Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimebarikiwa kwa Kumtanguliza Mungu

Nimebarikiwa kwa Kumtanguliza Mungu

Nimebarikiwa kwa Kumtanguliza Mungu

Limesimuliwa na Pierre Worou

“Bonjour!” Nimekuwa nikiwasalimu watu hivyo kwa Kifaransa tangu nilipozaliwa. Lakini mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 1975, nilikamatwa kwa kufanya hivyo. Acha nikueleze ni nini kilichoongoza kwenye tukio hilo na nini kimetukia tangu hapo.

NILIZALIWA Januari 1, 1944 (1/1/1944), katika eneo la mjini la Malété, huko Savé, katikati mwa Benin. * Wazazi wangu walinipa jina la Kiyoruba, Abiola. Nilipokuwa kijana, nilibadili jina hilo na nikaanza kuitwa Pierre, jina nililofikiri kuwa la kisasa na maarufu zaidi.

Watu wa eneo letu waliwapa vijana wote majina ya utani. Waliniita Pasta kwa sababu nilipozaliwa nilifanana na kasisi wa eneo letu. Hata hivyo, nilipenda sana kucheza mpira kuliko kuhudhuria madarasa ya katekisimu.

Mnamo 1959, nilihamia Sakété, mji ulio kusini mwa nchi, ili niendelee na masomo. Niliishi na binamu yangu Simon aliyekuwa mwalimu na ambaye alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wawili wa Yehova. Mwanzoni sikupendezwa kuketi na kusikiliza mazungumzo yao. Baadaye nilimwuliza binamu yangu mwingine, Michel, ikiwa angejiunga nami katika funzo hilo. Alikubali, na hiyo ndiyo iliyokuwa mara yangu ya kwanza kusikia jina la Mungu, Yehova.

Jumapili moja, mimi, Simon, na Michel tuliamua hatutaenda kanisani bali tutahudhuria mkutano wa Mashahidi. Tulivunjika moyo sana kuona kulikuwa na watu watano tu, yaani, wale Mashahidi wawili na sisi watatu. Hata hivyo, tulitambua kwamba tulichokuwa tukisikia ndio ukweli wa Biblia na tukaendelea kujifunza. Michel ndiye aliyekuwa wa kwanza kuonyesha wakfu wake kwa Mungu kwa kubatizwa. Leo yeye ni painia, kama Mashahidi wa Yehova wanavyowaita watumishi wa wakati wote.

Simon alihamia maeneo ya kaskazini kwenye jiji la Kokoro, nami niliambatana naye. Kulikuwa na kusanyiko la Mashahidi huko Ouansougon. Simon alienda kwa teksi, nami nikaendesha baiskeli yangu kilomita 220 hadi huko. Mimi na yeye tulibatizwa huko Septemba 15, 1961 (15/9/1961).

Magumu ya Utumishi wa Wakati Wote

Nilijiruzuku kwa kuchora na kuuza picha na vilevile kwa kulima shamba lililozaa vizuri. Mwangalizi anayesafiri, Philippe Zannou, alipotembelea kutaniko letu, aliniuliza ikiwa nimewahi kufikiri kuhusu kufanya utumishi wa wakati wote nikiwa painia. Baada ya kuzungumzia jambo hilo pamoja, mimi na rafiki yangu Emmanuel Fatunbi tuliamua tungeanza kazi hiyo mnamo Februari (Mwezi wa 2) 1966. Baada ya muda, nilianza kutumika nikiwa mwangalizi anayesafiri, nikitembelea makutaniko yaliyozungumza lugha ya Fon, Gun, Yoruba, na Kifaransa.

Mwishowe nilikutana na dada Mkristo aliyeitwa Julienne mwenye tabia zenye kupendeza ambaye alipendezwa na maisha rahisi, kama mimi. Tulioana Agosti 12, 1971 (12/8/1971), naye akajiunga nami katika kazi ya kutembelea makutaniko. Mwana wetu Bola alizaliwa Agosti 18, 1972. Tulipokuwa tukitembelea makutaniko, niliendesha baiskeli huku Julienne akiketi nyuma yangu akiwa amembeba Bola mgongoni. Kwa kawaida, Shahidi wa kutaniko tulilokuwa tukitembelea angebeba mizigo yetu kwenye baiskeli yake. Tuliyatembelea makutaniko kwa njia hiyo kwa miaka minne.

Siku moja Julienne alikuwa mgonjwa na usiku wote alikuwa na maumivu mengi. Asubuhi iliyofuata nilienda barabarani kutafuta msaada. Kwa ghafula, teksi ikatokea, na hilo halikuwa jambo la kawaida katika eneo hilo. Jambo la kushangaza hata zaidi, haikuwa na abiria! Nilimweleza dereva hali yangu na kumwuliza ikiwa angetupeleka Porto Novo, kwenye mji mkuu, uliokuwa umbali wa kilomita 25 hivi. Alikubali. Tulipowasili huko, alitabasamu na kusema: “Usilipe chochote. Hiyo ni zawadi yangu.”

