Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakati Wako Ujao Umeamuliwa Mapema?

Je, Wakati Wako Ujao Umeamuliwa Mapema?

Maoni ya Biblia

Je, Wakati Wako Ujao Umeamuliwa Mapema?

Watu wengi wanaamini kwamba maisha yao na wakati wao ujao umeamuliwa mapema na mtu fulani mwenye nguvu sana. Wanahisi kwamba tangu kuzaliwa hadi kufa, sote tunaishi maisha ambayo tayari yameandikwa mapema katika akili ya Mungu. Wanasema kwamba ‘Mungu ni mweza-yote na anajua kila kitu, kwa hiyo bila shaka lazima awe anajua kila kitu kuhusu wakati uliopita, wakati uliopo, na wakati ujao.’

UNA maoni gani? Je, Mungu anaamua mapema jinsi maisha yetu na mwisho wetu utakavyokuwa? Kwa maneno mengine, je, uhuru wa kuchagua ni halisi au ni jambo la kuwaziwa tu? Biblia inasema nini?

Je, Mungu Anajua Mambo Yote Yatakayotukia?

Biblia inatueleza waziwazi kwamba Mungu anajua mambo fulani mapema. Anajua “tangu mwanzo ule mwisho,” linasema andiko la Isaya 46:10. Hata alitumia wanadamu kuandika unabii mwingi. (2 Petro 1:21) Kwa kuongezea, kila wakati unabii huo umetimia kwa kuwa Mungu ana hekima na nguvu za kutimiza kila jambo linalohusiana na unabii huo. Hivyo, Mungu anaweza kujua mambo mapema na pia anaweza kuamua mapema jinsi mambo yatakavyokuwa anapochagua kufanya hivyo. Lakini je, Mungu huamua mapema mambo ya yatakayompata kila mwanadamu au hata idadi kamili ya wale watakaookolewa? Biblia haisemi hivyo.

Biblia inafundisha kwamba Mungu huchagua mambo ya wakati ujao anayotaka kuamua mapema. Kwa mfano, Mungu alitabiri kwamba “umati mkubwa” wa wanadamu waadilifu ungeokoka uharibifu wa waovu mwishoni mwa mfumo huu wa mambo. (Ufunuo 7:9, 14) Ingawa hivyo, ona kwamba Mungu hakusema idadi hususa ya umati huo mkubwa. Kwa nini? Yeye haamui mapema mambo yatakayowapata watu mmoja-mmoja. Mungu ni kama baba mwenye upendo wa familia kubwa. Anajua kwamba angalau baadhi ya watoto Wake watakubali upendo Wake, lakini haamui mapema idadi yao.

Hebu linganisha jinsi Mungu anavyotumia uwezo wa kuamua mambo mapema na jinsi anavyotumia nguvu zake. Akiwa Mweza-Yote, Mungu ana nguvu zisizo na mipaka. (Zaburi 91:1; Isaya 40:26, 28) Lakini je, anatumia nguvu zake bila kuzidhibiti? Hapana. Kwa mfano, aliamua kutotumia nguvu zake dhidi ya Wababiloni, waliokuwa maadui wa taifa la Israeli la kale, hadi wakati uliofaa. Mungu alisema: “Niliendelea kujizuia.” (Isaya 42:14) Kanuni hiyohiyo inatumika kuhusu uwezo wake wa kujua na kuamua mambo mapema. Yehova anajizuia ili aturuhusu tutumie uhuru wa kuchagua aliotupa.

Mungu anapodhibiti uwezo wake, haimaanishi kwamba yeye si mkamilifu. Badala yake, hilo linatukuza ukuu wake na linatuvuta kwake kwani linaonyesha kwamba yeye si mtawala mwenye nguvu tu anayejua kila kitu, bali pia yeye ni mwenye upendo na anaheshimu uhuru wa kuchagua wa viumbe wake wenye akili.

Kwa upande mwingine, ikiwa Mungu anaamua mapema kila kitu hata kila aksidenti mbaya au jambo lolote ovu ambalo limewahi kutukia, je, kwa kufaa hatungemlaumu kwa sababu ya taabu na mateso yote yanayotokea ulimwenguni? Hivyo tukichunguza mambo kwa undani, fundisho la kwamba Mungu huamua mambo mapema halimheshimu Mungu bali linamletea suto. Linamfanya aonekane kuwa mkatili, asiye na haki, na asiye na upendo, mambo ambayo ni kinyume cha yale Biblia inasema kumhusu.—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Uamuzi Ni Wako

Kupitia mtumishi wake Musa, Mungu aliliambia hivi taifa la Israeli: “Nimeweka uzima na kifo mbele yako, . . . nawe lazima uchague uzima . . . kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye; kwa maana yeye ni uhai wako na urefu wa siku zako.” (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Ikiwa Mungu angekuwa ameamua mapema Waisraeli ambao wangempenda na kupata uhai na wale ambao wangempuuza na hivyo kufa, maneno Yake hayangekuwa ya kweli au yenye faida yoyote. Je, unaamini kwamba Mungu “mpenda-haki” na aliye mfano bora zaidi wa upendo angetenda hivyo bila kufikiria?—Zaburi 37:28; 1 Yohana 4:8.

Himizo la Mungu kwa watumishi wake kwamba wachague uzima linatuhusu leo hata zaidi, kwa kuwa kutimizwa kwa unabii wa Biblia kunaonyesha kwamba tunakaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo haraka sana. (Mathayo 24:3-9; 2 Timotheo 3:1-5) Tunaweza kuchagua uzima jinsi gani? Tunafanya hivyo kama Waisraeli wa kale walivyofanya.

Unaweza ‘Kuchagua Uzima’ Jinsi Gani?

Tunachagua uzima kwa “kumpenda Yehova,” kwa “kuisikiliza sauti yake,” na kwa “kushikamana naye.” Bila shaka, tunaweza kufanya mambo hayo tu ikiwa tunamfahamu Mungu na kuelewa matakwa yake kwa ajili yetu. Akisali kwa Mungu, Yesu Kristo alisema: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Italiki ni zetu; Yohana 17:3, Union Version.

Ujuzi huo wenye thamani unaweza kupatikana katika Biblia Takatifu, ambayo kwa kufaa inaitwa Neno la Mungu. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16) Kwa kweli, zawadi hiyo ya kiroho ni uthibitisho unaoonekana wa kwamba Mungu hajatuamulia mapema wakati wetu ujao bali anataka tufanye maamuzi yanayotegemea ujuzi aliotoa.—Isaya 48:17, 18.

Kupitia Biblia, ni kana kwamba Mungu anatuambia hivi: ‘Hili ndilo kusudi langu kwa wanadamu na dunia, na hivi ndivyo mnayopaswa kufanya ili kupata uzima wa milele. Sasa ni juu yako kuamua ikiwa utanisikiliza au kunipuuza.’ Ndiyo, Mungu amesawazisha kikamili uwezo wake wa kuamua mambo mapema na kuheshimu uhuru wetu wa kuchagua! Je, utachagua uzima “kwa kuisikiliza sauti yake [Mungu] na kwa kushikamana naye”?

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Ni kwa kadiri gani Mungu anatumia uwezo wake wa kujua mambo mapema?—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Isaya 46:10.

▪ Kwa nini Mungu haamui mapema kila jambo, kutia ndani mambo mabaya yanayowapata watu?—Kumbukumbu la Torati 32:4.

▪ Ni nini kitakachoamua wakati wetu ujao?—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Biblia inafundisha kwamba Mungu huchagua mambo ya wakati ujao anayotaka kuamua mapema