Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwaminifu kwa Mungu kwa Zaidi ya Miaka 70

Mwaminifu kwa Mungu kwa Zaidi ya Miaka 70

Mwaminifu kwa Mungu kwa Zaidi ya Miaka 70

Limesimuliwa na Josephine Elias

“Usiwe na wasiwasi,” mume wangu akaninong’onezea kutoka katika chumba cha gerezani. “Iwe wataniua au wataniachilia huru nitabaki nikiwa mwaminifu kwa Yehova.” Mimi pia nilikuwa nimeazimia kuendelea kuwa mwaminifu. Ninahisi hivyo hadi leo.

NILIZALIWA mnamo 1916 huko Sukabumi, jiji dogo katika nyanda za juu za Java Magharibi, Indonesia. Wazazi wangu walikuwa Wachina matajiri walioishi katika nyumba kubwa yenye watumishi. Nilikuwa na ndugu watano, watatu wakubwa kuliko mimi na wawili wadogo. Mimi ndiye niliyekuwa msichana pekee na hivyo nilipenda michezo ya wavulana. Nilipanda juu ya paa za nyumba na kufurahia michezo. Hata hivyo, jambo fulani lilinihangaisha sana.

Wazo la kuteketezwa katika moto wa mateso liliniogopesha sana. Walimu wangu waliniambia kwamba wasichana watundu walitupwa motoni. Na kwa sababu nilikuwa mtundu, nilihisi ningetupwa huko. Baadaye, nilipokuwa katika shule ya sekondari huko Jakarta (ambayo wakati huo iliitwa Batavia), nikawa mgonjwa. Daktari alifikiri kwamba ningekufa, kwa hiyo, mama mwenye nyumba alijaribu kunifariji kwa kuniambia karibuni nitaenda mbinguni. Hata hivyo, nilihofia kwamba nitaenda motoni.

Mama yangu, Kang Nio, na kaka yangu Dodo walikuja upesi Jakarta kunichukua. Tukiwa njiani kuelekea nyumbani, Dodo aliniuliza, “Ulijua kwamba Biblia haifundishi juu ya moto wa mateso?”

“Ulijuaje jambo hilo?” nikamwuliza. Mama alisoma maandiko katika Biblia kuonyesha kwamba wafu hawajui jambo lolote na kwamba wanangojea kufufuliwa. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 5:28, 29) “Tulifundishwa mambo haya na Mashahidi wa Yehova,” wakaniambia. Walinipa kijitabu kidogo chenye kichwa Where Are the Dead? ambacho nilianza kusoma moja kwa moja. * Kabla ya kufika nyumbani, nilisema, “Hii ndiyo kweli!”

Nawahubiria Wengine

Kufikia wakati huo familia yetu ilikuwa imehamia Bandung, jiji kubwa huko Java Magharibi. Nikiwa huko nilipona polepole. Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 1937, tulitembelewa na Clem Deschamp, Shahidi Mwaustralia aliyekuwa akitumikia huko Jakarta. Alipotutembelea, mimi, mama yangu, na kaka zangu—Felix, Dodo, na Peng—tulibatizwa ili kuonyesha wakfu wetu kwa Mungu. Baadaye, ndugu zangu wadogo Hartanto na Jusak na baba yangu, Tan Gim Hok, pia wakawa Mashahidi. *

Tulipobatizwa, tuliungana na Clem katika kampeni ya pekee ya kuhubiri ya siku tisa. Alitufundisha jinsi ya kuhubiri kwa kutumia kadi ya ushuhuda iliyokuwa na ujumbe rahisi wa Biblia katika lugha tatu. Pia tuliwahubiria watu wa ukoo na marafiki kwa njia isiyo rasmi. Punde si punde, kikundi chetu kidogo huko Bandung kikawa kutaniko, kutaniko la pili nchini Indonesia.

Baadaye katika mwaka huo, familia yetu ilihamia Jakarta ili kuwahubiria Wachina 80,000 walioishi huko. Mimi, Mama, na Felix, tukawa mapainia, ambao ni watumishi Wakristo wa wakati wote. Pia tulihubiri huko Bandung, Surabaya, na sehemu nyingine. Muda mwingi nilihubiri peke yangu. Nilikuwa kijana, mwenye nguvu, na nilifurahia kumtumikia Mungu. Hata hivyo, kulikuwa dalili za vita na baada ya muda mfupi imani yangu ingejaribiwa.

Vita Vyaleta Majaribu

Mnamo Desemba (Mwezi wa 12) 1941, Asia ilihusishwa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu. Jeshi la Japani lilidhibiti Indonesia kabisa. Vichapo vya Biblia vilipigwa marufuku, nasi hatungeweza kuhubiri hadharani. Nilibeba mchezo wa chesi nilipowatembelea watu wenye kupendezwa ili watu wafikirie kwamba nilikuwa nikicheza chesi.

