Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watoto na Intaneti—Mambo Ambayo Wazazi Wanaweza Kufanya

Watoto na Intaneti—Mambo Ambayo Wazazi Wanaweza Kufanya

Watoto na Intaneti—Mambo Ambayo Wazazi Wanaweza Kufanya

UKIWA mzazi, ni jambo gani lingekuhangaisha zaidi—kujua kwamba mtoto wako ana funguo za gari au kujua kwamba amefungua vituo vya Intaneti bila usimamizi? Mambo yote mawili yanaweza kuwa hatari. Na yote yanahitaji mtu awe mwangalifu. Wazazi hawawezi sikuzote kuwazuia watoto wao kuendesha gari, lakini wanaweza kuhakikisha kwamba watoto wao wamefundishwa kuendesha gari kwa njia salama. Wazazi wengi wamechukua hatua kama hiyo kuhusu matumizi ya Intaneti. Kanuni za Biblia zifuatazo zitakusaidia.

“Kila mtu aliye mwerevu atatenda kwa ujuzi.” (Methali 13:16) Wazazi ambao watoto wao wanatumia Intaneti wanahitaji kujua mambo ya msingi kuhusu Intaneti na kujua watoto wao wanafanya nini wanapotuma ujumbe mfupi, wanapofungua tovuti, au kufanya mambo mengine kwenye Intaneti. “Usikate kauli kwamba wewe ni mzee sana au huna elimu ya kutosha kujifunza,” anasema Marshay, mama mwenye watoto wawili. “Usiachwe nyuma na tekinolojia.”

“Utafanya ukuta wa ukingoni kwa ajili ya dari lako [tambarare], . . . kwa sababu mtu anaweza kuanguka kutoka hapo.” (Kumbukumbu la Torati 22:8) Watu wanaotoa huduma za Intaneti na programu za kompyuta wametengeneza programu zinazoweza kuchuja au kuzuia ujumbe unaokuambia ufungue tovuti zisizofaa. Programu fulani zinaweza hata kumzuia mtoto asitoe habari za kibinafsi kama vile jina au anwani yake. Hata hivyo, mzazi anapaswa kujua kwamba vichujio hivyo havichuji habari zote mbaya. Pia, watoto wengi wenye umri mkubwa walio na ujuzi wa kompyuta wanaweza kujua jinsi ya kuepuka programu hizo.

“Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Uchunguzi uliofanywa nchini Uingereza ulionyesha kwamba kijana 1 kati ya 5 hivi aliye na umri wa kati ya miaka 9 na 19 anaweza kutumia Intaneti katika chumba chake cha kulala. Kuweka kompyuta mahali palipo wazi kunawasaidia wazazi kuchunguza kile ambacho watoto wao wanafanya kwenye Intaneti na kunaweza kuwatia moyo watoto wajiepushe na vituo visivyofaa.

“Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Waefeso 5:15, 16) Weka wakati ambao watoto wanaweza kutumia Intaneti, muda wanaopaswa kuitumia, na vituo ambavyo wanapaswa kufungua na vile ambavyo hawapaswi. Zungumzia sheria zako pamoja na watoto wako, na uhakikishe kwamba wamezielewa.

Bila shaka, huwezi kuwachunguza watoto wako wasipokuwa nyumbani. Hivyo, ni muhimu kuwafundisha kanuni zinazofaa ili wafanye maamuzi yenye hekima wakati ambapo wewe uko mbali nao. * (Wafilipi 2:12) Eleza waziwazi matokeo ya kuvunja sheria zako kuhusiana na Intaneti. Kisha tekeleza sheria hizo.

“[Mama mzuri] anaangalia shughuli za nyumba yake.” (Methali 31:27) Chunguza jinsi watoto wako wanavyotumia Intaneti na uwaeleze kwamba utakuwa unawachunguza. Kufanya hivyo si kuingilia faragha yao. Kumbuka kwamba Intaneti hutumiwa na watu wote. Shirika la Upelelezi la Marekani linapendekeza kwamba wazazi wanapaswa kuchunguza kwa ukawaida akaunti za watoto wao za Intaneti, barua-pepe zao na tovuti ambazo wanafungua.

“Uwezo wa kufikiri utakutunza, utambuzi utakulinda, ili kukukomboa kutoka katika njia mbaya, na kutoka kwa mtu anayesema mambo mapotovu.” (Methali 2:11, 12) Huwezi kuchunguza jinsi mtoto wako anavyotumia Intaneti kila wakati. Hivyo, viwango unavyofundisha, na mfano unaoweka, zitawalinda watoto wako hata zaidi. Kwa hiyo, tenga wakati wa kuzungumza na watoto wako kuhusu hatari za Intaneti. Njia bora zaidi ya kuwalinda watoto wako dhidi ya hatari za Intaneti ni kuwasiliana nao waziwazi. Tom, baba Mkristo anasema hivi: “Tulizungumza na wavulana wetu kuhusu watu ‘wabaya’ kwenye Intaneti. Pia tuliwaeleza ponografia ni nini, kwa nini wanapaswa kuiepuka, na kwa nini hawapaswi kamwe kuwasiliana na watu wasiojua.”

Unaweza Kuwalinda Watoto Wako

Jitihada zinahitajiwa ili kuwalinda watoto wako kutokana na hatari za Intaneti, na njia ya kupata habari kupitia vifaa vya elektroniki inabadilika kila mara. Huenda tekinolojia mpya ikawa na faida na hatari nyingi sana kwa watoto. Wazazi wanaweza kuwatayarisha jinsi gani watoto wao kwa ajili ya hatari watakazokabili wakati ujao? “Hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi,” inasema Biblia.—Mhubiri 7:12.

Wasaidie watoto wako kuwa na hekima. Pia, wasaidie waelewe jinsi ya kuepuka hatari za Intaneti na jinsi ya kuitumia kwa njia inavyofaa. Hivyo, Intaneti inaweza kuwa kifaa kizuri ambacho hakitahatarisha usalama wa watoto wako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Wazazi wanapaswa kukumbuka kwamba vijana wengi wanaweza kutumia Intaneti kupitia simu za mkononi na vifaa vingine vya mkononi, na pia michezo fulani ya video.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Huko Uingereza, asilimia 57 ya vijana walio na umri wa kati ya miaka 9 na 19 wanaotumia Intaneti kila juma wamepata ponografia; hata hivyo, ni asilimia 16 tu ya wazazi wanaoamini kwamba mtoto wao ameona ponografia kwenye Intaneti

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Wataalamu wanaamini kwamba huenda kila siku watu wapatao 750,000 wanaovizia watoto ili wafanye nao ngono wanatumia vituo vya maongezi na vituo vya kuwatafutia watu wachumba

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Nchini Marekani, asilimia 93 ya vijana wenye umri wa kati ya miaka 12 na 17 wanatumia Intaneti

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Je, unaweza kumfundisha mtoto wako jinsi ya kutumia Intaneti kwa njia inayofaa?