Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sayari Iliyo Hai

Sayari Iliyo Hai

Sayari Iliyo Hai

DUNIA ina viumbe wengi sana wa aina mbalimbali, huenda hata kuna mamilioni ya jamii za viumbe. Viumbe wengi wanaoishi kwenye udongo, hewa, na maji, ni wadogo sana hivi kwamba hawawezi kuonekana kwa macho. Kwa mfano, kwenye gramu moja ya mchanga kulipatikana jamii 10,000 hivi za bakteria bila kutaja idadi kamili ya vijidudu! Vijidudu fulani vimepatikana kilomita tatu hivi chini ya ardhi!

Pia, anga limejaa viumbe hai, na hilo halimaanishi tu ndege, popo, na wadudu. Ikitegemea msimu, anga hujaa chavua na viumbe wengine wenye chembe moja, kutia ndani mbegu, na katika maeneo fulani maelfu ya vijidudu vya aina mbalimbali. “Hilo linafanya unamna-namna wa vijidudu hewani uwe sawa na ule wa vijidudu kwenye udongo,” linasema gazeti Scientific American.

Wakati huohuo, si rahisi kuchunguza bahari yote kwa kuwa ili kuchunguza vilindi vya bahari, wanasayansi wanahitaji kutumia tekinolojia ghali sana. Hata matumbawe ambayo yanaweza kufikiwa kwa urahisi na ambayo yamechunguzwa kwa undani, huenda bado yana mamilioni ya jamii za viumbe ambao hawajagunduliwa.

Hata hivyo, tunajua kwamba Dunia imejaa viumbe wengi sana hivi kwamba wamebadili kemikali katika sayari, hasa katika sehemu ya dunia iliyo na uhai. Kwa mfano, katika bahari, kalisi-kaboneti iliyo kwenye makoa na marijani inasaidia kusawazisha kemikali majini “kama tu dawa ya kutuliza kiungulia inavyosawazisha asidi tumboni,” inasema ripoti ya Shirika la Kitaifa la Usimamizi wa Bahari na Anga la Marekani. Mimea na miani yenye chembe moja inayopatikana katika maziwa na bahari, husaidia kudhibiti viwango vya kaboni dioksidi na oksijeni majini na hewani. Bakteria na kuvu hufanya kazi pamoja kumeng’enya madini katika udongo ili mimea iweze kuifyonza. Naam, dunia imeitwa kwa kufaa sayari iliyo hai.

Hata hivyo, uhai haungekuwepo duniani kama hakungekuwa na vipimo fulani sahihi kabisa katika maeneo fulani. Baadhi ya vipimo hivyo havikujulikana kwa undani hadi karne ya 20. Vipimo hivyo sahihi vinatia ndani mambo yafuatayo:

1. Mahali dunia ilipo katika kikundi cha nyota cha Kilimia na katika mfumo wa jua, kutia ndani mzunguko wa dunia, mwinamo wake, mwendo wa mzunguko, na mwezi

2. Nguvu za sumaku ya dunia na anga ambazo hutenda kama ngao maradufu

3. Maji mengi sana

4. Mizunguko ya asili ambayo husafisha na kurekebisha dunia

Unaposoma kuhusu mambo hayo katika makala zinazofuata, jiulize: ‘Je, mambo yaliyo duniani yalijitokeza yenyewe au yalitokezwa na mbuni mwenye akili? Ikiwa yalitokezwa na mbuni mwenye akili, Muumba alikuwa na kusudi gani alipoiumba dunia?’ Makala ya mwisho katika mfululizo huu itajibu swali hilo.

[Sanduku katika ukurasa wa 3]

“HATUPASWI HATA KUFIKIRI KUNA MUUMBA”

Ingawa uthibitisho uliopo unaonyesha kwamba ulimwengu umebuniwa kwa njia nzuri sana hivi kwamba haiwezekani kuwa ulijitokeza tu, wanasayansi wengi wanakataa kuamini kwamba kuna Muumba. Si kwamba sayansi inawalazimisha watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu “wakubali ufafanuzi kwamba [ulimwengu] ulijitokeza,” anasema mwanamageuzi Richard C. Lewontin. Badala yake, anasema, wanachochewa na “uamuzi waliofanya mapema . . . kwamba [ulimwengu] ulijitokeza,” na wameazimia kubuni “dhana itakayowasaidia kuamini [ulimwengu] ulijitokeza.” Anaongezea hivi akizungumza kuhusu wanasayansi kwa ujumla: “Kwa kuwa wazo la kwamba ulimwengu ulijitokeza ndilo wazo pekee linalopatana na akili, hatupaswi hata kufikiri kuna Muumba.”

Je, ni jambo la hekima kufikia mkataa huo sugu hasa ikiwa uthibitisho mwingi unaonyesha kwamba kuna Muumba? Unaonaje?—Waroma 1:20.