Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maadili Yalipoporomoka Ghafula

Maadili Yalipoporomoka Ghafula

Maadili Yalipoporomoka Ghafula

UNGESEMA maadili yalianza kuporomoka ghafula wakati gani? Je, uliona yalipoanza kuporomoka au labda una watu wa ukoo na marafiki wenye umri mkubwa ambao waliona mambo hayo yalipoanza kutendeka? Wengine wanasema kwamba Vita vya Kwanza vya Ulimwengu ambavyo vilianza 1914, vilitokeza kipindi hiki cha maadili yaliyopotoka kupita kiasi. Profesa wa historia Robert Wohl aliandika hivi katika kitabu chake (The Generation of 1914) kinachozungumzia kizazi cha 1914: “Wale walioishi wakati wa vita wanaamini kabisa kwamba ulimwengu mmoja uliisha na mwingine ukaanza Agosti 1914.”

“Kila mahali, viwango vya tabia katika jamii ambavyo tayari vilikuwa vikiporomoka viliharibika kabisa,” anasema mwanahistoria Norman Cantor. “Ikiwa wanasiasa na majenerali waliwatendea mamilioni waliokuwa chini yao kama wanyama wanaopelekwa machinjioni, basi ni kanuni gani za kidini au za kiadili ambazo zingeweza kuwazuia watu wasitendeane kwa ukatili kama wanyama wa mwituni? . . . Uchinjaji uliofanyika wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu [1914-1918] ulishusha kabisa thamani ya uhai wa mwanadamu.”

Katika kitabu chake cha kihistoria (The Outline of History), mwanahistoria Mwingereza H. G. Wells alisema kwamba baada ya ulimwengu kukubali nadharia ya mageuzi, “maadili yalianza kupotoka kwa kiwango kikubwa.” Kwa nini? Wengine walidai kwamba mwanadamu ni mnyama wa hali ya juu tu. Wells, ambaye alikuwa mwanamageuzi, aliandika hivi mnamo 1920: “Waliamua kwamba mwanadamu ni mnyama wa kijumuiya kama mbwa-mwitu wakali wa India . . . , ilionekana sawa kwao kwamba wenye nguvu kati ya binadamu walipaswa kukandamiza na kutiisha walio dhaifu.”

Kwa kweli, kama Cantor alivyosema, vita vya kwanza vya ulimwengu viliathiri sana maoni ya watu kuhusu maadili. Alieleza hivi: “Kila kitu ambacho kizazi cha zamani kilifanya kilionwa kuwa makosa, iwe ni siasa zake, mavazi, au maoni yake kuhusu ngono.” Makanisa ambayo yalipotosha mafundisho ya Kikristo kwa kukubali nadharia ya mageuzi na kuwatia moyo watu wajihusishe katika vita, yalichangia sana kuporomoka kwa maadili. Brigedia Jenerali Frank Crozier wa Uingereza aliandika: “Makanisa ya Kikristo ndiyo wachochezi wakuu wa umwagikaji wa damu ulioko, nasi tumeyatumia sana.”

Sheria za Maadili Zatupiliwa Mbali

Mwongo mmoja baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, wakati wa ile inayoitwa Miaka ya Kujitumbukiza Kwenye Anasa (1920-1929), kanuni za zamani na vizuizi vya maadili viliwekwa kando na mwelekeo wa kukubali mwenendo wowote ukachukua mahali pake. Mwanahistoria Frederick Lewis Allen anasema hivi: “Miaka kumi iliyofuatia vita hivyo inaweza kuitwa kwa kufaa kuwa Mwongo wa Tabia Mbaya. . . . Utaratibu wa mambo wa zamani pamoja na fungu la kanuni ambazo zilikuwa zimefanya uhai uwe bora na wenye thamani, zilikuwa zimetoweka, na haikuwa rahisi kupata kanuni nyingine.”

Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi ulimwenguni ambao ulitukia katika miaka ya 1930 uliwatumbukiza watu kwenye umaskini uliowafanya wafikirie mambo kwa uzito. Hata hivyo, kufikia mwisho wa mwongo huo, ulimwengu ulikuwa umeingia tena katika vita vingine vilivyosababisha vifo na uharibifu mkubwa sana, yaani, Vita vya Pili vya Ulimwengu. Punde si punde, mataifa yakaanza kutengeneza silaha za maangamizi, na hivyo kuukomboa ulimwengu kutokana na Mshuko huo. Wakati huohuo kufanya hivyo kuliutumbukiza ulimwengu katika kuteseka na kutokeza hali zenye kuogofya sana. Kufikia mwisho wa vita hivyo, mamia ya majiji yalikuwa magofu; majiji mawili nchini Japani yalikuwa yameangamizwa kabisa, kila moja kwa bomu la atomi! Mamilioni ya watu walikufa katika kambi za mateso zenye ukatili. Kwa ujumla, vita hivyo vilisababisha vifo vya wanaume, wanawake, na watoto wapatao milioni 50.

Wakati wa hali hizo zenye kutisha sana za Vita vya Pili vya Ulimwengu, badala ya kushikamana na viwango vya maadili vilivyokuwepo kwa muda mrefu, watu walianzisha viwango vyao wenyewe vya maadili. Kitabu (Love, Sex and War—Changing Values, 1939-1945) kinachozungumzia kubadilika kwa kanuni za maadili kilisema hivi: “Ilionekana kwamba viwango vyote vya maadili kuhusu ngono vilikuwa vimeondolewa wakati wa vita, kwani ukosefu wa maadili ambao uliruhusiwa kwa watu waliokuwa vitani uliwaathiri pia raia. . . . Hekaheka na msisimko wa vita ulimomonyoa maadili, na uhai wa raia ulionekana kuwa usio na thamani kubwa kama tu ule wa askari waliokuwa vitani.”

Hofu ya kwamba mtu anaweza kufa wakati wowote iliwafanya watu watamani sana kuwa na mahusiano ya kimahaba, hata kwa muda mfupi tu. Akitetea utovu huo wa maadili katika ngono wakati wa miaka hiyo ya vita, mwanamke mmoja Mwingereza alisema hivi: “Si eti tulikuwa na maadili mapotovu, ni kwamba tu vita vilikuwa vikiendelea.” Askari mmoja Mmarekani alikiri hivi, “Kwa maoni ya watu wengi, tulikuwa na maadili mapotovu, lakini tulikuwa vijana na tungeweza kufa wakati wowote.”

Watu wengi walionusurika vita hivyo waliathiriwa sana na mambo yenye kutisha waliyoyaona. Hadi leo, watu wengine kutia ndani wale ambao wakati huo walikuwa watoto, hukumbuka matukio hayo vizuri sana na kuhisi ni kana kwamba yanatukia tena. Wengi walipoteza imani yao na viwango vya maadili. Bila kuheshimu mamlaka yoyote ambayo inaweza kuweka viwango vya lililo sawa na lililo kosa, watu walianza kuona mambo yote yanaweza kubadilika ikitegemea hali.

Viwango Vipya

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, uchunguzi mbalimbali ulichapishwa kuhusu tabia ya watu kuelekea ngono. Uchunguzi mmoja kama huo nchini Marekani katika miaka ya 1940 uliitwa Ripoti ya Kinsey iliyokuwa na zaidi ya kurasa 800. Kwa sababu hiyo, watu wengi walianza kuzungumza waziwazi kuhusu mambo ya ngono ambayo kabla ya hapo hayangeweza kuzungumziwa waziwazi. Ingawa baadaye ilionekana kwamba takwimu zilizotolewa katika ripoti hiyo kuhusu watu wanaofanya ngono na watu wa jinsi yao na matendo mengine mapotovu ya ngono zilikuwa zimetiliwa chumvi, uchunguzi huo ulifunua jinsi maadili yalivyoporomoka baada ya vita hivyo.

