shuleni na hilo liliniletea matatizo.”—Maria.

WEWE huwa pamoja na wanashule wenzako mchana kutwa. Unakabili magumu, mfadhaiko, na kupata mafanikio yaleyale kama wao. Kwa njia fulani, huenda ukahisi kwamba una mapendezi sawa na wanashule wenzako kuliko na wazazi, ndugu na dada zako, au Wakristo wenzako. Inaeleweka kwamba huenda ukavutiwa kufanya urafiki nao. Je, kuna ubaya wowote kufanya hivyo? Je, kuna hatari zozote? Ni wakati gani urafiki shuleni huvuka mipaka? Unaweza kuweka mipaka gani?

Unahitaji Marafiki

Kila mtu anahitaji marafiki, yaani, watu ambao anaweza kustarehe nao hali ikiwa nzuri na kuwategemea katika hali mbaya. Yesu alikuwa na marafiki, naye alifurahia kushirikiana nao. (Yohana 15:15) Yesu alipokuwa anakaribia kufa kwenye mti wa mateso, Yohana, rafiki yake wa karibu, ‘mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda sana,’ alikuwa amesimama karibu. (Yohana 19:25-27; 21:20) Unahitaji marafiki kama Yohana ambao watakuwa pamoja nawe kwa heri na shari. Methali moja ya Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Pengine unahisi kwamba umempata rafiki kama huyo shuleni, mmoja wa wanadarasa wenzako ambaye urafiki wenu ni wa chanda na pete. Mna mapendezi yaleyale, nanyi hufurahia kuzungumza pamoja. Ni kweli kwamba huenda rafiki huyo asiwe mwabudu mwenzako; lakini kwa maoni yako, yeye haonekani kuwa “mashirika mabaya.” (1 Wakorintho 15:33) Ni kweli kwamba vijana wengine ambao hawana imani kama yako inayotegemea Biblia hufuata viwango safi. (Waroma 2:14, 15) Lakini je, hilo linamaanisha kwamba usitawishe urafiki wa karibu nao?

Wakristo Hawajitengi na Watu

Bila shaka Wakristo wa kweli hawajitengi na watu ambao si waamini. Ili watimize mgawo wao wa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ Wakristo huzungumza na wanaume na wanawake kutoka kila jamii, dini, na utamaduni. (Mathayo 28:19) Wao hawajitengi na majirani, wafanyakazi, au wanashule wenzao. Badala yake, Wakristo hupendezwa kikweli na wengine.

Mtume Paulo alituwekea mfano mzuri. Alijua jinsi ya kuzungumza na “watu wa namna zote,” hata ingawa walikuwa na imani tofauti na yake. Bila shaka, kusudi la Paulo halikuwa kushirikiana nao. Badala yake, alisema: “Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.”—1 Wakorintho 9:22, 23.

Unaweza kufuata mfano wa Paulo. Waonyeshe marika wako urafiki. Jifunze kuwasiliana nao vizuri. Huenda baadhi ya wanashule wenzako wakataka kuwa na tumaini linalotajwa katika Biblia kama wewe. Fikiria kisa cha Janet, msichana Mkristo. Yeye na wanadarasa wenzake walipewa mgawo wa kuandika maneno machache kuhusu wanafunzi wengine, kisha kila mmoja wao alisoma yale ambayo wanafunzi wengine waliandika kumhusu. Janet alipokea karatasi moja iliyosema: “Wewe huonekana kuwa mwenye furaha sana nyakati zote. Tafadhali tueleze sababu inayokufanya uwe hivyo!”

Kama kisa hicho kinavyoonyesha, huenda baadhi ya wanadarasa wenzako wakataka kujua mambo unayoamini. Kwa hiyo, ni jambo linalofaa kuwaonyesha urafiki. Bila shaka kufanya hivyo kutakupa nafasi ya kuwaeleza mambo unayoamini. Waruhusu wanadarasa wenzako waeleze maoni yao pia, na uwasikilize kwa makini. Ujuzi wa kuwasiliana unaopata shuleni utakusaidia utakapoanza kufanya kazi na kukabiliana na hali kama hizo. Kuwa mwenye urafiki shuleni na kazini kutakusaidia ‘kulipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.’—Tito 2:10.

Urafiki Usiofaa

Bila shaka kuna tofauti kati ya kuwa mwenye urafiki kuelekea mwanadarasa mwenzako na kuwa na urafiki wa karibu naye. Paulo aliandika hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Ili uwe na urafiki wa karibu na mtu fulani, ni lazima nyote wawili muwe na viwango na miradi ileile. Hilo haliwezekani ikiwa mtu huyo hafuati mafundisho na viwango vya Biblia kama wewe. Huenda kufungwa nira isivyo sawa na mwanadarasa asiyeamini kukakufanya ujihusishe na mazoea mabaya au kuharibu tabia zako nzuri.

