Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dhana au Mambo Hakika?

Dhana au Mambo Hakika?

Dhana au Mambo Hakika?

Mzee Mkristo Timotheo aliwatahadharisha wale wanaopenda kumwabudu Mungu wa kweli wazikazie uangalifu “mafundisho yaliyopotoka” na “dhana.” (1 Timotheo 1:3, 4, Byington) Je, tahadhari kama hiyo inahitajika leo? Bila shaka, kwa sababu mawazo yasiyofaa kuhusu Biblia na mafundisho yake yanawapotosha watu wasiipate ibada ya kweli. Hapa chini kuna maoni ambayo watu hutoa kuhusu Biblia na mambo hakika yanayosemwa katika Biblia. Hilo linaweza kukusaidia kupambanua kati ya dhana na mambo hakika.

Dhana: Miujiza inayotajwa katika Biblia haingeweza kutukia.

Mambo hakika: Wanadamu wana mengi ya kujifunza kuhusu uumbaji wa Mungu. Hakuna mwanasayansi anayeweza kufafanua kwa ukamili nguvu za uvutano ni nini, atomu inafanyizwa kwa vitu gani hasa au kufafanua kwa usahihi wakati ni nini. “Je, unaweza kuvumbua mambo yenye kina ya Mungu, au, je, unaweza kuvumbua kikomo chenyewe cha Mweza-Yote?” (Ayubu 11:7) Kwa kuwa mambo yanayohusu uumbaji ni ya hali ya juu sana kupita uwezo wetu wa kufikiri, wanasayansi stadi wanasita kusema kwamba mambo fulani hayawezekani.

Dhana: Dini zote zinawaongoza watu kwa Mungu.

Mambo hakika: Yesu alisema hivi: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:31, 32) Kama dini zote zinawaongoza watu kwa Mungu, je, kungekuwa na haja ya waumini wa dini hizo kuwekwa huru? Kwa kweli, Yesu alifundisha kwamba ni watu wachache tu walio katika “barabara inayoongoza kwenye uzima.”—Mathayo 7:13, 14.

Dhana: Watu wote wema huenda mbinguni wanapokufa.

Mambo hakika: “Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake. Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia.” (Zaburi 37:11, 29, 34) Ni watu 144,000 tu watakaokwenda mbinguni. Mungu amewapa kazi ya ‘kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 4.

Dhana: “Agano la Kale” haliwafai Wakristo.

Mambo hakika: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Timotheo 3:16, 17) “Kwa maana mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) “Agano la Kale,” yaani, Maandiko ya Kiebrania, ni chanzo muhimu sana cha mwongozo wa kiroho na linatupa msingi wa kuwa na imani katika “Agano Jipya,” yaani, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Dhana: Sehemu kubwa ya kitabu cha Mwanzo, kutia ndani masimulizi kuhusu Adamu na Hawa, ni ya kuwaziwa tu.

Mambo hakika: Historia ya ukoo wa Yesu inayorudi nyuma hadi kwa Adamu, iliandikwa na mwandikaji wa Injili Luka. (Luka 3:23-38) Kama masimulizi ya kitabu cha Mwanzo ni ya kuwaziwa tu, basi ni majina gani katika historia hiyo ya ukoo ambayo ni ya watu halisi na ni majina gani ambayo si ya watu halisi? Yesu, ambaye aliishi mbinguni kabla ya kuja duniani, aliamini kile kilichoandikwa katika kitabu cha Mwanzo, kutia ndani simulizi la Adamu na Hawa. (Mathayo 19:4-6) Hivyo, kutilia shaka kitabu cha Mwanzo ni sawa na kumtilia shaka Yesu mwenyewe, na waandikaji wale wengine wa Biblia.—1 Mambo ya Nyakati 1:1; 1 Wakorintho 15:22; Yuda 14.