Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dyslexia Haijanizuia Kufikia Miradi Yangu

Dyslexia Haijanizuia Kufikia Miradi Yangu

Dyslexia Haijanizuia Kufikia Miradi Yangu

Limesimuliwa na Michael Henborg

Nina tatizo la kujifunza linaloitwa “dyslexia”. Tatizo hilo, ambalo pia limewaathiri baba, mama, na ndugu zangu wadogo watatu, limefanya iwe vigumu kwangu kusoma lugha yangu ya mama ya Kidenishi, na nilikuwa na matatizo mengi sana shuleni. Hata hivyo, nimesaidiwa na kutiwa moyo sana, hasa na familia yangu.

KUMEKUWA na vizazi vinne vya Mashahidi wa Yehova katika familia yetu, na sikuzote kusoma, hasa kusoma Biblia na vichapo vya Biblia, kumekuwa sehemu muhimu ya maisha yetu. Pia, mimi na ndugu yangu mdogo Flemming tuliandamana na Baba kwa ukawaida kwenye utumishi wa Kikristo, na hilo lilitufanya tuthamini umuhimu wa kusoma na kuandika vizuri.

Nilisoma kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! nilipokuwa mtoto. Ilinichukua saa nyingi hata kufikia saa 15 kumaliza gazeti moja! Isitoshe, nilianza mradi wa kusoma Biblia nzima. Pia nilijiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ambayo inafanywa katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Shule hiyo inawazoeza wanafunzi kusoma na kuandika vizuri na kutoa hotuba mbele ya wasikilizaji. Maandalizi hayo yote yalinisaidia sana katika kukabiliana na dyslexia. Hata hivyo, wakati huo sikujua kwamba ningekabili magumu mengi zaidi. Acheni nieleze.

Kujifunza Kiingereza

Mnamo 1988, nilipokuwa na umri wa miaka 24, nilianza kutumika kama painia, yaani, mtumishi wa wakati wote wa habari njema. Kwa kuwa Denmark ina wahamiaji wengi, nilitaka kuwafundisha kweli za Biblia. Ili nifanye hivyo kwa njia inayofaa, nilihitaji kujifunza Kiingereza. Huo ulikuwa mradi mgumu sana kwangu. Hata hivyo, kupitia subira na masomo ya ziada, nilifanya maendeleo polepole, na baada ya muda niliweza kuwahubiria habari njema ya Ufalme wa Mungu wahamiaji waliozungumza Kiingereza katika mji wa nyumbani wa Copenhagen. Kwa kweli, nilifanya makosa mengi sana nilipokuwa nikizungumza, lakini sikuruhusu hilo linizuie.

Pia, kuelewa Kiingereza kulinisaidia kutumika kama mfanyakazi wa kujitolea katika miradi ya ujenzi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi mbalimbali. Kwanza nilitumwa Ugiriki, na baadaye nikasaidia katika ujenzi wa ofisi ya tawi ya Madrid, Hispania.

Kwa sababu nilitaka kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri, niliomba kujiunga na Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ya Mashahidi wa Yehova. Shule hiyo hutoa mazoezi ya pekee kwa majuma manane kwa wanaume Wakristo waseja ambao wako tayari kukubali migawo katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa habari njema. (Marko 13:10) Nilikaribishwa kuhudhuria darasa la Kiingereza nchini Sweden.

Darasa hilo lilianza Septemba 1, 1994 (1/9/1994). Nilitaka kujitayarisha vizuri, kwa hiyo nilijifunza Kiingereza kwa saa nne kila siku kwa miezi minane, na nikajiunga na kutaniko la Kiingereza. Kisha, shule ilipoanza, sikuruhusu tatizo langu linizuie kufanya maendeleo. Kwa mfano, walimu walipouliza maswali, mara nyingi niliinua mkono ingawa sikuwa na hakika sikuzote kuhusu maneno sahihi ya kutumia. Baada ya kuhitimu, nilitumwa Copenhagen nikatumike nikiwa painia. Ingawa nilikuwa nimepata ugumu kujifunza Kiingereza, ningekabili changamoto kubwa zaidi.