Maria alijifunza jambo hilo baada ya kupatwa na hali ngumu. Kwa kuwa alikuwa mwenye urafiki, alipata marafiki kwa urahisi lakini hakujua jinsi ya kuweka mipaka. Anasema hivi: “Nilifurahia kupendwa na wote, wasichana na wavulana. Kwa sababu hiyo nilijikuta nikizama kwenye matatizo ambayo singeweza kujitoa.”

Kama Maria, huenda ikawa vigumu kwako kutambua wakati urafiki na mtu mwingine ambaye ana imani tofauti na yako umepita mipaka. Hata hivyo, unaweza kujilinda usipatwe na maumivu ya kihisia kwa kuweka mipaka iliyo wazi kuhusu mtu ambaye utafahamiana naye kijuu-juu tu na yule utakayechagua awe rafiki yako wa karibu. Unaweza kufanyaje hivyo?

Jinsi ya Kuchagua Marafiki Wazuri

Kama ilivyotajwa awali, Yesu alikuwa na marafiki wa karibu alipokuwa hapa duniani. Aliwapata kwa kuishi maisha manyoofu na kwa kuzungumza kuhusu mambo ya kiroho. Watu walipokubali mafundisho yake na kuishi kama yeye, walikuwa na uhusiano wa karibu naye. (Yohana 15:14) Kwa mfano, baada ya kumsikiliza Yesu, wanaume wanne walichochewa sana hivi kwamba ‘waliacha kila kitu, wakamfuata.’ Wanaume hao, Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana wakawa marafiki wa karibu wa Yesu.—Luka 5:1-11; Mathayo 4:18-22.

Maneno na matendo ya Yesu yalionyesha wazi kwamba alishikilia kwa dhati mambo aliyoamini na hangebadili msimamo wake kamwe. Wale ambao hawakutaka kumkubali Yesu na mafundisho yake walimwacha, naye Yesu aliwaacha waende zao.—Yohana 6:60-66.

Kwa mfano, Yesu aliguswa moyo sana na unyoofu wa mwanamume mmoja kijana. Biblia inasema: ‘Yesu alimtazama akampenda.’ Lakini mwanamume huyo alipojua mambo ambayo Yesu alitazamia kutoka kwa marafiki wake, ‘alienda zake.’ Mwanamume huyo alionekana kuwa mtu mzuri, na bila shaka ‘Yesu alimpenda.’ Hata hivyo, Yesu alitazamia mengi zaidi kutoka kwa marafiki wake. (Marko 10:17-22; Mathayo 19:16-22) Vipi wewe?

Huenda ukawa na uhusiano mzuri na mwanashule mwenzako. Hata hivyo, jiulize: ‘Je, mtu huyo yuko tayari kufanya yale ambayo Yesu anaagiza? Je, yeye anataka kujifunza kumhusu Yehova, yule ambaye Yesu alituagiza tumwabudu?’ (Mathayo 4:10) Majibu ya maswali hayo yataonekana wazi unapozungumza na wanadarasa wenzako na kuishi kulingana na viwango vya Biblia.

Inafaa kuwa mwenye urafiki kuelekea wanadarasa wenzako, kama vile tu Yesu alivyokuwa mwenye urafiki kuelekea watu wa namna zote. Lakini Yesu alihakikisha kwamba marafiki wake wa karibu walimpenda Yehova, Baba yake wa mbinguni. Unaweza kufanya vivyo hivyo. ‘Dumisha mwenendo wako ukiwa mzuri’ shuleni, na uwe na busara unapozungumza na wengine kuhusu imani yako. Zaidi ya hayo, hakikisha kwamba unachagua marafiki wazuri.—1 Petro 2:12.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kuna hatari gani kutumia wakati wako wa ziada baada ya shule na mwanadarasa ambaye si mwamini? Je, hilo ni jambo la hekima?

▪ Baada ya kusoma makala hii, je, unahisi kwamba uhusiano wako na mwanadarasa mwenzako umepita mipaka? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina fulani yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

How Can I Make Real Friends?

Video hii ambayo imetolewa na Mashahidi wa Yehova, inaonyesha vijana kutoka Marekani, Italia, Ufaransa, na Hispania wakihojiwa na kueleza waziwazi maoni yao. Inapatikana katika lugha 36.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Huenda baadhi ya wanadarasa wenzako wakataka kujua mambo unayoamini