Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilijifunza Kumtegemea Mungu

Nilijifunza Kumtegemea Mungu

Nilijifunza Kumtegemea Mungu

SIMULIZI LA ELLA TOOM

FAMILIA yetu iliishi karibu na mji mdogo wa Otepää, kusini mwa Estonia, kilometa 60 hivi kutoka mpaka wa Urusi. Mnamo Oktoba 1944, miezi michache baada ya kumaliza masomo ya sekondari, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa karibu kwisha. Jeshi la Urusi lilipowafukuzia Wajerumani kupitia Estonia, sisi na majirani wetu, tukiwa watu 20 hivi, tulijificha msituni pamoja na mifugo yetu.

Kwa miezi miwili mabomu yalipokuwa yakianguka kila mahali, tulikuwa karibu na eneo la vita. Tungeketi karibukaribu nami ningesoma sehemu fulani za Biblia, hasa kutoka kitabu cha Maombolezo. Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kusoma Biblia. Siku moja nilipanda mlima mrefu, nikapiga magoti, na kusali, “Vita vitakapokwisha, ninaahidi kwamba nitaenda kanisani kila Jumapili.”

Baada ya muda mfupi vita vilielekea upande wa magharibi. Mwishowe, Ujerumani iliposalimu amri mnamo Mei 1945, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikwisha huko Ulaya. Nilitimiza ahadi yangu kwa Mungu na nikaenda kanisani kila juma. Lakini ni wanawake wachache tu wenye umri mkubwa waliohudhuria. Niliona haya kuwa hapo. Mtu alipopitia kwetu kututembelea, nilificha Biblia chini ya meza.

Punde si punde, nilipata kazi ya ualimu katika shule moja karibu na kwetu. Kufikia wakati huo milki ya Wakomunisti ilikuwa ikitawala na watu wengi waliamini kwamba hakuna Mungu. Hata hivyo, nilikataa kujiunga na Chama cha Kikomunisti. Nilifanya mambo mengi ya kijamii kama vile, kupanga tamasha za dansi za kitamaduni za watoto.

Jinsi Nilivyokutana na Mashahidi

Watoto walihitaji mavazi ya kuigiza, hivyo mnamo Aprili 1945, nilienda kumwona Emilie Sannamees, ambaye ni mshonaji stadi. Kumbe alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova! Aliuliza, “Wewe una maoni gani kuhusu hali za ulimwengu?” Kwa kuwa kulikuwa na mkutano kuhusu amani huko San Francisco, Marekani, nilisema, “Hivi karibuni serikali hii itakoma, nami nina hakika kwamba mkutano unaoendelea kuhusu amani unafanywa ili kuhakikisha kwamba itakoma.”

Emilie alisema kwamba mkutano huo kuhusu amani hautaleta manufaa ya kudumu naye akajitolea kunionyesha sababu kutoka katika Biblia. Wakati huo sikutaka kumsikiliza mwanamke huyo mpole, mwenye umri wa makamo, hivyo aliniuliza swali, “Je, unajua mahali ambapo Mungu alitaka Adamu na Hawa waishi?” Kwa kuwa sikuweza kumjibu, aliniambia tu, “Mwulize baba yako.”

Nilifanya hivyo niliporudi nyumbani. Baba hakuweza kujibu naye akaniambia kwamba hatuhitaji kujihangaisha na kujifunza Biblia; tulihitaji tu kuamini. Niliporudi kuchukua mavazi hayo, nilimwambia kwamba Baba hakujua jibu la swali lake. Yeye na dada yake walitoa Biblia zao na kunisomea maagizo ambayo Mungu aliwapa Adamu na Hawa, kuhusu kutunza bustani iliyokuwa makao yao na kuishi humo kwa furaha milele. Walinionyesha kutoka katika Biblia kwamba Mungu alikusudia Adamu na Hawa wazae watoto na kupanua makao yao ya Paradiso yaenee ulimwenguni kote. Nilistaajabishwa na uthibitisho huo wa Kimaandiko!−Mwanzo 1:28; 2:8, 9, 15; Zaburi 37:29; Isaya 45:18; Ufunuo 21:3, 4.

Mkutano Wangu wa Kwanza wa Kikristo

Kwa kuwa ningehudhuria mtaala wa miezi mitatu wa ualimu huko Tartu, Emilie alinieleza mahali ambapo Shahidi fulani alikuwa akiishi katika jiji hilo. Pia alinipa kitabu Creation, ambacho kilinipendeza kwa sababu ya maelezo yake ya wazi kuhusu kweli za Biblia. Kwa hiyo, Agosti 4, 1945, nilienda kwenye nyumba niliyokuwa nimeelekezwa.

