Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inawezekana Kuwapenda Adui Zako?

Je, Inawezekana Kuwapenda Adui Zako?

Maoni ya Biblia

Je, Inawezekana Kuwapenda Adui Zako?

“Mimi ninawaambia ninyi,” akasema Yesu Kristo, “endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni, kwa kuwa yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:44, 45.

JE, UNAFIKIRI dini inawachochea watu wapendane na wawe na amani au inachochea chuki na jeuri? Leo, watu wengi huona kwamba dini inachochea chuki na jeuri hasa inapojihusisha na siasa, ukabila, au mambo ya kizalendo. Hata hivyo, kama maneno ya Yesu yanavyoonyesha, wale ambao ni ‘wana wa kweli wa Mungu’ wanawapenda watu wengine—hata adui zao—kama Mungu anavyofanya.

Mtumishi mwingine wa Mungu alisema: “Ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe . . . Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:20, 21) Lakini je, inawezekana kuwa na upendo kama huo katika ulimwengu huu uliogawanyika? Mashahidi wa Yehova wanajibu bila kusita, ndiyo! Fikiria mfano wa Yesu na wafuasi wake wa mapema.

Waliwapenda Adui Zao

Yesu alifundisha ukweli kumhusu Mungu, na watu wengi walimsikiliza kwa furaha. Hata hivyo, wengine walimpinga, wengi wao bila kujua. (Yohana 7:12, 13; Matendo 2:36-38; 3:15, 17) Lakini, Yesu aliendelea kuwahubiria watu wote ujumbe wenye kuokoa uhai, kutia ndani wapinzani wake. (Marko 12:13-34) Kwa nini? Alijua kwamba huenda wengine wakabadili njia zao, wamtambue kuwa Masihi, na wapatanishe maisha yao na kweli zinazopatikana katika Neno la Mungu.—Yohana 7:1, 37-46; 17:17.

Hata usiku ambao Yesu alikamatwa isivyo haki na wapinzani waliokuwa na silaha, alionyesha kwamba aliwapenda adui zake. Alimponya mmoja kati ya watu hao waliokuja kumkamata ambaye mtume Petro alikuwa amemkata kwa upanga. Pindi hiyo, Yesu alitoa kanuni muhimu ambayo inawaongoza wafuasi wake wa kweli hadi leo. Alisema hivi: “Wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:48-52; Yohana 18:10, 11) Miaka 30 hivi baadaye, Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. . . . Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa [Mungu].” (1 Petro 2:21, 23) Ni wazi Petro alikuwa amejifunza kwamba wafuasi wa kweli wa Kristo wanapaswa kuwapenda wengine, si kulipiza kisasi.—Mathayo 5:9.

Wote ambao ‘wanafuata hatua za Yesu kwa ukaribu’ wanaonyesha mtazamo wenye upendo na wenye fadhili kama wake. “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, . . . akiendelea kujizuia chini ya uovu,” inasema 2 Timotheo 2:24. Sifa hizo huonekana katika maisha ya Mkristo ambayo hujitahidi kufanya mapatano na kuishi kwa amani.

‘Mabalozi wa Kristo’ Wanaofanya Amani

Mtume Paulo aliwaandikia hivi waamini wenzake: “Kwa hiyo sisi ni mabalozi walio badala ya Kristo . . . Kama walio badala ya Kristo tunaomba: ‘Mpatanishwe pamoja na Mungu.’” (2 Wakorintho 5:20) Mabalozi hawaingilii mambo ya kisiasa na ya kijeshi ya nchi walikotumwa. Kazi yao ni kutetea serikali ya nchi ambayo wanawakilisha.

Ndivyo ilivyo na mabalozi na wajumbe wa kweli wa Kristo. Wanamwona Yesu kuwa Mfalme na wanatetea Ufalme wake wa kimbingu kwa kutangaza habari njema kwa amani. (Mathayo 24:14; Yohana 18:36) Kwa hiyo, Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa siku zake: “Hatupigi vita kulingana na tulivyo katika mwili. Kwa maana silaha za vita vyetu si za kimwili, bali ni zenye nguvu kwa Mungu kwa ajili ya kupindua . . . mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.”—2 Wakorintho 10:3-5; Waefeso 6:13-20.

Paulo alipoandika maneno hayo, Wakristo walikuwa wakiteswa katika nchi nyingi. Kwa kweli, wangeweza kulipiza kisasi. Lakini waliendelea kuwapenda adui zao na kuwaambia wote waliokuwa tayari kusikiliza ujumbe wa upatanisho. Kitabu Encyclopedia of Religion and War kinasema hivi: “Wafuasi wa mapema wa Yesu walikataa kupigana na kujiunga na utumishi wa kijeshi,” kwa kuwa walitambua kwamba mazoea hayo “hayakupatana na kanuni ya upendo ambayo Yesu alifundisha na agizo lake kwamba mtu anapaswa kuwapenda adui zake.” *

Kama tu Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wanamtambua Yesu kuwa Mfalme wao. Pia wanamtambua kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu—serikali ya kimbingu ambayo hivi karibuni italeta amani na usalama wa kudumu duniani. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Hivyo, kama tu mabalozi na wajumbe, wanatangaza sifa bora za Ufalme huo. Wakati huohuo, wao hujitahidi kuwa raia wazuri katika nchi wanamoishi, wakilipa kodi na kutii sheria ambazo hazipingani na sheria ya Mungu.—Matendo 5:29; Waroma 13:1, 7.

Hata hivyo, inasikitisha kwamba kama tu Wakristo wa mapema, nyakati nyingine Mashahidi hueleweka vibaya, huharibiwa sifa, na kuteswa. Lakini wao hawalipizi kisasi kamwe. Badala yake, wao hujaribu kuwa “wenye kufanya amani na watu wote,” wakitazamia kwamba huenda wapinzani fulani ‘watapatanishwa pamoja na Mungu’ na kuwa na taraja la kupata uzima wa milele. *Waroma 12:18; Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 “Waandishi wote Wakristo walioishi kabla ya Konstantino [maliki wa Roma wa 306-337 W.K.] walipinga mauaji yaliyotokea vitani,” kinasema kitabu Encyclopedia of Religion and War. Mtazamo huo ulibadilika uasi-imani uliotabiriwa katika Biblia ulipoanza kuenea.—Matendo 20:29, 30; 1 Timotheo 4:1.

^ fu. 15 Sawa tu na Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova hutetea kisheria uhuru wao wa kidini wanapohitaji kufanya hivyo.—Matendo 25:11; Wafilipi 1:7.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Wakristo wanapaswa kuwatendea adui zao jinsi gani?—Mathayo 5:43-45; Waroma 12:20, 21.

▪ Yesu alitendaje alipoteswa?—1 Petro 2:21, 23.

▪ Kwa nini Wakristo wa mapema walipinga vita?—2 Wakorintho 5:20; 10:3-5.