Kwa kipindi fulani, kulikuwa na jitihada ya kudumisha maadili yanayofaa. Kwa mfano, kwenye redio, sinema, na televisheni, habari chafu zilichujwa. Lakini jambo hilo halikudumu. William Bennett, ambaye awali alikuwa waziri wa elimu wa Marekani, alieleza hivi: “Hata hivyo, kufikia miaka ya 1960, ustaarabu ulianza kuporomoka kwa kasi nchini Marekani.” Jambo hilo lilionekana pia katika nchi nyingine nyingi. Kwa nini maadili yaliporomoka kwa kasi sana katika miaka ya 1960?

Kana kwamba mambo hayo yalitendeka kwa mfululizo, harakati ya kuwakomboa wanawake na kubadilika kwa mitazamo kuhusu ngono pamoja na yale yaliyoitwa maadili mapya, yalianza mwongo huohuo. Pia, dawa za kupanga uzazi zilibuniwa. Kwa kuwa sasa watu wangeweza kufurahia ngono bila hofu ya kupata mimba, walianza kufanya ngono ovyoovyo bila kuwajibika.

Wakati huohuo, vyombo vya habari, sinema, na televisheni vililegeza viwango vyake vya maadili. Baadaye, Zbigniew Brzezinski, ambaye hapo awali alikuwa mkuu wa Baraza la Usalama wa Kitaifa la Marekani alisema hivi kuhusu maadili yanayoonyeshwa katika televisheni: “Wanatukuza kujitosheleza, wao huonyesha jeuri na ukatili kuwa mambo ya kawaida, [na] wanaunga mkono kufanya ngono na watu wengi.”

Kufikia miaka ya 1970, mashine za kuchezea kanda za video zilikuwa zimeanza kutumiwa sana. Sasa watu wangeweza kuona picha chafu sana wakiwa faraghani, habari ambazo hawangeweza kutazama katika majumba ya sinema ya umma. Katika nyakati za karibuni, mtu yeyote aliye na kompyuta, popote alipo ulimwenguni anaweza kupata ponografia chafu zaidi kwenye Intaneti.

Matokeo yake yanatisha. Hivi majuzi, msimamizi mmoja wa gereza huko Marekani alisema: “Miaka kumi iliyopita vijana walipoletwa hapa, ningeweza kuwapa mashauri kuhusu lililo sawa na lililo kosa. Lakini vijana wanaoletwa siku hizi hawaelewi ninasema nini.”

Tunaweza Kupata Wapi Mwongozo?

Hatuwezi kutafuta mwongozo kuhusu maadili kutoka kwa makanisa ya ulimwengu. Badala ya kushikilia kanuni za uadilifu kama Yesu na wafuasi wake wa karne ya kwanza, makanisa yamejifanya kuwa sehemu ya ulimwengu huu na matendo yake maovu. Mwandishi mmoja aliuliza hivi: “Ni vita gani ambavyo vimewahi kupiganwa ambavyo haikudaiwa kwamba Mungu alikuwa akiunga mkono pande zote?” Kasisi mmoja huko New York City alisema hivi miaka fulani iliyopita kuhusu kushikilia viwango vya Mungu vya maadili: “Kanisa ndilo shirika pekee ulimwenguni ambalo wafuasi wake wanahitajiwa kutimiza matakwa machache sana ya kiadili kuliko hata yale ambayo mtu anahitaji kutimiza ili aingie kwenye basi.”

Ni wazi kwamba kuporomoka haraka kwa maadili katika ulimwengu huu kunaonyesha kwamba hatua fulani zinapaswa kuchukuliwa. Hatua gani? Ni mabadiliko gani yanayohitajiwa? Ni nani atakayefanya mabadiliko hayo, nayo yatafanywaje?

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Uchinjaji uliofanyika wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu [1914-1918] ulishusha kabisa thamani ya uhai wa mwanadamu

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Vitumbuizo vilivyopotoka vinapatikana kwa urahisi zaidi