Nilibisha mlango lakini sikufunguliwa, hivyo nilibisha tena kwa nguvu sana hivi kwamba jirani alifungua mlango wake na kunielekeza mahali pengine. Alinielekeza kwenye Barabara ya Salme 56. Hapo nilimwuliza mwanamke aliyekuwa akimenya viazi katika kibanda, “Je, kuna mkutano wa kidini unaofanywa hapa?” Kwa hasira aliniambia niondoke na kwamba sikutakikana hapo. Lakini niliposisitiza, nilialikwa kwenye chumba cha juu ili nijiunge na kikundi kilichokuwa kikijifunza Biblia. Baada ya muda mfupi kulikuwa na mapumziko kwa ajili ya chakula cha mchana nami nilitaka kuondoka. Lakini wengine walisisitiza nisiondoke.

Wakati wa mapumziko ya mchana, niliona vijana wawili wa kiume, waliokuwa wembamba sana, wakiwa wameketi karibu na dirisha. Baadaye niliambiwa kwamba wakati wa vita walijificha mahali mbalimbali kwa zaidi ya mwaka mmoja ili wasikamatwe. * Wakati wa kipindi cha alasiri, Friedrich Altpere alitumia neno “Har–Magedoni” katika hotuba yake. Kwa kuwa sikufahamu neno hilo, nilimwuliza maana yake baadaye, naye akanionyesha katika Biblia. (Ufunuo 16:16) Alishangaa kwamba neno hilo lilikuwa jipya kwangu.

Niligundua kwamba mkutano huo ulikuwa umepangiwa Mashahidi wanaojulikana na kutumainika peke yao. Baadaye nilifahamu kwamba ulikuwa mkutano wao wa kwanza baada ya vita! Kuanzia wakati huo, nilitambua kabisa uhitaji wa kumtegemea Mungu. (Methali 3:5, 6) Mwaka mmoja baadaye, mnamo Agosti 1946, nikiwa na umri wa miaka 20, nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu wa kweli, Yehova.

Kukabiliana na Upinzani wa Familia

Serikali ilisisitiza kwamba watoto wafundishwe shuleni kuwa hakuna Mungu. Jambo hilo lilitahini dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia. Nilitaka kubadili kazi yangu. Nilipomwambia Mama jambo hilo, alinishambulia kwa hasira, na kung’oa nywele zangu kadhaa. Niliamua kuondoka nyumbani. Lakini Baba alinitia moyo nivumilie, akisema kwamba angenisaidia.

Ndugu yangu Ants aliungana na Mama kunipinga. Kisha siku moja aliniomba vichapo fulani, ambavyo alisoma na kupendezwa navyo sana. Mama alikasirika sana. Hata Ants alianza kuwaeleza wengine shuleni kumhusu Mungu, lakini alipokabili upinzani, aliacha kushirikiana na Mashahidi. Muda fulani baadaye, alijeruhiwa kichwani alipokuwa akipiga mbizi. Alipooza mwili wote lakini akili yake ilikuwa sawa. Akiwa amelala kitandani aliniuliza, “Je, Yehova atanisamehe?” “Ndiyo,” nikamjibu. Ants alikufa siku chache baada ya hapo. Alikuwa na umri wa miaka 17 tu.

Mnamo Septemba 1947, niliacha kufanya kazi shuleni. Bado Mama alikuwa mkali kunielekea. Alipotupa nguo zangu zote nje ya nyumba, niliondoka na kuanza kuishi na Emilie Sannamees na dada yake mkubwa. Walinitia moyo sana kwa kunikumbusha kwamba Yehova hawaachi kamwe watumishi wake.

Majaribu Huko Estonia Baada ya Vita

Emilie na dada yake waliniruhusu nifanye nao kazi ya kushonea nguo familia zilizoishi mashambani. Mara nyingi tungewaeleza kweli za Biblia. Nilifurahia sana kipindi hicho kwani sikujifunza tu kushona bali pia nilipata uzoefu zaidi katika huduma ya Kikristo. Zaidi ya kushona, nilipata pia kazi ya muda ya kufunza hesabu. Hata hivyo, mnamo 1948, serikali ilianza tena kuwakamata Mashahidi.