Ilimbidi Julienne alale katika nyumba ya Shahidi mmoja kwa majuma mawili. Kwa fadhili, daktari alikuja kumwona kila siku. Pia alikuja na dawa zilizohitajika. Alipomchunguza Julienne mara ya mwisho, nilimwuliza kwa wasiwasi anipe gharama ya huduma zake. Nilishangaa alipojibu, “Sitakulipisha chochote.”

Mabadiliko Makubwa

Mnamo 1975, Dahomey ilianza kufuata mfumo wa kiserikali wa Maksi. Jina la nchi hiyo lilibadilishwa na kuwa Jamhuri ya Watu wa Benin. Maisha ya kila siku pia yalibadilika. Salamu mpya ilianzishwa: “Pour la révolution?” (Uko tayari kwa ajili ya mapinduzi?) Watu walipaswa kujibu: “Prêt!” (Niko tayari!) Dhamiri zetu zilizozoezwa na Biblia hazikuturuhusu kurudia maneno hayo ya kisiasa. Hilo lilitokeza uhasama mwingi.

Jumapili (Siku ya Yenga) moja karibu na mwisho wa mwaka wa 1975, nilikuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba karibu na St. Michel, nilipokamatwa. Kama nilivyoeleza awali, mwanamume mmoja alikuwa amenisalimu “Pour la révolution?” nami nikamjibu “Bonjour!” Nilipelekwa kwenye kituo cha polisi na nikachapwa. Lakini baadaye siku hiyo Mashahidi watatu wa eneo hilo walifanya mipango ili niachiliwe.

Nilikuwa Shahidi wa kwanza wa Yehova kukamatwa. Punde si punde, Mashahidi wengine wengi nchini kote walikamatwa pia. Serikali ilitwaa Majumba ya Ufalme na wamishonari wakafukuzwa nchini. Hata ofisi ya tawi ilifungwa na Mashahidi wengi wakakimbilia Togo upande wa magharibi au Nigeria upande wa mashariki.

Familia Yetu Yaongezeka Huko Nigeria

Mwana wetu wa pili, Kola, alizaliwa Aprili 25, 1976 (25/4/1976). Siku mbili baadaye, sheria ya serikali Na. 111 ilipiga marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova. Tulielekea Nigeria, ambako tulienda kwenye Jumba la Ufalme lililojaa wakimbizi. Siku iliyofuata mipango ilifanywa na tukagawiwa makutaniko jirani. Muda mfupi baada ya kikundi kimoja cha wakimbizi kuondoka kwenye jumba hilo, kikundi kingine kiliwasili. Malori yalitumiwa kuwasafirisha watu waliowasili kwenye makutaniko ya maeneo mengine.

Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Nigeria iliniomba niwatembelee Mashahidi wote kutoka Benin. Kisha niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi anayesafiri wa kikundi cha makutaniko ya Kiyoruba huko Nigeria, na baadaye nikayatembelea yale ya lugha ya Gun. Tulisafiri kwa pikipiki. Bola aliketi mbele yangu naye Kola alikuwa kati yangu na Julienne.

Mnamo 1979 tuligundua kwamba mke wangu angemzaa Jemima, kwa hiyo ikawa lazima kwetu kuacha kazi ya kuyazungukia makutaniko. Dada mdogo wa Julienne ambaye tulimwita Pépé, alikuja kutoka Benin ili aishi nasi. Familia yetu iliendelea kukua. Tulizaa wana wawili: Caleb, aliyezaliwa mnamo 1983 na Silas, aliyezaliwa mnamo 1987. Kwa hiyo, tukawa watu wanane katika familia yetu. Mimi na Julienne tulitaka kuwa wazazi wazuri, lakini pia tulitaka kubaki katika utumishi wa wakati wote ikiwa ingewezekana. Tungefanya hivyo jinsi gani? Tulikodi shamba na kupanda mihogo, mahindi, na viazi. Kisha tukajenga nyumba ndogo katika kijiji cha Ilogbo-Eremi.

Baada ya watoto kwenda shuleni, mimi na Julienne tulihubiri asubuhi. Sikuzote tulirudi nyumbani kula pamoja kama familia. Kisha, baada ya kupumzika, tulifanya kazi shambani. Pia Julienne na Pépé waliuza mazao sokoni. Sisi sote tulifanya kazi kwa bidii. Tunafurahi kwamba hatukuwa wagonjwa mara nyingi katika miaka hiyo.

