Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kubadili Dini Yako?

Je, Ni Vibaya Kubadili Dini Yako?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Vibaya Kubadili Dini Yako?

Avtar alipoanza kujifunza Biblia, familia yao ya Wakalasinga ilikasirika. “Katika nchi yetu,” anasema, “ukibadili dini yako jamii inakutenga. Hata majina yetu yana maana ya kidini. Kubadili dini yako kunaonwa kuwa kukataa utambulisho wako na kukosea familia yako heshima.”

MWISHOWE Avtar alikuwa Shahidi wa Yehova. Je, alifanya vibaya kubadili dini yake? Huenda ukawa na maoni kama ya familia yake. Huenda ukahisi kwamba dini ni sehemu muhimu ya historia na utamaduni wa familia na haipaswi kubadilishwa.

Ni muhimu kuheshimu familia yako. Biblia inasema: “Msikilize baba yako aliyekuzaa.” (Methali 23:22) Lakini ni muhimu zaidi kutafuta kujua ukweli kumhusu Muumba wetu na makusudi yake. (Isaya 55:6) Je, mtu anaweza kupata ukweli huo? Ikiwa ndivyo, ukweli huo ni muhimu kadiri gani kwako?

Kutafuta Dini ya Kweli

Dini za ulimwengu zinafundisha mafundisho yanayotofautiana. Bila shaka, mafundisho hayo yote hayawezi kuwa ya kweli. Kwa sababu hiyo, lazima kuwe na watu wengi ambao, kama Biblia inavyosema, “wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Hata hivyo, kama vile mtume Paulo alivyosema kwenye 1 Timotheo 2:4, mapenzi ya Mungu ni kwamba ‘watu wa namna zote wapate ujuzi sahihi wa kweli.’ Ujuzi sahihi unaweza kupatikana jinsi gani?

Fikiria sababu za kuichunguza Biblia. Paulo, mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na roho ya Mungu aliandika hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha.” (2 Timotheo 3:16) Unapotafuta kweli, chunguza uthibitisho wa kwamba yale ambayo Biblia inasema ni kweli. Chunguza hekima yake isiyo na kifani, usahihi wake wa kihistoria, na unabii wake uliotimizwa.

Badala ya kufundisha kwamba dini zote zinaelekeza watu kwa Mungu, Biblia inawaambia wasomaji wake wasiamini kila kitu wanachosikia lakini “[wajaribu] maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) Kwa mfano, fundisho lolote ambalo kwa kweli linatokana na Mungu lazima lipatane na utu wake kutia ndani sifa yake kuu, upendo.—1 Yohana 4:8.

Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu anataka ‘kwa kweli tumpate.’ (Matendo 17:26, 27) Kwa kuwa Muumba wetu anataka tutafute kweli, haingekuwa kosa kutenda kulingana na uthibitisho tunaopata, hata kama itamaanisha kubadili dini yetu. Lakini tutatatuaje matatizo ambayo huenda yakasababishwa na kubadili dini?

Ushikamanifu kwa Familia na kwa Mungu

Watu wanapobadili dini yao, huenda wakaamua kwamba hawatashiriki tena sikukuu au sherehe fulani za kidini. Inaeleweka kwamba jambo hili linaweza kusababisha mgogoro katika familia. Yesu alikubaliana na jambo hilo. Aliwaambia hivi wafuasi wake: “Nilikuja kuleta mgawanyiko, mtu kumpinga baba yake, binti kumpinga mama yake, mke aliye mchanga kumpinga mama-mkwe wake.” (Mathayo 10:35) Je, Yesu alimaanisha kwamba mafundisho ya Biblia yalikusudiwa kusababisha ugomvi? Hapana. Aliona mapema jambo linaloweza kutokea watu wa familia wanapompinga yule anayechukua msimamo thabiti ulio tofauti na wao kuhusu dini.

Je, hali ya kutoelewana katika familia inapaswa kuepukwa kabisa? Biblia inafundisha kwamba watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao na wake wanapaswa kujitiisha kwa waume zao. (Waefeso 5:22; 6:1) Hata hivyo, Biblia inawaagiza wale wanaompenda Mungu ‘wamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Matendo 5:29) Hivyo, nyakati nyingine, kwa sababu ya ushikamanifu wako kwa Mungu unaweza kufanya maamuzi yasiyopendwa na wengine katika familia.

Ingawa Biblia inatofautisha waziwazi mafundisho ya kweli na yasiyo ya kweli, Mungu anampa kila mtu uhuru wa kuchagua jinsi atakavyotenda. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Mtu yeyote hapaswi kulazimishwa kuabudu kwa njia asiyoikubali au kufanywa achague kati ya dini yake na familia yake. Je, kujifunza Biblia kunavunja familia? Hapana. Kinyume na hilo, Biblia inamtia moyo mume na mke walio na dini tofauti waendelee kukaa pamoja kama familia.—1 Wakorintho 7:12, 13.

Kushinda Woga

Huenda ukaogopa maoni ya watu wa jamii ukianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Mariamma anasema hivi: “Familia yangu ilikuwa na wasiwasi kwamba sitapata mume mzuri ambaye atanitunza. Hivyo walinipinga nilipoanza kujifunza Biblia.” Mariamma alimtegemea Yehova Mungu na akaendelea kujifunza. (Zaburi 37:3, 4) Unaweza kufanya vivyo hivyo. Badala ya kuogopa matokeo, fikiria faida. Ujumbe wa Biblia unabadili maisha na kuboresha tabia za watu. Watu hujifunza kuonyesha upendo usio wa kichoyo kwa familia zao. Mtu anaweza kushinda mazoea mabaya kama vile kutukana watu, kuwatendea jeuri, na kutumia vibaya vileo na dawa za kulevya. (2 Wakorintho 7:1) Biblia inachochea tabia nzuri kama ushikamanifu, unyoofu, na bidii. (Methali 31:10-31; Waefeso 4:24, 28) Ukijifunza Biblia utaona faida za kufuata mafundisho yake maishani mwako.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini uchunguze mafundisho ya dini yako?—Methali 23:23; 1 Timotheo 2:3, 4.

▪ Unaweza kutambua mafundisho ya kweli jinsi gani?—2 Timotheo 3:16; 1 Yohana 4:1.

▪ Je, upinzani kutoka kwa watu wa familia ukuzuie kujifunza Biblia?—Matendo 5:29.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Ujumbe wa Biblia unabadili maisha na kuboresha tabia za watu

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mariamma na mume wake