Mwaka uliofuata, katika mwezi wa Oktoba, nilikuwa nikifanya kazi katika shamba fulani nilipoambiwa kwamba askari walikuwa wameenda kwa akina Sannamees kunikamata. Nilipoenda shambani kwa Ndugu Hugo Susi kujificha, nilipata kwamba alikuwa amekamatwa. Mwanamke mmoja niliyekuwa nimemshonea nguo alinikaribisha nikae kwake. Baadaye niliishi katika mashamba mbalimbali nikishona na kuendelea kuhubiri.

Majira ya baridi kali yalipoanza, nilikuwa katika mji wa Tartu. Askari wa Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB) walinipata nyumbani mwa Linda Mettig, kijana Shahidi mwenye bidii aliyekuwa na umri mkubwa kidogo tu kuliko mimi. Nilikamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi ili nihojiwe. Maofisa wa polisi vijana walinilazimisha nivue nguo zangu zote nao wakanikodolea macho. Niliaibika sana. Hata hivyo, niliposali kwa Yehova, nilipata amani na moyo ukatulia kabisa.

Baada ya hapo, nilitiwa ndani ya seli ndogo ambapo hata singeweza kulala chini. Niliruhusiwa kutoka nje tu nilipoenda kuhojiwa. Maofisa waliniambia: “Hatusemi ukane kwamba kuna Mungu. Acha tu mahubiri yako ya kipumbavu! Unaweza kuwa na maisha mazuri.” Kisha wangenitisha hivi: “Je, unataka kuishi, au unataka kufa na Mungu wako huko Siberia?”

Kwa siku tatu ambazo nilihojiwa, sikuruhusiwa kulala. Kutafakari kanuni za Biblia kulinisaidia kuvumilia. Mwishowe, mmoja wa walionihoji aliniambia nitie sahihi hati iliyosema kwamba ningeacha kuhubiri. Nilisema: “Nimefikiria jambo hilo sana, na naona ni afadhali niendelee kuishi gerezani nikiwa na uhusiano mzuri na Mungu badala ya kuwa huru na kupoteza kibali chake.” Aliposikia hilo mtu huyo alisema hivi kwa sauti: “Mjinga wewe! Ninyi nyote mtakamatwa na kupelekwa Siberia!”

Kuwekwa Huru Bila Kutazamia

Kwa kushangaza, kabla tu ya saa sita usiku, waliokuwa wakinihoji waliniambia nichukue vitu vyangu na kuondoka. Kwa kuwa nilijua ningefuatwa, sikwenda nyumbani kwa ndugu zangu Wakristo kwani ningewasaliti. Kwa kweli, nilipokuwa nikitembea barabarani, wanaume watatu walinifuata. Baada ya kusali Yehova aniongoze, nilipita katika barabara yenye giza na kukimbia katika bustani. Nililala chini na kujifunika kwa majani. Ningeweza kusikia sauti ya miguu yao na kuona mwangaza wa tochi zao.

Baada ya saa kadhaa, mifupa yangu ilianza kufa ganzi kwa sababu ya baridi. Mwishowe, nilitembea kwenye barabara zilizojengwa kwa mawe nikiwa nimebeba viatu vyangu ili visipige kelele. Nilitoka jijini na kutembea ndani ya mtaro kando ya barabara kuu. Magari yalipokaribia, nililala chini. Saa kumi na moja alfajiri nilifika nyumbani kwa Jüri na Meeta Toomel, karibu na jiji la Tartu.

Mara moja Meeta alinitayarishia bafu ya mvuke ili nijipashe joto. Siku iliyofuata alienda katika jiji la Tartu na kuwasiliana na Linda Mettig. Linda aliniambia hivi, “Acha tuanze kuhubiri sasa ili tueneze habari njema kotekote Estonia.” Baada ya kubadili sura yangu kwa mtindo mpya wa nywele, vipodozi kidogo, na miwani, tulianza kuhubiri. Miezi iliyofuata, tulisafiri mbali sana kwa baiskeli. Tukiwa njiani tuliwatia moyo waamini wenzetu walioishi mashambani.