Baraka Bila Elimu ya Juu

Hatukuwatia moyo watoto wetu wafuatie elimu ya juu. Tulijua kwamba kutanguliza masilahi ya Ufalme, kukuza sifa za Kikristo, na kufanya kazi kwa bidii, ndiyo mambo yanayoleta mafanikio maishani. Tulijaribu kukazia mambo hayo katika mioyo ya watoto wetu. Nilijifunza pamoja nao, na ilikuwa shangwe iliyoje kuwaona wakimpenda Yehova, wakijiweka wakfu ili wamtumikie, na kubatizwa ili kuonyesha wakfu wao!

Pépé alikuwa na umri mkubwa kuliko watoto wetu naye ndiye aliyekuwa wa kwanza kuondoka nyumbani. Mwanzoni, alipokuja kuishi nasi, nilimfundisha kusoma. Ingawa hakuwa na elimu nyingi, alijifunza Biblia kwa bidii na kuzingatia mambo mengine ya kiroho. Baada ya kutumika akiwa painia kwa muda fulani, aliolewa na Monday Akinra, mwangalizi anayesafiri, na akajiunga naye katika kazi hiyo. Sasa wana mwana, anayeitwa Timothy. Pépé na Monday wanaendelea katika utumishi wa wakati wote, na Monday anatumiwa sana katika makusanyiko.

Bola alienda kufunzwa upishi katika kampuni moja kubwa. Muda mfupi baadaye msimamizi mmoja alitambua mazoea yake mazuri ya kazi, kutegemeka kwake, na sifa nyingine nzuri za Kikristo. Baada ya muda, alipandishwa cheo katika kampuni hiyo. Zaidi ya hilo, yeye ni mume mzuri kwa mke wake mrembo, Jane, na baba mzuri kwa watoto wake watatu, na pia yeye ni mzee anayechukua madaraka yake kwa uzito katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova huko Lagos, Nigeria.

Kola alifunzwa kuwa mshonaji na pia akawa painia. Kwa kuwa alijifunza Kiingereza alipokuwa Nigeria, mnamo 1995 alialikwa atumike katika Idara ya Tafsiri kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Benin. Ametumika huko kwa miaka 13 iliyopita.

Utumishi Wetu Nchini Benin

Tulisisimka kusikia kwamba sheria ya serikali nchini Benin ya Januari 23, 1990, ilitangaza kwamba sheria iliyokuwa imetolewa mapema ya kupiga kazi yetu marufuku ilikuwa imefutwa. Wakimbizi wengi walirudi. Pia, wamishonari wapya waliwasili nchini Benin, na ofisi ya tawi ikafunguliwa tena. Mnamo 1994, familia yetu ilirudi Benin, lakini Pépé, Bola, na familia zao walibaki Nigeria.

Nilifaulu kupata kazi ya muda. Kutokana na pesa tulizopata kwa kukodisha nyumba yetu huko Nigeria na msaada wenye ukarimu wa Bola, tulifaulu kujenga nyumba ambamo sisi watano tuliishi karibu na ofisi ya tawi. Jemima alitumika akiwa painia kwa zaidi ya miaka sita, akijiruzuku kwa kufanya kazi ya kushona nguo. Kisha akaolewa na Kokou Ahoumenou, na sasa wanafanya kazi katika ofisi ya tawi iliyo karibu. Hivi karibuni Caleb na Silas watamaliza shule. Kwa msaada wa Mungu na ushirikiano wa familia yetu, mimi na Julienne tumebaki katika utumishi wa wakati wote, sasa kwa zaidi ya miaka 40.

Mungu amebariki sana kazi ya kuhubiri nchini Benin. Nilipobatizwa mwaka wa 1961, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 871 waliokuwa wakihubiri ujumbe wa Ufalme nchini humu. Mwaka niliokamatwa, idadi hiyo ilikuwa imeongezeka na kufikia 2,381. Kufikia wakati tuliporudi Benin mwaka wa 1994, idadi ilikuwa imepanda kufikia 3,858, licha ya marufuku ya miaka 14. Leo idadi hiyo ni zaidi ya maradufu, yaani, zaidi ya 9,000, na watu 35,752 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu mnamo 2008.

Nyakati nyingine mimi huenda mahali nilipokamatwa miaka 30 iliyopita na kutafakari yaliyotendeka. Mimi ninamshukuru Mungu hasa kwa kuibariki familia yangu. Hatujakosa chochote. Na bado mimi huwasalimu watu “Bonjour!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Wakati huo Benin iliitwa Dahomey na ilikuwa sehemu ya Afrika Magharibi ya Ufaransa.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Alitabasamu na kusema: “Usilipe chochote. Hiyo ni zawadi yangu”

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Hatukuwatia moyo watoto wetu wafuatie elimu ya juu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nilipokuwa mwangalizi anayesafiri, 1970

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tukiwa na wana wetu wawili, Bola na Kola, 1976

[Picha katika ukurasa wa 15]

Leo, nikiwa nimezungukwa na familia yangu—mke wangu, watoto watano, wajukuu watatu, na pia familia ya Pépé