Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dunia Itategemeza Vizazi Vijavyo?

Je, Dunia Itategemeza Vizazi Vijavyo?

Je, Dunia Itategemeza Vizazi Vijavyo?

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI KANADA

▪ Baada ya miaka minne ya uchunguzi wa makini wa mifumo mikubwa ya ikolojia ulimwenguni, kikundi cha wasomi na viongozi wa mazingira waliohusika walichapisha ripoti yao ya kwanza. Uchunguzi huo uliitwa Ukaguzi wa Milenia wa Mifumo ya Ikolojia [MA]. Zifuatazo ni baadhi ya kauli walizokata: Katika miaka 50 iliyopita, uhitaji wenye kuongezeka wa chakula, maji safi, mbao, nyuzi, na mafuta umesababisha mabadiliko makubwa sana katika mifumo ya ikolojia ya dunia na hivyo kupunguza uwezo wa dunia wa kutegemeza vizazi vijavyo. Uwezo wa asili wa dunia wa kuchavusha mimea, kusafisha hewa na kutokeza oksijeni kupitia mimea, na uwezo wa bahari wa kutokeza upya virutubisho unatumiwa kupita kiasi. Pia dunia inakabili tisho kubwa la kutoweka kwa jamii nyingi za viumbe.

“Wanadamu wanaiharibu dunia kwa kasi sana hivi kwamba wanaongeza hatari ya mifumo ya asili kuacha kutenda kwa njia ya kwamba magonjwa yataongezeka, misitu itaharibiwa, au kutakuwa na maeneo ya bahari yasiyo na viumbe,” lilisema gazeti Globe and Mail la Kanada. Gazeti hilo liliendelea kusema hivi: “Vinamasi, misitu, maeneo ya savana, milango ya mito, maeneo ya uvuvi ya pwani, na maeneo mengine ambayo husafisha hewa, maji na kutokeza upya virutubisho kwa ajili ya viumbe hai wote yanaharibiwa sana hivi kwamba hayawezi kurekebishwa.” Ingawa baraza la wakurugenzi wa MA linakubali kwamba wanadamu wana uwezo wa kupunguza uharibifu wa mifumo ya ikolojia, wanasema kwamba ili kutimiza hilo “kunapaswa kuwa na mabadiliko makubwa ya jinsi mazingira yanavyotendewa.”

Je, Dunia inaweza kuokolewa? Ndiyo! Tukiwa watunzaji wa uumbaji wa Mungu, tunapaswa kufanya yote tunayoweza kuonyesha tunathamini mazingira. (Zaburi 115:16) Hata hivyo, Mungu tu ndiye anayeweza kusawazisha tena mifumo ya ikolojia. ‘Mtengenezaji wetu Mkuu’ anaahidi kwamba ataielekezea dunia fikira na ‘kuipatia wingi.’ (Ayubu 35:10; Zaburi 65:9-13) Ahadi hiyo inatia ndani bahari na kila kitu kilichomo kwa sababu akiwa Muumba, Yehova Mungu ana nguvu juu ya bahari. (Zaburi 95:5; 104:24-31) Na bila shaka, anachoahidi kitatimia kwa sababu Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’—Tito 1:2.

Inafariji sana kujua kwamba dunia itategemeza vizazi vijavyo. Hilo linawachochea wote wanaomwogopa Mungu wamsifu kwa sababu ya hekima, nguvu, na wema wake mwingi na kumtukuza kwa upendo wake mwingi kuelekea kazi zake za uumbaji.—Zaburi 150:1-6.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 12]

Globe: NASA photo