Julai 24, 1950, Mashahidi walipanga kusanyiko katika kibanda cha kuhifadhi nyasi cha mwanafunzi wa Biblia karibu na Otepää. Tulipogundua kwamba mipango ya kusanyiko hilo ilikuwa imegunduliwa na shirika la KGB, tuliwaonya wengi wa akina ndugu waliokuwa njiani. Mipango ilifanywa tukutane mahali pengine siku iliyofuata, na watu 115 hivi walihudhuria. Kila mtu alienda nyumbani akiwa na shangwe na akiwa amechochewa zaidi kuliko wakati mwingine wowote kudumisha uaminifu chini ya majaribu. *

Baadaye, mimi na Linda tuliendelea kuhubiri na kuwatia moyo Wakristo wenzetu. Baadaye katika mwaka huohuo tulishiriki kuvuna viazi na tukawahubiria wafanyakazi wenzetu ujumbe wa Ufalme. Mwenye shamba moja alisimama na kusikiliza tukizungumza kwa saa moja naye akasema, “Habari hizi ni habari za pekee kwelikweli!”

Mimi na Linda tulirudi katika jiji la Tartu ambako tuligundua kuwa Mashahidi wengi zaidi walikuwa wamekamatwa, kutia ndani mama ya Linda. Marafiki wetu wengi walikuwa wamekamatwa kutia ndani Emilie Sannamees na dada yake. Kwa kuwa tulijua kwamba maofisa wa shirika la KGB walikuwa wakitutafuta, tulinunua baiskeli mbili na tukaendelea kuhubiri nje ya Tartu. Usiku mmoja maofisa wa KGB walinipata nyumbani kwa Alma Vardja, ambaye alikuwa amebatizwa karibuni. Walipotazama pasipoti yangu, mmoja wao alisema kwa mshangao: “Ella! Tumekuwa tukikutafuta kila mahali!” Huo ulikuwa usiku wa Desemba 27, 1950.

Kufungwa Kisha Kuhamishwa Hadi Siberia

Mimi na Alma tulipakia vitu vichache kwa utulivu, kisha tukala. Maofisa hao wa KGB walishangaa na kusema, “Hata hamtoi machozi. Mnaketi tu hapo mkila.” Tuliwajibu, “Tunaenda kwenye mgawo wetu mpya nasi hatujui tutakula lini tena.” Nilibeba blanketi ambayo nilitumia kutengeneza soksi nzito na sweta. Baada ya kufungwa kwa miezi mingi, mnamo Agosti 1951, mimi pamoja na Mashahidi wengine tulihamishwa hadi Estonia. *

Kutoka Estonia tulihamishwa kwa gari-moshi hadi Leningrad (sasa ni St. Petersburg), Urusi, na kutoka hapo tukapelekwa kwenye kambi zenye sifa mbaya huko Vorkuta, Komi, juu ya Mzingo wa Aktiki. Kulikuwa na Mashahidi watatu katika kikundi chetu. Nikiwa shuleni nilikuwa nimejifunza Kirusi na nilikuwa nikifanya mazoezi tangu nilipokamatwa. Kwa hiyo, tulipofika kwenye kambi nilikuwa nikizungumza Kirusi vizuri.

Huko Vorkuta tulikutana na mwanamke kijana kutoka Ukrainia ambaye alijifunza na kuwa Shahidi katika kambi ya mateso ya Nazi huko Poland. Mnamo 1945 yeye na Mashahidi wengine 14 waliingizwa katika meli ambayo Wajerumani walitaka kuizamisha katika Bahari ya Baltiki. Hata hivyo, meli hiyo ilifika salama huko Denmark. Baadaye, aliporudi Urusi, alikamatwa kwa sababu ya kuhubiri na akatumwa huko Vorkuta, ambako alitutia moyo sana.

Pia tulikutana na wanawake wawili, ambao waliuliza kwa Kiukrainia, “Je, kuna yeyote kati yenu ambaye ni Shahidi wa Yehova?” Mara moja tulitambua kwamba wao ni dada zetu Wakristo! Walitutia moyo na kututunza. Wafungwa wengine walisema ni kana kwamba tulikuwa tukingojewa na washiriki wa familia yetu.

Nahamishwa Hadi Kambi za Mordovia

Mnamo Desemba 1951, uchunguzi wa kitiba ulipoonyesha kwamba nina tatizo la kikoromeo, nilihamishwa karibu kilometa 1,500 kusini-magharibi kwenye jela kubwa ya Mordovia kilometa 400 hivi kusini-mashariki ya Moscow. Miaka kadhaa iliyofuata, nilikutana na Mashahidi kutoka Hungary, Poland, Ujerumani, na Ukrainia katika kambi za wanawake ambako nilifungwa. Pia nilikutana na Maimu, mfungwa wa kisiasa kutoka Estonia.

