Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Sisi Huzeeka?

Kwa Nini Sisi Huzeeka?

Kwa Nini Sisi Huzeeka?

“Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.”—AYUBU 14:1, UNION VERSION.

HUENDA ukawazia kwamba lazima viumbe-hai vyote vizeeke. Magari na mashini ambazo hutumiwa kila siku mwishowe huacha kufanya kazi. Huenda mtu akafikiri kwamba wanyama huzeeka na kufa kwa njia hiyohiyo. Lakini profesa wa elimu kuhusu wanyama Steven Austad anasema: “Viumbe vinatofautiana sana na mashini. Jambo kuu linalotofautisha viumbe na mashini ni kwamba viumbe vina uwezo wa kujirekebisha.”

Inastaajabisha jinsi ambavyo mwili wako hujirekebisha baada ya kujeruhiwa, lakini inastaajabisha hata zaidi jinsi ambavyo mwili hujirekebisha kila siku. Kwa mfano, fikiria mifupa yako. “Inapotazamwa kwa nje, inaonekana kuwa haina uhai, lakini mifupa ni tishu hai ambayo daima hujiangamiza na kujirekebisha upya katika maisha yako yote,” linasema gazeti Scientific American. “Hatua hiyo ya kujirekebisha hufanyiza upya kabisa kiunzi cha mifupa ya mwanadamu kila baada ya miaka 10.” Sehemu nyingine za mwili wako hufanyizwa upya mara nyingi zaidi. Huenda chembe fulani za ngozi, ini, na matumbo zikafanyizwa upya karibu kila siku. Kila sekunde, mwili wako hutokeza chembe mpya zipatazo milioni 25. Ikiwa mwili wako haungefanya hivyo, na sehemu zote za mwili wako zisijirekebishe na kujibadili, ungezeeka ukiwa mtoto.

Hoja ya kwamba hatuchakai ilistaajabisha zaidi wanabiolojia walipoanza kujifunza kuhusu molekuli katika chembe-hai. Chembe zako zinapofanyizwa upya, lazima kila chembe mpya iwe na nakala ya DNA yako. DNA ndiyo molekuli iliyo na habari nyingi inayohitajika ili kufanyiza upya mwili wako. Hebu wazia DNA imetokezwa mara ngapi, si tu katika mwili wako tangu ulipozaliwa, bali tangu uhai wa binadamu ulipoanza! Ili kuelewa jinsi jambo hilo linavyostaajabisha, fikiria kile ambacho kingetokea iwapo ungetumia mashini ya fotokopi kutoa nakala ya hati fulani kisha utumie nakala hiyo mpya kutokeza nakala nyingine. Ikiwa ungefanya hivyo tena na tena, ubora wa nakala ungeendelea kudhoofika na mwishowe nakala hiyo haingeweza kusomeka. Jambo la kufurahisha ni kwamba ubora wa DNA yetu haudhoofiki au kuchakaa kadiri chembe zetu zinavyotokeza chembe mpya tena na tena. Kwa nini? Kwa sababu chembe zetu zina njia nyingi za kurekebisha kasoro katika nakala ya DNA. Ikiwa hazingeweza kufanya hivyo, wanadamu wangekuwa wametoweka zamani za kale!

Kwa kuwa sehemu zote za mwili wetu, kuanzia zile kubwa hadi molekuli ndogo kabisa hufanyizwa upya au kurekebishwa daima, kuchakaa hakuelezi kwa ukamili sababu inayofanya tuzeeke. Mifumo mingi ya mwili hujirekebisha na kujifanyiza upya kwa miaka mingi, katika njia tofauti na mwendo tofauti. Kwa hiyo, kwa nini mifumo hiyo yote huacha kufanya kazi karibu wakati uleule?

Je, Kuzeeka Kumepangwa Kimbele?

Kwa nini paka huishi miaka 20, lakini mnyama mwenye ukubwa sawa naye anayeitwa opossum huishi kwa miaka 3 tu? * Kwa nini popo anaweza kuishi kwa miaka 20 au 30, lakini panya huishi kwa miaka 3 tu? Kwa nini kobe-jitu anaweza kuishi kwa miaka 150 lakini tembo aishi kwa miaka 70 tu? Mambo kama vile chakula, uzito wa mwili, ukubwa wa ubongo, au ukuzi hayaelezi sababu inayofanya viumbe fulani waishi muda mrefu na wengine waishi muda mfupi. Kichapo Encyclopædia Britannica kinasema: “Chembe za urithi zina maagizo ambayo huonyesha miaka hususa ambayo viumbe fulani wataishi.” Muda ambao viumbe wataishi umeandikwa kwenye chembe za urithi. Lakini kiumbe anapokaribia kufa, ni nini hufanya utendaji wote wa mwili uache kufanya kazi?