Kujifunza Kitamili

Mnamo Desemba (Mwezi wa 12) 1995, nilipewa mgawo wa kutumika katika kutaniko la Kitamili katika mji wa Herning, huko Denmark. Nilifikiri kwamba Kitamili ni kati ya lugha ngumu zaidi ulimwenguni. Lugha hiyo ina herufi 31, na pia ina konsonanti zilizounganishwa na irabu ili kutokeza herufi za pekee. Zote ni 250 hivi kwa ujumla!

Mwanzoni, nilitoa hotuba katika Kidenishi na zikatafsiriwa katika Kitamili. Mwishowe nilipoanza kuzungumza Kitamili, sidhani kuna mtu aliyenielewa. Hata hivyo, watu walinisikiliza kwa makini ingawa wengi wao waliona ni kana kwamba nilikuwa nikizungumza kwa njia yenye kuchekesha. Ili nijifunze haraka zaidi, niliamua kuhamia Sri Lanka, nchi ambayo Kitamili kinazungumzwa na mamilioni ya watu.

Nilipofika Sri Lanka mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1996, kulikuwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe. Kwa muda fulani, niliishi katika mji wa Vavuniya uliokuwa kati ya vikundi viwili vilivyokuwa vikipigana. Mashahidi wa eneo hilo hawakuwa na vitu vingi vya kimwili, lakini walikuwa na upendo na ukarimu mwingi sana, nao walijaribu sana kunifundisha Kitamili. Watu ambao si Mashahidi walivutiwa sana kwamba mzungu pekee katika eneo lao alikuwa akijaribu kuzungumza lugha yao. Kwa kuwa walithamini sana mambo na walikuwa wanyenyekevu, ilikuwa rahisi zaidi kwangu kuzungumza nao kuhusu Biblia.

Mnamo Januari 1997, nilihitaji kurudi Denmark, na mwaka uliofuata, nilimwoa Camilla, ambaye alikuwa painia. Nilitamani sana kurudi Sri Lanka, hivyo, Desemba 1999, nilirudi nikiwa pamoja na mke wangu. Muda si muda, tulikuwa tukijifunza Biblia na familia na watu kadhaa, na tuliandamana na Mashahidi wa eneo hilo kwenye mafunzo yao ya Biblia. Tulikuwa tumezama kabisa katika huduma na lugha ya huko.

Machi (Mwezi wa 3) 2000, ilibidi turudi Denmark. Ilikuwa vigumu sana kuwaacha Mashahidi wenzetu na wanafunzi wa Biblia kwani tuliwapenda sana. Lakini kulikuwa na kazi nyingi zaidi mbele yetu, kutia ndani kazi ngumu ya kujifunza lugha nyingine!

Twaanza Kujifunza Kilatvia

Mnamo Mei 2002, mimi na Camilla, tukiwa tumeoana kwa miaka minne, tulialikwa tutumike kama wamishonari huko Latvia, nchi ya Ulaya iliyo mashariki ya Denmark. Camilla alijifunza Kilatvia haraka na angeweza kuzungumza baada ya majuma sita tu! Lakini ilinichukua muda mrefu zaidi. Kwa kweli, hadi leo ninahisi kwamba sijafanya maendeleo makubwa, ingawa nimesaidiwa sana. Hata hivyo, nimeazimia kuendelea kujifunza lugha hiyo. *

Camilla anaendelea kunitegemeza sana nasi tunafurahia utumishi wetu wa umishonari. Tumejifunza Biblia na watu wengi sana wenye uthamini. Ninaposahau maneno au ninapovunja kanuni za sarufi, Mashahidi na wanafunzi wa Biblia hujaribu kunielewa kwa subira na kunisaidia. Hilo hunifanya niwe na ujasiri ninapohubiri na pia ninapotoa hotuba kwenye mikutano ya Kikristo.

