Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatari Inayowahangaisha Wazazi Wote

Hatari Inayowahangaisha Wazazi Wote

HEATHER na Scott ni wenzi wa ndoa wachangamfu walio na mtoto mwenye umri wa miaka mitatu aliye na afya nzuri. * Wanamtunza mwana wao vizuri. Kwenye ulimwengu wa leo hilo si jambo rahisi, linatia ndani mahangaiko na majukumu mengi. Watoto wanahitaji kufundishwa mambo mengi sana. Heather na Scott wanahisi kwamba wana daraka zito hasa kuhusu jambo moja: Wanataka kumlinda mtoto wao asitendewe vibaya kingono. Kwa nini?

“Baba yangu hakuwa mwenye urafiki, alikuwa mwenye hasira na mlevi,” anasema Heather. “Alinipiga sana na kunitendea mimi na dada zangu vibaya kingono.” * Watu wengi wanakubali kwamba kutendewa hivyo kunaweza kumfanya mtu awe na matatizo makubwa sana ya kihisia. Si ajabu kwamba Heather ameazimia kumlinda mwana wake! Scott naye ameazimia kufanya vivyo hivyo.

Wazazi wengi wanahangaishwa sana na suala la watoto kutendewa vibaya. Labda wewe pia unahangaishwa na jambo hilo. Tofauti na Scott na Heather huenda usiwe umekumbwa moja kwa moja na mambo kama hayo, lakini bila shaka umesikia ripoti zenye kushtua kuhusu kuenea kwa zoea hilo lenye kuchukiza. Ulimwenguni pote wazazi wazuri wanaogopa wanaposikia kuhusu mambo yanayowapata watoto katika maeneo yao.

Haishangazi kuwa mtafiti mmoja anayechunguza masuala ya watu kutendewa vibaya kingono alisema kwamba kuenea kwa visa vya kutendea watoto vibaya ni “moja kati ya ugunduzi wenye kuvunja moyo wa enzi yetu.” Habari hizo ni zenye kuhuzunisha, lakini je, inashangaza kwamba mambo kama hayo yanazidi kuenea? Wanafunzi wa Biblia hawashangazwi na mambo hayo. Neno la Mungu linaeleza kwamba tunaishi katika wakati wenye taabu unaoitwa “siku za mwisho,” wakati ambapo watu wangekuwa “wakali,” na pia wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe” na “wasio na upendo wa asili.”—2 Timotheo 3:1-5.

Kuwatendea watoto vibaya kingono ni suala lenye kuogopesha. Kwa kweli, wazazi fulani huchukizwa wanapowaza kuhusu uovu wa watu wanaowatendea watoto vibaya kingono. Lakini, je, wazazi wanaweza kukabiliana na tatizo hilo? Au je, kuna hatua zinazofaa ambazo wazazi wanaweza kuchukua ili kuwalinda watoto wao? Makala zinazofuata zitazungumzia maswali haya.

^ fu. 2 Majina katika makala hizi yamebadilishwa.

^ fu. 3 Kumtendea mtoto vibaya kingono hutukia wakati ambapo mtu mzima anamtumia mtoto kutosheleza tamaa zake za kingono. Mara nyingi kunatia ndani kile ambacho Biblia inakiita uasherati, au por·neiʹa, ambayo inatia ndani kupapasa-papasa viungo vya uzazi, kufanya ngono, na ngono ya kinywa au ya mkundu. Vitendo vingine kama kupapasa-papasa matiti, kuwatongoza watoto, kumwonyesha mtoto ponografia (picha au habari za ngono), kuwachungulia sehemu zao za siri, na mtu kuwaonyesha kimakusudi sehemu zake za siri, vinaweza kutiwa ndani kati ya mambo ambayo Biblia inashutumu kuwa “mwenendo mpotovu” au “ukosefu wa usafi . . . kwa pupa.”—Wagalatia 5:19-21; Waefeso 4:19.