Mwanabiolojia wa molekuli Dakt. John Medina anaandika hivi: “Inaonekana kwamba kuna ishara zisizoeleweka ambazo hutokea nyakati fulani na kuagiza chembe ziache kufanya kazi yao ya kawaida.” Pia anasema: “Kuna chembe za urithi ambazo zinaweza kuagiza chembe nyingine, na hata mwili wote uzeeke na kufa.”

Mwili wetu unaweza kulinganishwa na kampuni ambayo imekuwa ikifanya kazi kwa mafanikio kwa miaka mingi. Kwa ghafula, meneja wake wanaacha kuajiri na kuzoeza wafanyakazi wapya, wanaacha kurekebisha na kununua mashini mpya, na wanaacha kudumisha na kujenga upya majengo. Baada ya muda mfupi, kampuni hiyo itaanza kuzorota. Lakini kwa nini meneja hao walibadili sera zao zilizoleta mafanikio? Swali hilo ni sawa na lile ambalo wanabiolojia wanaochunguza kuzeeka wanakabili. Kitabu The Clock of Ages kinasema: “Katika utafiti kuhusu kuzeeka, jambo moja linalotatanisha sana ni kujaribu kuelewa sababu inayofanya chembe ziache kujifanyiza upya na kuanza kufa.”

Je, Kuzeeka Kunaweza Kukomeshwa?

Kuzeeka kumetajwa kuwa “tatizo gumu zaidi la kibiolojia kueleweka.” Baada ya kujaribu kwa miaka mingi, utafiti wote wa kisayansi haujafunua kisababishi cha kuzeeka sembuse jinsi ya kuukomesha. Mnamo 2004 gazeti Scientific American lilichapisha onyo la wanasayansi 51 wanaochunguza kuzeeka. Walionya hivi: “Hakuna bidhaa hata moja inayopatikana sasa ya kuzuia kuzeeka ambayo imethibitishwa kuwa inaweza kupunguza, kuzuia, au kufanya wazee wawe vijana tena.” Ingawa chakula bora na mazoezi yanaweza kuboresha afya yako na kupunguza hatari za kufa mapema kutokana na ugonjwa, hakuna kitu kinachoweza kuzuia kuzeeka. Mikataa hiyo inatukumbusha maneno haya ya Yesu yanayopatikana katika Biblia: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?”—Mathayo 6:27.

Akitoa muhtasari kuhusu maendeleo ya kutafuta matibabu ya kuzeeka, Medina anaandika hivi: “Kwa kweli hatujui hasa sababu inayofanya tuzeeke. . . . Baada ya kuanzisha kampeni ya kukomesha kansa miaka mingi iliyopita, bado hatujapata tiba ya kansa. Na kuzeeka ni jambo gumu zaidi kushughulikia kuliko kansa.”

Mkataa Muhimu Wafikiwa Baada ya Utafiti

Utafiti kuhusu jinsi ambavyo viumbe hufanya kazi na sababu inayofanya vizeeke haujakatisha matumaini ya kuishi muda mrefu zaidi. Watu fulani wamegundua kwamba utafiti wao umewachochea kufikia mkataa muhimu ambao utawasaidia kuelewa kuzeeka. Mwanabiolojia wa molekuli Michael Behe anaandika hivi: “Kwa muda wa miaka 40 biokemia ya kisasa imefichua mambo mengi kuhusu chembe ambayo hayakujulikana awali. . . . Matokeo ya uchunguzi huo wote, yaani, kuchunguza uhai kwa kuangalia jinsi ambavyo molekuli za chembe hufanya kazi, ni uthibitisho ulio wazi na wenye kutokeza kwamba viumbe-hai ‘vilibuniwa’!” Mtu fulani alitumia akili nyingi kubuni viumbe-hai. Bila shaka, Behe siye mtu wa kwanza kufikia mkataa huo. Baada ya kufikiria muundo wa mwili wa binadamu, mtunga-zaburi wa kale aliandika hivi: “Nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—Zaburi 139:14.

Ikiwa viumbe vyote vilivyo hai vimebuniwa, basi twapaswa kujiuliza swali hili lenye kuvuta fikira, Je, Mungu, yule Mbuni Mkuu aliumba wanadamu waishi kwa muda kama ule wa wanyama wengi, au je, anataka tuishi muda mrefu zaidi kuliko wanyama?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Mnyama anayeitwa opossum ni kati ya wanyama wasiokuwa na kondo na aliye na kifuko cha kubebea watoto ambaye hupatikana Amerika Kaskazini.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

‘Tumeumbwa kwa njia ya ajabu’

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Je, kuzeeka husababishwa na kuchakaa?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]

DNA: Photo: www.comstock.com