Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maji Yanayoongoza Kwenye Uzima

Maji Yanayoongoza Kwenye Uzima

Maji Yanayoongoza Kwenye Uzima

Yesu alikuwa akisafiri kupitia Samaria, kaskazini ya Yerusalemu. Alikuwa mchovu na mwenye kiu. Akiwa ameketi kando ya kisima, alimwomba mwanamke Msamaria amchotee maji. Mwanamke huyo alishangaa kwamba Myahudi angemwomba maji, kwa sababu katika karne ya kwanza, Wayahudi na Wasamaria hawakupendana.

Mwanamke huyo aliyeshangaa alimwuliza Yesu hivi: “Wewe, ujapokuwa Myahudi, unawezaje kuniomba maji ya kunywa, na mimi ni mwanamke Msamaria?”

Yesu akamjibu hivi: “Kama ungalijua zawadi ya bure inayotoka kwa Mungu, na ni nani ambaye anakuambia, ‘Nipe maji ninywe,’ ungalimwomba, naye angalikupa maji yaliyo hai.”

Kisha Yesu akamfafanulia zaidi hivi: “Kila mtu anayekunywa maji haya atapatwa na kiu tena. Yule atakayekunywa maji ambayo nitampa hatapatwa na kiu hata kidogo, lakini maji ambayo nitampa yatakuwa chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.”—Yohana 4:1-15.

Yesu alikuwa akizungumzia maji gani?

BIBLIA inamwita Muumba wetu, Yehova Mungu, “chemchemi ya maji yaliyo hai.” (Yeremia 2:13) Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu, na kuwepo kwetu kunategemea kunywa maji anayotoa, ya kimwili na ya kiroho.

Sasa kuliko wakati mwingine wowote kuna uhitaji wa kupata mwongozo wa kiroho. Kwa kweli, tunaweza kusema kwamba kuna ukame wa kiroho duniani. Watu wana kiu cha kupata majibu ya maswali kama vile: Wafu wako wapi? Je, kuna tumaini la kuishi pamoja nao tena? Kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke? Je, watu watapata kitulizo kutokana na vita, uhalifu, njaa, na magonjwa wakati ujao? Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba majibu yanayoridhisha ya maswali hayo yanaweza kupatikana katika “maji” yenye kuburudisha ya Neno la Mungu, Biblia.

Yesu alipozungumza na mwanamke Msamaria kisimani, kama ilivyofafanuliwa hapo awali, alitaja maji yenye uhai ya kweli ambayo tunapata kwenye Neno la Mungu. Mashahidi wa Yehova wanakualika unywe maji safi ya kweli. Mwaliko huo unatajwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia: “Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.

Ili kujifunza mengi zaidi jinsi Ufalme wa Mungu utakavyowafaidi wanadamu, wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika Jumba la Ufalme lililo karibu nawe au uwaandikie kwa kutumia anwani ifaayo kati ya zile zilizoorodheshwa katika ukurasa wa 5 wa gazeti hili. Unaweza pia kutazama Tovuti yao www.watchtower.org.

[Sanduku katika ukurasa wa 8, 9]

JE, DINI IMEKATA KIU CHA WANADAMU?

Kwenda kanisani au kudai tu kuwa mtu wa kidini hakuwezi kumfanya mtu apate maji ya kweli yenye kuburudisha. Ukweli ni kwamba dini nyingi kubwakubwa za leo zimeongeza matatizo ya wanadamu badala ya kuyatatua. Fikiria mfano mmoja: Nyakati za vita, Wakatoliki wamewaua Wakatoliki, Waprotestanti wamewaua Waprotestanti, na pande zote mbili zilimwomba Mungu ili washinde!

Kwa kuongezea, kuna ripoti nyingi za makosa yanayofanywa na makanisa, yanayohusu viongozi wa kidini wanaotumia pesa vibaya au kuwatendea watoto vibaya kingono. Kwa kweli, maji yanayotolewa na dini nyingi yamechafuliwa. (Ufunuo 17:4-6; 18:1-5) Hali iko kama inavyoelezwa katika Biblia kwenye andiko la Tito 1:16: “Wao hutangaza hadharani kwamba wanamjua Mungu, lakini humkana kwa matendo yao.” Kwa kiwango kikubwa, dini haijafanya mengi ili kukata kiu cha wanadamu katika siku hizi zenye ukame wa kiroho.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? chenye kurasa 224 na sura 19, kina majibu ya Biblia kwa maswali ya msingi kama vile:

“Mungu ana kusudi gani kwa dunia?”

“Wafu wako wapi?”

“Je, tunaishi katika ‘siku za mwisho’?”

Kwa nini Mungu anawaacha watu wateseke?”

[Picha katika ukurasa wa 9]

Unaweza kupata ‘maji ya kweli’ katika Jumba la Ufalme lililo karibu nawe