Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupiga Mbinja—Njia ya Pekee ya “Kuzungumza”

Kupiga Mbinja—Njia ya Pekee ya “Kuzungumza”

Kupiga Mbinja—Njia ya Pekee ya “Kuzungumza”

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI MEXICO

▪ Kwenye eneo lenye milima la Oaxaca, Mexico, wakaaji wa eneo hilo wanaoitwa Mazatec hawana simu za mkononi au zingine zozote. Hata hivyo, wanaweza kuwasiliana wakiwa umbali wa kilomita mbili au zaidi, labda wanapokuwa wakifanya kazi kwenye mashamba ya kahawa yaliyo kwenye upande wa milima. Wanawezaje kufanya hivyo? Zamani za kale, Wamazatec walibuni mfumo wa lugha yao wa kupiga mbinja. Pedro, kijana Mmazatec anasema hivi: “Maneno katika Kimazateco yanatofautishwa kulingana na sauti. Hivyo, tunapopiga mbinja, tunaiga sauti na mtindo wa kuzungumza lugha. Sisi hupiga mbinja kupitia mdomo, si kwa kutumia vidole vyetu.” *

Rafiki ya Pedro anayeitwa Fidencio anaeleza faida za kupiga mbinja: “Tunatumia njia hii tunapowasiliana na mtu aliye mbali na kwa kawaida kwa mazungumzo mafupi. Kwa mfano, huenda baba alimtuma mwana wake dukani anunue chapati zinazoitwa tortilla lakini akasahau kumtuma nyanya. Ikiwa mvulana huyo yuko mbali hivi kwamba hawezi kusikia maneno, baba anaweza kumpigia mbinja na kumpa maagizo hayo.”

Pia, Mashahidi wa Yehova mara kwa mara wanapiga mbinja wanapowasiliana. Pedro anaeleza: “Ninapotembelea maeneo ya mbali na ninataka kumwomba ndugu yangu wa kiroho aandamane nami, sihitaji kwenda mpaka kwenye nyumba yake. Mimi hupiga mbinja tu.”

“Ili tujue ni nani ‘anayezungumza,’” anasema Pedro, “kila mtu ana njia yake ya kibinafsi ya kupiga mbinja. Kwa kawaida, ni wanaume peke yao katika jamii ya Mazatec wanaopiga mbinja. Huenda mwanamke akaelewa lugha hiyo na hata kuitumia katika familia lakini hataitumia kuwasiliana na mwanamume yeyote tu. Hiyo si tabia nzuri.”

Si Wamazatec peke yao wanaowasiliana kwa kupiga mbinja, kuna watu wengine wanaowasiliana kwa kupiga mbinja nchini China, Papua New Guinea, na katika Visiwa vya Canary. Watu hao kwa kawaida huishi kwenye maeneo ya milima na misitu mikubwa. Kwa kweli, huenda kuna lugha zaidi ya 70 za aina hiyo, na angalau lugha 12 zimefanyiwa uchunguzi.

Tunastaajabishwa na uwezo huo wa wanadamu wa kubuni. Hivyo ukiunganisha kipawa hicho na tamaa yetu ya kuwasiliana, hakuna jambo linaloweza kuzuia kubuni njia mpya za kuwasiliana.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza hivi: “Kwa kubadili mwendo, uzito, na sauti ya mbinja, Wamazatec wamefaulu kuwasilisha mawazo mbalimbali.”