Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuazimia Kuwa Tajiri Kiroho

Kuazimia Kuwa Tajiri Kiroho

Kuazimia Kuwa Tajiri Kiroho

ILI mtu awe tajiri kimwili anahitaji kuendelea kujitahidi na kujinyima mambo fulani. Ndivyo ilivyo na kuwa tajiri kiroho. Yesu alidokeza jambo hilo aliposema hivi: “Jiwekeeni hazina mbinguni.” (Mathayo 6:20) Hazina za kiroho hazitokei zenyewe tu. Mtu hawezi kuwa tajiri kimwili kwa sababu tu ana akaunti ya benki. Vivyo hivyo, hawezi kuwa tajiri kiroho eti kwa sababu tu ana dini. Ili mtu asitawishe uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, awe mtu wa kiroho, na awe na sifa nyingi za kiroho anahitaji kuwa na azimio, wakati, kuendelea kujitahidi, na kujinyima mambo fulani.—Methali 2:1-6.

Je, Unaweza Kuwa na Mambo Yote Mawili?

Je, inawezekana mtu awe tajiri kiroho na wakati huohuo awe tajiri kimwili? Huenda ikawezekana, lakini mtu anaweza kukazia fikira jambo moja tu kati ya hayo. Yesu alisema: “Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24b) Kwa nini? Kwa sababu ni vigumu kujitahidi kupata utajiri wa kiroho na wakati uleule kujitahidi kupata mali. Mambo hayo mawili hayapatani, na moja litachukua mahali pa lingine. Kwa hiyo, kabla hajawaambia wanafunzi wake wajiwekee hazina za kiroho, Yesu alisema: “Acheni kujiwekea hazina duniani.”—Mathayo 6:19.

Mtu akipuuza shauri la Yesu na kujaribu kuwa tajiri kiroho na kimwili, ni nini kitakachotukia? Yesu alisema: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine.” (Mathayo 6:24a) Mtu anapojitahidi kupata yote mawili, anaweza kuanza kuona kwamba mambo ya kiroho yanachosha na ni kizuizi, hata ikiwa anahisi wajibu wa kuyatekeleza. Badala ya kumtegemea Mungu, hata anaweza kuona pesa na mali kuwa njia kuu ya kushughulikia matatizo maishani. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”—Mathayo 6:21.

Inafaa kila Mkristo afikirie kwa uzito mashauri hayo ya Biblia kabla ya kuamua jinsi atakavyotumia wakati wake, mambo ambayo atakazia fikira, na mahali ambapo ataelekeza moyo wake. Ingawa Mungu haweki mipaka hususa kuhusu kiasi cha mali ambacho Mkristo anaweza kujirundikia, hilo halimaanishi kwamba mtu hataathiriwa anapopuuza maonyo ya Mungu kuhusu pupa. (1 Wakorintho 6:9, 10) Kama tulivyoona, wale wanaopuuza mashauri ya Biblia na kuazimia kuwa matajiri wanaathiriwa kiroho, kiakili, na kihisia. (Wagalatia 6:7) Kinyume na hilo, Yesu alisema kwamba wale wanaotambua mahitaji yao ya kiroho watapata furaha. (Mathayo 5:3) Ndiyo, Muumba wetu na Mwana wake wanajua mambo ambayo yatatuletea furaha na mafanikio.—Isaya 48:17, 18.

Uamuzi Ambao Hutaujutia

Basi utaamua kumtumikia Mungu au mali? Ni kweli kwamba tunapaswa kushughulikia mahitaji yetu ya kimwili. Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, mtume Paulo alisema hivi: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” Pia, Paulo aliwahimiza Wakristo waweke tumaini lao, si katika pesa, bali katika Mungu na “wawe matajiri katika matendo mazuri.” (1 Timotheo 5:8; 6:17, 18) Utakazia nini fikira? Kusudi lako kuu maishani litakuwa nini? Kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake ndiyo ya maana zaidi kati ya matendo mazuri ambayo Paulo alitaja. (Mathayo 28:19, 20) Wakristo wanapochagua kupunguza mali zao ili wafanye mengi zaidi katika kazi hiyo ya maana na si ili kustarehe au kufurahia maisha tu, ‘wanajiwekea wenyewe hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao’ katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Na hata sasa wanatambua kwamba utajiri wa kiroho ni “bora kama nini kuliko dhahabu!”—1 Timotheo 6:19; Methali 16:16; Wafilipi 1:10.

Fikiria kisa cha Eddie, ambaye alipokuwa kijana watu wa familia yao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Wakati fulani, familia yao ilipoteza mali zao zote na ikawabidi wahame kutoka katika nyumba yao. Eddie anasema hivi: “Zamani nilikuwa nikijiuliza kile ambacho kingetokea ikiwa tungepoteza kila kitu. Sasa wakati huo ulikuwa umefika. Na unajua kilichotokea? Hakuna! Bado tulikula, tulikunywa, na tulikuwa na mavazi. Yehova alitupa tulichohitaji, na baada ya muda tukapata tena vitu tulivyopoteza. Kisa hicho kilinifundisha kuchukua kwa uzito ahadi ya Yesu iliyo katika Mathayo 6:33—kwamba tukitanguliza Ufalme wa Mungu maishani, hatuhitaji kuhangaikia mahitaji yetu ya kimwili.” Leo, Eddie ni mwangalizi anayesafiri, naye anatumikia pamoja na mke wake. Mahitaji yao ya kimwili yanatoshelezwa. Zaidi ya yote, wao ni matajiri kiroho.

Faida Zisizo na Kifani

Tofauti na hazina zilizo duniani, ambazo wezi wanaweza kuiba, utajiri wa kiroho ni wa kudumu. (Methali 23:4, 5; Mathayo 6:20) Ni kweli kwamba ni vigumu kupima maendeleo ya kiroho. Ni rahisi zaidi kupima maendeleo ya mtu ya kimwili kuliko ilivyo kupima maendeleo yake katika kukuza upendo, shangwe, au imani. Lakini faida za utajiri wa kiroho hazina kifani. Akizungumza kuhusu wanafunzi ambao wangeacha hata nyumba zao na mashamba yao, yaani, njia yao ya kupata riziki, ili kuwa na nafasi kwa ajili ya mambo ya kiroho, Yesu alisema: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Hakuna mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara mia sasa katika kipindi hiki cha wakati, nyumba na ndugu na dada na mama na watoto na mashamba, pamoja na mateso, na katika mfumo wa mambo unaokuja uzima wa milele.”—Marko 10:29, 30.

Utatanguliza nini? Mungu au mali?

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Je, unafanya bidii kupata mali za kimwili . . .

. . . au mali za kiroho?