Mnamo 1943, niliolewa na André, painia mwenye ujasiri na sauti nzito yenye kuamrisha. Tulipeleka vichapo vya Biblia kwa siri katika sehemu zote za Java. Ikiwa tungekamatwa tungeteswa na kuuawa. Tuliponea chupuchupu mara nyingi sana.

Wakati mmoja tulipokuwa tukipanda gari la moshi huko Sukabumi, mimi na André tulisimamishwa na polisi wa jeshi la Japani wenye kuogopesha wanaoitwa Kempeitai. Nilikuwa na vichapo vilivyopigwa marufuku ndani ya mfuko wangu. “Umebeba nini ndani ya mfuko wako?” akauliza polisi mmoja.

“Nguo,” akasema André.

“Na chini ya nguo hizo kuna nini?” polisi huyo akauliza.

“Nguo nyingine,” akasema André.

“Lakini, kuna nini chini kabisa ya mfuko huo?” akauliza polisi huyo. Nilisimama kwa hofu na kusali kimya kwa Yehova. “Afadhali wewe mwenye uangalie,” akajibu André.

Msaidizi wa polisi huyo akaingiza mkono wake katika mfuko. Ghafula, alipiga mayowe kwa uchungu na kuutoa mkono wake haraka kutoka mfukoni. Alikuwa amechomwa na sindano. Ofisa huyo aliyekuwa ameaibika alituamuru upesi tufunge mfuko na kupanda gari la moshi.

Kwenye safari nyingine kwenda Sukabumi, polisi hao wa Kempeitai waligundua kwamba mimi ni Shahidi na wakaniagiza niende kwenye makao yao makuu. Nilienda pamoja na André na kaka yangu Felix. Tukiwa huko André alihojiwa kwanza. Alinyeshewa na maswali. “Mashahidi wa Yehova ni nani? Je, mnaipinga serikali ya Japani? Wewe ni mpelelezi?”

“Sisi ni watumishi wa Mungu Mweza-Yote na hatujafanya kosa lolote,” akajibu André. Ofisa mkuu akanyanyua upanga mrefu wa Kijapani kutoka ukutani.

“Vipi nikikuua sasa?” akafoka. André akaweka kichwa chake juu ya dawati na kusali kimyakimya. Baada ya muda mrefu, maofisa waliangua kicheko. “Wewe ni jasiri!” akasema ofisa. Kisha akamwambia André aondoke na akatuambia mimi na Felix tuingie. Maneno yetu na ya André yalipopatana, ofisa huyo alisema kwa sauti kubwa: “Ninyi si wapelelezi. Tokeni hapa!”

Sisi watatu tulienda nyumbani tukimsifu Yehova kwa furaha. Bado hatukujua kwamba tungekabili matatizo mengine.

Imani Yetu Yajaribiwa Zaidi

Miezi michache baadaye, André alisalitiwa na “ndugu wa uwongo” na akafungwa na Kempeitai. (2 Wakorintho 11:26) Nilimtembelea gerezani. Alikuwa amekonda na alikuwa dhaifu sana. Chakula alichookota kwenye bomba la kutolea maji kwenye seli yake ndicho kilichomsaidia aendelee kuishi. Walinzi wa gereza hawakuweza kuvunja utimilifu wake. Kama ilivyotajwa mwanzoni, alininong’onezea kutoka gerezani: “Usiwe na wasiwasi. Iwe wataniua au wataniachilia huru nitabaki nikiwa mwaminifu kwa Yehova. Wanaweza kunibeba kutoka hapa nikiwa maiti lakini hawatanibeba nikiwa msaliti.”

Baada ya kufungwa kwa miezi sita, André alifikishwa katika Mahakama Kuu ya Jakarta. Familia na marafiki walijaa ndani ya mahakama. Tulikuwa na wasiwasi mwingi.

“Kwa nini unakataa kujiunga na jeshi la Japani?” hakimu akauliza.

“Mimi ni askari wa Ufalme wa Mungu,” André akajibu, “na askari hawezi kutumikia majeshi mawili wakati uleule.”

“Je, unaweza kuwaambia wengine wasijiunge na jeshi?” akauliza hakimu.

“Hapana,” akajibu André, “uamuzi ni wao.”

André aliendelea kujitetea akinukuu Biblia mara nyingi. Hakimu huyo, aliyekuwa Mwislamu sugu, alivutiwa sana. “Huenda tukawa na imani tofauti, lakini siwezi kumlazimisha mtu apingane na dhamiri yake,” akasema hakimu huyo. “Uko huru.”

Familia na marafiki waliokuwa mahakamani walifarijika kama nini, na moyo wangu uliruka-ruka. André alinijia na kunishika mkono. Watu wa familia na marafiki walituzunguka, wakitupongeza kwa msisimuko.

Kuhubiri Kuhusu Uhuru wa Kweli

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kwisha, mapinduzi yalizuka dhidi ya utawala wa kikoloni wa Uholanzi nchini Indonesia. Maelfu ya watu walikufa, na wakazi wa vijiji vizima walitoroka nyumbani. Wazalendo walijaribu kutulazimisha tuseme “Merdeka” kwa sauti, neno linalomaanisha “Uhuru.” Lakini tuliwaambia katika mambo kama hayo ya kisiasa sisi hatuungi mkono upande wowote.

