Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Kazi

Uwe na Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Kazi

Uwe na Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Kazi

KATIKA kipindi hiki chenye matatizo mengi ya kiuchumi, kila mtu anahangaikia kuwa na kazi inayotegemeka, yenye mapato ambayo yatatosheleza mahitaji ya familia yake. Si rahisi kufanya hivyo, hasa wakati maelfu ya watu wanaachishwa kazi. Ikiwa wewe ni mmoja wa wale ambao wameachishwa kazi ghafula, kibarua kigumu sasa ni kujitahidi kutafuta kazi nyingine.—Ona masanduku kwenye ukurasa wa 8 na 9.

Lakini, bado kuna mambo mengine muhimu maishani zaidi ya kufanya kazi kwa bidii. Glenn, mwanamume mwenye familia anayeishi Australia, anasema hivi: “Ukweli wa mambo ni kwamba hakuna mtu ambaye husema hivi anapokaribia kufa, ‘Laiti ningetumia wakati mwingi zaidi kazini.’” Pasipo shaka, maisha yenye kuridhisha na yaliyo na kusudi yanatia ndani kufanya kazi ya kimwili. Lakini si hayo tu. Yanatia ndani pia kutenga wakati wa kuwa pamoja na familia, kuwa na burudani, na kushughulikia mahitaji ya kiroho. Unaweza kutengaje wakati wa kushughulikia mambo hayo muhimu maishani kwa usawaziko?

Wakati wa Kazi, Wakati wa Kupumzika

Biblia inatuambia tufanye kazi kwa bidii ili kuandalia familia mahitaji yake. (Waefeso 4:28) Hata hivyo, inatuhimiza pia ‘tule, tunywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yetu yote iliyo ngumu.’ (Mhubiri 3:13) Kwa kweli, kufanya kazi kwa saa nyingi bila kupumzika vya kutosha au kuwa na burudani kunaweza kufanya tukose kufurahia mambo mengi maishani. Kunaweza pia kusababisha matatizo mabaya ya afya.

Kufanya kazi kupita kiasi kwa muda mrefu kumehusianishwa na kuwa mnene kupita kiasi, uraibu wa kileo, ugonjwa wa moyo, aksidenti kazini, matumizi mabaya ya dawa, wasiwasi, uchovu, kushuka moyo, na matatizo mengine mengi yanayohusiana na mfadhaiko. Kufanya kazi kupita kiasi kunaweza pia kusababisha kifo. Ripoti moja inakadiria kwamba nchini Japani, karibu watu 10,000 hufa kila mwaka kwa sababu ya kufanya kazi kupita kiasi, idadi ambayo inalingana na ya wale wanaokufa kutokana na aksidenti za barabarani kila mwaka nchini humo. Tatizo hilo ambalo limeitwa karoshi, yaani, “kufa kutokana na kufanya kazi kupita kiasi,” limeenea katika nchi nyingine pia.

Ona kwamba Biblia inashauri hivi kwa hekima: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:6) Kuwa na usawaziko ni muhimu sana. Usiruhusu kazi iwe uraibu wako. Tunza afya yako ya kiakili, kimwili, na kihisia kwa kutenga wakati wa kupumzika na kufurahia matunda ya kazi yako.

“Tunapaswa kufanya kazi ili tujiruzuku, si kufanya kazi kuwa ndilo jambo la maana maishani,” anasema Andrew, ambaye ana mke na watoto watatu. Kuwa na usawaziko kuhusu kazi na kuwa na pindi za kupumzika na burudani kutakusaidia pia kushughulikia mahitaji ya familia yako. Lakini si rahisi kufanya hivyo, hasa ikiwa una mahitaji ya kifedha.

Kusawazisha Kazi na Maisha ya Familia

Leo familia nyingi zina shughuli nyingi kupita kiasi na hazina wakati wa kuwa pamoja. Mwanamke mmoja huko Uingereza analalamika hivi: “Kazi huchukua nguvu zangu nyingi na watoto wangu hupata masalio.” Huko Marekani, kijana 1 kati ya 5 waliohojiwa alitaja kwamba “kutokuwa na wakati wa kutosha pamoja na wazazi” ndilo jambo linalowahangaisha sana vijana. Uchunguzi mwingine uliofanywa Marekani unaripoti kwamba, kwa wastani, wenzi wa ndoa ambao wanafanya kazi huzungumza pamoja kwa dakika 12 tu kwa siku.