Alipokuwa gerezani huko Estonia, Maimu alijifungua, na mlinzi mwenye fadhili akampeleka mtoto kwa mama ya Maimu. Katika gereza hilo huko Mordovia, tulijifunza Biblia na Maimu, naye akakubali aliyokuwa akijifunza. Alimwandikia barua mama yake, ambaye pia alikubali kweli za Biblia na kumfunza Karin, binti ya Maimu. Miaka sita baadaye Maimu alifunguliwa kutoka gerezani naye akaungana tena na mtoto wake. Karin alipokuwa mkubwa, alioa Shahidi mwenzake. Wametumika pamoja kwa miaka 11 iliyopita katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Tallinn, Estonia.

Ndani ya kuta za jela hiyo kubwa ya Mordovia kulikuwa na kambi moja ndogo iliyokuwa na ulinzi mkali. Mimi na Mashahidi wengine sita tulifungwa huko kwa sababu ya utendaji wetu wa Kikristo. Lakini hata tulipokuwa hapo, tuliandika nakala ndogo sana za makala za Mnara wa Mlinzi na kuwapa wengine katika kambi zilizokuwa karibu kwa siri. Njia moja tuliyofanya hivyo ni kwa kuchonga shimo ndani ya sabuni, kutia makala hiyo ndani, na kufunika tena sabuni hiyo.

Katika kipindi nilichofungwa kwenye kambi za Mordovia, niliwasaidia watu kumi kuchukua msimamo wa kumtumikia Mungu. Mwishowe, Mei 4, 1956, niliambiwa, “Uko huru kwenda na kumwamini Mungu wako, Yehova.” Nilifika nyumbani huko Estonia mwezi huohuo.

Nilirudi Nyumbani Miaka 50 Hivi Iliyopita

Sikuwa na kazi, pesa wala makao. Lakini siku chache baada ya kurudi, nilikutana na mwanamke ambaye alipendezwa na mafundisho ya Biblia. Aliniruhusu niishi kwa muda pamoja naye na mume wake katika chumba chao kimoja. Nilinunua uzi fulani kwa pesa nilizokopa na kushona sweta ambazo niliuza sokoni. Baadaye nilipewa kazi katika Hospitali ya Matibabu ya Kansa ya Tartu ambako nilifanya kazi mbalimbali kwa miaka saba iliyofuata. Wakati huohuo, Lembit Toom pia alirudi kutoka uhamishoni Siberia, na mnamo Novemba 1957 tukafunga ndoa.

Tuliandamwa na maofisa wa KGB, nasi tulidhulumiwa kila mara kwa kuwa kazi yetu ya kuhubiri bado ilikuwa imepigwa marufuku. Hata hivyo, tulijitahidi kadiri tulivyoweza kuwaeleza wengine imani yetu. Lembit alieleza habari hiyo katika Amkeni! la Februari 22, 1999. Katika miaka ya mwishomwisho ya 1950 na katika miaka ya 1960 na ya 1970, Mashahidi waliokuwa wamehamishwa waliendelea kurudi nyumbani. Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1980, tulikuwa na Mashahidi zaidi ya 700 nchini Estonia. Mnamo 1991, kazi yetu ya Kikristo iliandikishwa kisheria, na tangu wakati huo tumeongezeka kufikia zaidi ya Mashahidi 4,100 nchini Estonia!

Sasa ni zaidi ya miaka 60 tangu nilipohudhuria mkutano ule wa kwanza wa siri wa Mashahidi nchini Estonia baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Tangu wakati huo, azimio langu limekuwa kutii maneno haya ya Biblia: “Mtegemee Yehova na ufanye mema.” Nimegundua kwamba unapofanya hivyo unapokea “maombi ya moyo wako.”—Zaburi 37:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Mmoja wa vijana hao alikuwa Lembit Toom, ambaye simulizi lake liko katika gazeti Amkeni! la Februari 22, 1999.

^ fu. 30 Kwa habari zaidi kuhusu kusanyiko hilo, ona Amkeni! la Februari 22, 1999, ukurasa wa 12-13.

^ fu. 34 Hata hivyo, Mashahidi wengi nchini Estonia, walikuwa wamehamishwa mapema mnamo Aprili 1951. Ona Amkeni! la Aprili 22, 2001, ukurasa wa 6-8, na video Faithful Under Trials—Jehovah’s Witnesses in the Soviet Union.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

“Acha tuanze kuhubiri sasa ili tueneze habari njema kotekote Estonia.”—Linda Mettig

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa na Mashahidi wengine tisa ndani ya jela ya Mordovia

[Picha katika ukurasa wa 24]

Leo, nikiwa na mume wangu, Lembit