Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watoto Waliofadhaika

Watoto Waliofadhaika

Watoto Waliofadhaika

▪ Pablo, mvulana mwenye umri wa miaka minane alijibu hivi mwalimu wake alipomwuliza ni kwa nini hakuwa amemaliza kazi ya shule: “Sikukuwa na wakati wa kutosha. Nimechoka.” Kama mvulana huyo kutoka Hispania aliyekuwa na macho mekundu kwa sababu ya usingizi, watoto wengi huwa na siku ndefu yenye kuchosha ambayo huenda ikahusisha saa 12 au zaidi za masomo na kazi ya shule. Kwa nini watoto wanapewa kazi nyingi sana ya shule?

Wazazi fulani hukubali watoto wao washiriki katika utendaji wa baada ya shule ili wawe na kitu cha kufanya kabla wazazi kurudi nyumbani. Wengine huwapangia watoto wao ratiba yenye utendaji mwingi ili wafanikiwe shuleni na kupata kazi nzuri. Ili kutimiza hilo, wazazi wengi huko Korea Kusini huwapeleka vijana wao kwenye “shule za kujifunza kwa makini,” ambapo wanakuwa na utendaji mwingi wenye kuchosha, nyakati nyingine kila siku ya juma kuanzia saa moja na nusu asubuhi hadi saa sita usiku au usiku zaidi. “Watafanya juu chini ili watoto wao wajiunge na vyuo vikuu bora kabisa,” inasema ripoti ya gazeti la New York Times.

Gazeti la Kihispania Mujer hoy linalochapishwa kila juma linasema hivi: “Wazazi wanaowashinikiza watoto wao wafanikiwe shuleni wanataka wawe na maisha mazuri, hata hivyo wanawataka wapate maksi za juu zaidi.” Ili watimize matarajio ya wazazi wao, huenda watoto wakajiwekea viwango vya juu sana, na hilo linaweza kuwafadhaisha sana. “Kulingana na uchunguzi wetu, watoto wamelemewa sana,” anasema Antonio Cano, msimamizi wa Shirika la Kihispania la Kuchunguza Mahangaiko na Mfadhaiko. Mtaalamu mwingine anasema kwamba asilimia 40 ya watoto walio chini ya umri wa miaka 15 huko Hispania wana mfadhaiko sana. Mfadhaiko huo unaweza kuwaathiri sana watoto na hata kufanya wajiue. Kwa mfano, huko Korea Kusini, “kujiua ndicho kisababishi cha pili cha vifo miongoni mwa vijana walio na umri wa kati ya miaka 10 na 19 baada ya aksidenti za barabarani,” linasema gazeti la The New York Times.

Bila shaka, vijana wanapaswa kusoma kwa bidii shuleni, na wazazi wanapaswa kuwasaidia kadiri wanavyoweza, kwa sababu hawatapata nafasi hiyo tena. Hata hivyo, “watoto si watu wazima. Hawawezi kukabiliana na siku ndefu yenye kuchosha,” anasema mwalimu anayeitwa Irene Arrimadas. Wazazi wenye upendo wanaoelewa hilo huhakikisha kwamba watoto wao wanapata wakati wa kutosha wa kupumzika na utendaji unaojenga wa familia. Akionyesha umuhimu wa kuwa na usawaziko, Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 4:6. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa maelezo zaidi kuhusu jinsi watoto wengi wanavyoshinikizwa, ona mfululizo wa makala “Kufadhaishwa Shuleni na Kwingine,” katika gazeti Amkeni! la Aprili 2009.