Licha ya jeuri, tulianza tena kuhubiri nyumba kwa nyumba. Tulitumia kadi zetu za ushuhuda za zamani na vichapo tulivyokuwa tumehifadhi wakati wa vita. Mnamo Mei (Mwezi wa 5) 1948, jeuri ilipopungua, mimi na André tulianza tena kufanya upainia, na hivyo tukawa mapainia pekee waliokuwepo Indonesia. Miaka mitatu baadaye tulifurahi sana kuwakaribisha Mashahidi 14 huko Jakarta, wote wakiwa wahitimu wa Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko New York, Marekani. Mazoezi waliyotupa yalitutayarisha kwa ajili ya madaraka mengine.

Juni (Mwezi wa 6) 1952, mimi na André tulipewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee huko Semarang, katikati mwa Java. Mwaka uliofuata sisi tulihudhuria darasa la 22 la Gileadi. Baada ya kuhitimu tulirudi Indonesia na tukatumwa Kupang, Timor. Baadaye tulipewa migawo huko Sulawesi Kusini na Sulawesi Kaskazini. Tukiwa huko tulikabili majaribu mengine ya imani.

Tunapigwa Tena Marufuku

Mnamo 1965 jaribio la mapinduzi lilisababisha vifo vya mamia ya maelfu ya watu. Makasisi fulani wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walijihusisha katika mapinduzi hayo na wakadai kwamba Mashahidi wa Yehova ni Wakomunisti. Kwa kupendeza, wenye mamlaka hawakudanganywa kwa urahisi. Hata hivyo, makasisi waliendelea kuwachongea Mashahidi. Mwishowe, Desemba 25, 1976, Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku.

Muda mfupi baada marufuku hiyo kutangazwa, mwendesha-mashtaka mkuu katika wilaya ya Manado alimwagiza André aende ofisini mwake. “Je, unajua kwamba Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku?” akauliza.

“Ndiyo,” akajibu André.

“Je, sasa uko tayari kubadili dini yako?” akasema mwendesha-mashtaka huyo.

André aliinama na kupigapiga kifua chake kwa mbwembwe. “Unaweza kung’oa moyo wangu kutoka kifuani mwangu, lakini huwezi kamwe kunifanya nibadili dini yangu,” akasema kwa sauti kubwa.

Akiwa ameshangaa, mwendesha-mashtaka akamwuliza, “Nitaandika nini katika ripoti yangu?”

“Andika kwamba bado mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na sijafanya kosa lolote,” akasema André.

“Itabidi nikunyang’anye vichapo vyako,” akasema mwendesha-mashtaka mkuu.

Usiku huo vijana Mashahidi waliondoa vichapo kutoka kwa nyumba yetu, na kuacha makatoni matupu. Tuliendelea kuhubiri tukitumia Biblia. Mwendesha-mashtaka hakutusumbua tena.

Nimekuwa na Maisha Mazuri!

Baadaye mimi na André tulifanya upainia huko Surabaya, kwenye kisiwa cha Java, na Bangka, kisiwa kilichoko kusini-mashariki mwa Sumatra. Hata hivyo, mnamo 1982, tulilazimika kurudi Jakarta kwa sababu ya afya mbaya. Tukiwa huko, André alikufa mwaka wa 2000, akiwa na umri wa miaka 85. Alikuwa painia mwenye bidii hadi kifo chake. Mwaka mmoja baada ya kifo chake, marufuku yaliondolewa.

Nimekuwa na maisha yenye kupendeza kama nini! Leo nina umri wa miaka 93, na nimekuwa painia kwa zaidi ya miaka 70. Mnamo 1937, nilipobatizwa, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 25 tu nchini Indonesia. Leo kuna Mashahidi karibu 22,000. Nafurahi sana kushiriki katika ukuzi huo! Lakini safari yangu imeanza tu. Ninataka kumtumikia Mungu kwa uaminifu milele.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 9 Wote katika familia waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova. Josephine na Jusak, ambao tu ndio wangali hai, bado wanamtumikia Yehova kwa bidii huko Jakarta.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Mimi ni askari wa Ufalme wa Mungu, na askari hawezi kutumikia majeshi mawili wakati uleule”

[Blabu katika ukurasa wa 14]

“Unaweza kung’oa moyo wangu kutoka kifuani mwangu, lakini huwezi kamwe kunifanya nibadili dini yangu”

[Ramani katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Maeneo tulimoishi na kuhubiri

INDONESIA

Sulawesi

Manando

Sumatra

Bangka

Java

JAKARTA

Sukabumi

Bandung

Semarang

Surabaya

Timor

Kupang

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mimi na André katika miaka ya 1970

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, kijitabu “Where Are the Dead?” kilinisadikisha kuhusu kweli za Biblia