Kwa nini nimekubali kazi ngumu ya kujifunza lugha nyingine ingawa ni vigumu sana kwangu kufanya hivyo? Kwa ufupi, si kwa sababu ninapenda lugha hizo bali kwa kuwa ninawapenda watu. Ni pendeleo kubwa sana kumsaidia mtu amjue Mungu wa kweli, Yehova, na kumkaribia. Na kama vile wamishonari wengi wamegundua, mara nyingi ni rahisi zaidi kufanya hivyo unapozungumza na watu katika lugha yao ya mama, lugha inayogusa mioyo yao.

Mimi na mke wangu tumewasaidia watu wengi wapate ujuzi sahihi wa kweli za Biblia. Hata hivyo, hatuwezi kujisifu. Badala ya hivyo, tunamshukuru Yehova kwa matokeo mazuri ambayo tumepata. Kwa kweli, sisi tunapanda na kutia maji kwenye mbegu za kweli ya Biblia; Mungu ndiye huzikuza.—1 Wakorintho 3:6.

Tatizo Linapokuwa na Faida

Ingawa dyslexia limekuwa tatizo kwangu, pia limenisaidia. Jinsi gani? Ninapotoa hotuba katika kutaniko, situmii sana maandishi na hivyo ninawatazama wasikilizaji sana. Pia, mimi hutumia vielezi ambavyo hufanya iwe rahisi kwa watu kukumbuka. Hivyo, kwa njia fulani, hali yangu imenisaidia kukuza ustadi wangu wa kufundisha.

Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu, ili aviaibishe vitu vyenye nguvu.” (1 Wakorintho 1:27) Tatizo langu limenifanya kuwa ‘kitu dhaifu’ katika njia fulani. Hata hivyo, kama mimi na wengine wengi walivyojifunza, Yehova anaweza kufanya mengi zaidi kuliko kusawazisha tu upungufu wetu. Tunahitaji tu kujiwekea miradi yenye usawaziko, kutotazamia mengi, kusali ili kupata roho takatifu ya Mungu, na kufanya mambo tunayotaka kutimiza.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Baada ya kutumika kwa miaka sita huko Latvia, hivi karibuni Henborg na mke wake walipewa mgawo wa kutumika Ghana.

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

MAMBO YANAYOHUSIANISHWA NA DYSLEXIA

Dyslexia ni nini? Neno “dyslexia” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kutoweza kuzungumza vizuri.” Dyslexia ni hali inayomwathiri mtu katika maisha yake yote, na inatia ndani matatizo kadhaa yanayohusiana na lugha, hasa kusoma. Watu walio na dyslexia wana tatizo la kuhusianisha herufi na sauti inayowakilishwa na herufi hizo. Hata hivyo, huenda dalili zikatofautiana katika watu mbalimbali.

Ni nini kinachosababisha dyslexia? Bado haijulikani waziwazi chanzo chake ni nini, ingawa inaonekana kwamba hali hiyo inaweza kurithiwa. Ingawa uchunguzi unaonyesha ukuzi na utendaji usio wa kawaida katika ubongo, dyslexia haihusiani na werevu au kukosa tamaa ya kujifunza. Kinyume na hilo, watu walio na tatizo hilo wana ustadi katika mambo yasiyohitaji ujuzi mwingi wa lugha.

Dyslexia hutibiwa jinsi gani? Ni jambo muhimu kutambua tatizo hilo mapema. Mazoezi mazuri ya kujifunza lugha yanatia ndani kutumia hisi kadhaa, hasa kusikia, kuona, na kugusa. Ili wafanye maendeleo kulingana na uwezo wao, wanafunzi wengi wanahitaji kufundishwa kibinafsi. Huenda pia wakahitaji kusaidiwa kihisia kwa sababu ya matatizo wanayopata shuleni. Wakifundishwa vizuri na kufanya kazi kwa bidii, wanafunzi walio na dyslexia wanaweza kujifunza kusoma na kuandika vizuri. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 31 Mambo yaliyotajwa hapo juu yanategemea habari kutoka kwa Shirika la Kimataifa la Dyslexia. Pia, ona makala “Kuwasaidia Watoto Wenye Matatizo ya Kujifunza,” katika toleo la Januari 2009 la gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Shahidi mwenzangu huko Sri Lanka

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Camilla huko Latvia