Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dunia Ipo Mahali Bora Zaidi

Dunia Ipo Mahali Bora Zaidi

Dunia Ipo Mahali Bora Zaidi

KATIKA nchi nyingi anwani hutia ndani nchi, jiji, na barabara. Acheni basi tuseme “nchi” ya dunia ni kikundi cha nyota cha Kilimia, “jiji” lake ni mfumo wa jua, yaani, jua pamoja na sayari zake, kisha tuseme “barabara” ya dunia ni mzunguko wake katika mfumo wa jua. kwa sababu ya maendeleo katika elimu ya nyota na fizikia, wanasayansi wamefahamu zaidi kwa nini dunia ipo mahali bora zaidi katika ulimwengu.

Kwanza, “jiji” letu, yaani, mfumo wetu wa jua, upo katika eneo la kikundi cha nyota cha Kilimia ambapo wanasayansi wengi wanasema ndipo tu panaweza kutegemeza uhai. Eneo hilo liko umbali wa miaka ya nuru 28,000 kutoka katikati ya kikundi hicho cha nyota na lina kiwango kinachofaa cha kemikali zinazohitajiwa kutegemeza uhai. Mbali zaidi na eneo hilo kemikali hizo ni chache zaidi; karibu zaidi na eneo hilo, ni hatari zaidi kwa sababu kuna miale hatari na vitu vingine. Gazeti Scientific American linasema, “tunaishi katika eneo bora zaidi.”

“Barabara” Bora Kabisa

Dunia iko katika “barabara” bora zaidi, yaani, njia ambayo dunia hutumia kulizunguka jua. Njia hiyo, ambayo iko umbali wa kilomita milioni 150 kutoka kwa jua, inapitia eneo ambalo wanasayansi wanasema ndilo eneo lililo karibu na jua linalofaa zaidi kwa uhai, mahali ambapo hakuna baridi wala joto kupita kiasi. Isitoshe, kwa kuwa dunia hulizunguka jua kwa kutumia njia inayokaribia kuwa na umbo la duara, umbali wake kutoka kwa jua hubaki vilevile mwaka mzima.

Wakati huohuo, jua ndiyo “chanzo cha nishati kinachofaa kabisa.” Liko imara, lina ukubwa unaofaa, na linatoa kiasi kinachofaa cha nishati. Kwa kufaa, jua limeitwa “nyota ya pekee sana.”

Jirani Bora Kabisa

Ikiwa ungeambiwa uchague jirani anayefaa zaidi kwa ajili ya dunia, hungepata jirani bora kuliko mwezi. Kipenyo chake ni robo tu ya kile cha dunia. Hivyo, unapolinganishwa na miezi ya sayari nyingine zilizo katika mfumo wa jua, mwezi wa dunia ni mkubwa sana ukilinganishwa na dunia. Hata hivyo, kuna sababu nzuri kwa nini una ukubwa huo.

Sababu moja ni kwamba mwezi huchangia sehemu kubwa katika kufanya maji yajae na kupwa baharini, jambo ambalo husaidia sana katika kuisafisha dunia. Pia, mwezi huchangia katika kufanya dunia izunguke katika mhimili wake bila kuyumbayumba. Kama mwezi uliobuniwa kwa njia inayofaa haungekuwepo, sayari yetu ingeyumbayumba kama pia inayozunguka, huenda hata nyakati nyingine ingepinduka na kulalia upande mmoja! Mabadiliko katika hali ya hewa, kiwango cha maji baharini, na mabadiliko mengine yangesababisha misiba.

Mwinamo na Mzunguko Bora Kabisa wa Dunia

Kwa kuwa dunia imeinama kwa digrii 23.5, hilo hufanya kuwe na majira mbalimbali katika mwaka, viwango mbalimbali vya joto, na kufanya kuwe na maeneo mbalimbali ya hali ya hewa. “Mwinamo wa sayari yetu katika mhimili wake unaonekana kuwa ‘bora kabisa’ ili kuendeleza uhai,” kinasema kitabu Rare Earth—Why Complex Life Is Uncommon in the Universe.

Pia, urefu wa mchana na usiku ni sahihi sana kwa sababu ya mzunguko wa dunia. Ikiwa dunia ingezunguka kwa muda mrefu zaidi, upande wa dunia unaoelekea jua ungeunguzwa na ule upande mwingine ungeganda. Vivyo hivyo, ikiwa siku zingekuwa fupi zaidi, hata kwa saa chache tu, kuzunguka huko kasi kungesababisha pepo zenye nguvu sana na zisizokoma na vilevile madhara mengine.

Naam, kila kitu kuhusu sayari yetu, iwe ni mahali dunia ilipo, au mwendo wa kuzunguka kwake, au mwezi wake, huthibitisha kwamba dunia ilibuniwa na Muumba mwenye hekima. * Mwanafizikia na mwanamageuzi Paul Davies anasema: “Hata wanasayansi ambao wanaamini kwamba hakuna Mungu watasifu sana ukubwa, utukufu, upatano, uzuri, na hekima iliyohusika katika kutokeza ulimwengu.”

Je, hekima hiyo yote inayoonekana ulimwenguni ilijitokeza tu, au inaonyesha kuna mbuni mwenye akili? Fikiria swali hilo unaposoma makala fupi inayofuata, ambayo inazungumzia ngao mbili za ajabu zinazokinga uhai duniani kutokana na vitu hatari vinavyotoka angani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ili ulimwengu wote uendelee kuwapo, kani nne za msingi zinahitajika: nguvu za uvutano, sumaku-umeme, na kani za nyuklia zenye nguvu na dhaifu. Zote zimepimwa kwa usahihi wa hali ya juu.—Ona sura ya 2 katika kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

JE, UNASONGA HARAKA KULIKO RISASI?

Utakapomaliza kusoma sanduku hili, utakuwa umesafiri maelfu ya kilomita bila kuhisi kana kwamba unarushwa-rushwa! Fikiria mambo yafuatayo.

Dunia ina mzingo wa kilomita 40,000 na inazunguka mara moja kila saa 24. Hivyo, maeneo yaliyo kwenye ikweta au karibu yanasonga kwa kilomita 1,600 hivi kwa saa. (Bila shaka, ncha za dunia hazisongi, zinazunguka hapohapo.)

Dunia yenyewe inazunguka jua kwa kilomita 30 hivi kwa sekunde, na mfumo wa jua kwa ujumla unazunguka kitovu cha Kilimia kwa mwendo wenye kustaajabisha wa kilomita 249 kwa sekunde. Kwa kulinganishwa, risasi husafiri kwa mwendo unaopungua kilomita mbili kwa sekunde.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Milky Way: NASA/JPL/Caltech

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Earth: Based on NASA/Visible Earth imagery