Watu wengi sasa wanachunguza tena mambo wanayotanguliza na kufanya mabadiliko kwa kuwa wamechoshwa na mkazo wa kufanya kazi. Timothy, aliye na mke na watoto wawili wadogo, anasema hivi: “Nilikuwa nikifanya kazi baada ya saa za kazi, na mke wangu alikuwa akifanya kazi Jumamosi [Siku ya Posho] na Jumapili [Siku ya Yenga]. Tulionana mara chache sana. Mwishowe, tulichunguza tena maisha yetu na kubadili muda tuliotumia kazini. Sasa tuna furaha zaidi.” Brian, ambaye ni meneja wa duka anasema: “Kwa kuwa tulikuwa tukitarajia mtoto wetu wa pili, nilitafuta kazi ambayo ingefaa familia yangu. Nilikubali kazi ambayo ningelipwa mshahara unaopungua ule niliokuwa nikipata kwa dola 10,000 kwa mwaka, lakini kufanya hivyo kuliniruhusu nifanye kazi saa zinazofaa.” Melina aliacha kufanya kazi alipojifungua binti yake wa kwanza. Anasema: “Ilikuwa vigumu kutegemea mshahara mmoja tu, lakini mimi na mume wangu tuliona ingefaa nikae nyumbani na Emily badala ya kumpeleka kwenye kituo cha kuwatunzia watoto.”

Ingawa hivyo, lazima tutambue kwamba ni vigumu kwa familia nyingi kulipia gharama za kila mwezi. Wenzi fulani wa ndoa huwa na kazi mbili ili tu waweze kulipia gharama za lazima, na katika visa vingine, wazazi wote wawili hufanya kazi, na hivyo wao huwaacha watoto watunzwe na babu na nyanya yao au wanawaacha kwenye kituo cha kuwatunzia watoto.

Unaweza kupata njia nyingine za kusawazisha majukumu kazini na ya familia. Jambo muhimu ni hili: Usikose kufurahia maisha ya familia kwa sababu ya kukazia fikira sana kazi yako.

Uwe na hakika kwamba ukiwa na usawaziko kuhusu kazi yako, burudani, na mahitaji ya familia yako, utapata baraka nyingi. Katika makala ya mwisho ya mfululizo huu, tutazungumzia jambo muhimu zaidi ambalo litatusaidia kuwa na maisha rahisi yaliyo na usawaziko.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Usiruhusu kazi iwe uraibu wako

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 4:6

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Usikose kufurahia maisha ya familia kwa sababu ya kukazia fikira sana kazi yako

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

PESA AU MAPUMZIKO?

Wasomi fulani wa karne ya 20 waliamini kwamba maendeleo ya kiteknolojia yatawasaidia watu waache kufanya kazi zenye kuchosha na kuwaingiza kwenye “kipindi cha mapumziko yasiyo na kifani.”

Mwanzoni mwa miaka ya 1930, Profesa Julian Huxley, alitabiri kwamba wakati ujao, hakuna mtu atahitaji kufanya kazi kwa zaidi ya siku mbili kwa juma. Mfanyabiashara Walter Gifford alisema kwamba teknolojia itampa “kila mtu nafasi ya kufanya chochote anachotaka . . . , wakati wa kujifunza jinsi ya kufurahia maisha [na] kuwa na wakati mwingi zaidi wa kufanya mambo yanayoridhisha akili na moyo.”

Lakini namna gani tamaa ya watu ya kuwa na vitu vya kimwili? Mwanasosiolojia Henry Fairchild alidai kwamba “katika muda usiozidi saa nne kwa siku,” viwanda vitakuwa “vikitokeza bidhaa nyingi kuliko zile tunazohitaji.”

Je, matabiri hayo yalitimia kwa usahihi? Katika karne ya 20 na 21, kumekuwa na ukuzi mkubwa na wa haraka sana wa kiuchumi. Hilo lilipaswa kupunguza sana kazi ambayo watu wanafanya. Lakini kumetokea nini? John de Graaf anaandika hivi: “[Watu] wameamua kutumia uwezo huo wa ziada kujikusanyia pesa zaidi na vitu vya kimwili badala ya kupumzika. Kwa ufupi, tumechagua pesa badala ya wakati.”