Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhakikisha Usalama Wako Unapoendesha Gari

Kuhakikisha Usalama Wako Unapoendesha Gari

Kuhakikisha Usalama Wako Unapoendesha Gari

INGAWA leo mamilioni ya watu wanaona kuendesha gari kuwa jambo la lazima, nyakati nyingine kufanya hivyo hutokeza madhara. Imekadiriwa kwamba kila mwaka, zaidi ya watu 1,200,000 hupoteza maisha yao katika aksidenti za barabarani ulimwenguni pote! Kwa hiyo, lingekuwa jambo muhimu kujifunza kuendesha gari kwa njia salama. Acheni tuchunguze hatua fulani tunazoweza kuchukua.

Jichunguze

Ripoti katika jarida Australian Journal of Social Issues ilisema kwamba mojawapo ya hatua muhimu zaidi ambayo dereva anaweza kuchukua ili kupunguza vifo vinavyosababishwa na aksidenti za barabarani ni kuhakikisha kwamba yuko katika hali inayofaa kuendesha gari. Hivyo, kabla ya kuanza safari, dereva anapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, niko katika hali inayofaa kuendesha gari?’ Uchovu unaweza kupunguza uwezo wa kufikiri na kufanya mambo. Ofisi ya Usafiri wa Barabarani ya Filipino inaorodhesha hasira, wasiwasi, na msisimko kuwa hisia zinazoathiri jinsi unavyoendesha gari na kumfanya mtu afanye maamuzi yasiyofaa na hata atende kwa jeuri barabarani.

Hali ya kimwili ya mtu pia inapaswa kufikiriwa, kwa sababu magonjwa fulani au majeraha yanaweza kumzuia mtu kuendesha gari kwa njia salama. Dereva ambaye anaheshimu uhai wa wengine hataendesha gari ikiwa ameathiriwa na kileo. Dawa fulani za kitiba na za kulevya zinaweza kuathiri utendaji wa dereva. Katika hali fulani lingekuwa jambo la busara kuvunja safari au kumwambia mtu mwingine aendeshe.

Chunguza Ustadi Wako

Hasa katika nchi zinazositawi, kadiri idadi ya magari inavyozidi kuongezeka ndivyo idadi ya madereva wapya na wasio na uzoefu inavyoongezeka. Hivyo, ni vizuri kufikiria mambo mawili ambayo dereva yeyote anaweza kufanya ili kuepuka aksidenti.

Kaa chonjo! Uwe macho, angalia ikiwa kuna vitu vyovyote hatari barabarani na pia nyuma yako, na ufikirie maamuzi ambayo madereva wengine wanaweza kufanya—kutia ndani maamuzi mabaya. Kwa kuwa magari mengi hugongana kwa sababu ya gari moja kufuata lingine kwa ukaribu, dereva mwenye hekima atahakikisha kuna umbali wa kutosha kati yake na magari mengine.

Tambua sehemu zisizoonekana vizuri na vikengeusha-fikira. Geuka uone ni nini kinachotendeka, usitegemee tu vioo vya gari. Epuka kukengeushwa unapoendesha gari. Usifanye mambo mengine unapoendesha gari—kuongea kwa simu au kutumia vifaa vingine kunakengeusha.

Ikiwa unaendesha pikipiki: Kichapo kimoja kinasema kwamba waendeshaji wa pikipiki wanakabili hatari mara 37 ya kufa katika misiba ya barabarani kuliko watu walio ndani ya magari. Unaweza kujilinda jinsi gani? Hatua zilizotajwa pia zinaweza kutumiwa na waendeshaji wa pikipiki. Isitoshe, Shirika la Usalama wa Pikipiki nchini Marekani linasema: “Hakikisha unaweza kuonekana.” Washa taa za pikipiki. Usiendeshe pikipiki mahali ambapo madereva wengine hawawezi kukuona. “Valia mavazi ya kukukinga.” Valia kofia ngumu na mavazi mazito yenye rangi nyangavu. “Kaa chonjo sana.” Wazia kwamba wengine hawakuoni, na hivyo endesha kwa uangalifu.

Chunguza Gari Lako

Dereva lazima azingatie usalama na gari lake linapaswa kuwa katika hali nzuri. Breki na sehemu nyingine zote za gari zinapaswa kuwa katika hali nzuri. Hakikisha kwamba tairi hazijakwisha ili kuzuia gari lisiteleze. Kiasi cha kutosha cha upepo katika tairi kitakuwezesha kudhibiti gari vizuri na kufunga breki. Magari mengi leo yana mikanda ya usalama. Mikanda hiyo haitakulinda ikiwa hutaifunga.

Endesha gari lako kulingana na hali. Barabara zenye unyevunyevu hasa zile zilizo na barafu au theluji, zinaathiri muda utakaochukua kusimamisha gari na uwezo wako wa kudhibiti usukani. Unapoendesha gari usiku, taa za mbele zinapaswa kuwa katika hali nzuri na upunguze mwendo. Kwa kuwa uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu, ingefaa tufanye chochote tunachoweza ili kulinda uhai wetu, kutia ndani kujifunza kuendesha gari kwa njia salama.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]

KUENDESHA GARI BILA KUTUMIA MAFUTA MENGI

Endesha gari kwa utaratibu: Kuendesha gari kwa kasi na kufunga breki mara kwa mara kunatumia mafuta mengi.

Zima injini ikiwa gari limesimama: Injini za magari mengi ya kisasa hazihitaji kupashwa joto kabla ya kuendeshwa. Ikiwa gari litasimama kwa zaidi ya nusu dakika, zima injini.

Dumisha kiasi kinachofaa cha upepo: Tairi zilizo na upepo wa kutosha husonga kwa urahisi zaidi, hivyo gari halitumii mafuta mengi sana.

Usiendeshe gari kwa kasi: Kuendesha gari kwa kasi sana ni hatari na kunatumia mafuta mengi.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 11]

▪ Uwe macho

▪ Funga mkanda wa usalama

▪ Usifanye mambo mengine unapoendesha gari

▪ Epuka kukengeushwa

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 12]

▪ Tambua sehemu zisizoonekana vizuri

▪ Breki ziwe katika hali nzuri

▪ Kiasi cha kutosha cha upepo katika tairi

▪ Tairi ambazo hazijaisha

▪ Dumisha umbali wa kutosha kati yako na magari mengine

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 13]

▪ “Valia mavazi ya kukukinga”

▪ “Hakikisha unaweza kuonekana”

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 13]

▪ Chunguza taa za mbele